Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Profesa Makame Mbarawa na Naibu Mawaziri wake wawili; Mheshimiwa Atupele Mwakibete na Mheshimiwa Godfrey Kasekenya kwa kazi kubwa wanazofanya kwenye kutengeneza mitandao ya barabara na ujenzi wa miundombinu mbalimbali nchi nzima.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utahusu umuhimu wa kujenga kwa lami barabara ya zamani ya Moshi - Arusha (Old Moshi Road) na changamoto za barabara katika jimbo langu la Moshi Vijijini.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa kwanza ni kuhusu umuhimu wa barabara ya zamani ya Moshi - Arusha (Old Moshi - Arusha Road). Hii ni barabara iliyokuwa imejengwa kwa lami toka wakati wa mkoloni. Kwa upande wa Arusha, kipande cha Mkoa wa Arusha kimeshajengwa na kinaendelea kukarabatiwa kwa kiwango cha lami (Kijenge hadi USA River). Kwa upande wa Mkoa wa Kilimanjaro, hakuna ambacho kimefanyika; kwa upande wa Moshi, barabara hii inaanzia keep left inakoanzia barabara ya Arusha kuelekea barabara ya International School kuelekea Daraja la Muitaliano, Magereza, Kwa Akwilini, Weruweru Sekondari kutokea Lambo Estate.

Mheshimiwa Spika, barabara hii ikitengenezwa, itakuwa ni ya mchepuko (bypass) kuingia na kutoka Mjini Moshi kama ilivyo ile ya USA River. Vilevile itakuwa ni ya msaada mkubwa kama kutatokea kikwazo cha aina yoyote ile cha magari kupita kwenye ile barabara kuu ya Arusha - Moshi.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa pili utahusu changamoto za barabara zinazojengwa na TANROADS Jimboni kwangu.

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo la Moshi Vijijini, barabara ya Kibosho Shine - Mto Sere inahudumiwa na TANROADS. Wameshaweka mitaro katika baadhi ya maeneo, na haijajengwa hata kidogo kwa kiwango cha lami. Barabara hii ni muhimu kwani ni sehemu ya kusafirisha watalii kwenda Mlima Kilimanjaro kupitia njia ya Umbwe. Tunaishukuru Serikali kwani kwenye bajeti ya mwaka 2023/2024 kupitia Mfuko Mkuu wa Serikali wamepanga kukarabati kilometa 2.1 za barabara hii kwa shilingi milioni 119.79.

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru Serikali kwa kuendeleza ujenzi wa barabara ya Kiboriloni - Kikarara - Tsuduni - Kidia kwa kiwango cha lami. Barabara hii inajengwa na TANROADS na bado haijakamilika. Mwaka 2023/2024 barabara hii imetengewa shilingi milioni 160.00 kutoka kwenye Mfuko wa Barabara.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kibosho Shine - Kwa Raphael - International School ilikuwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi toka mwaka 2005 na inajengwa na TANROADS lakini hadi leo haijakamilika. Bado kipande cha kama kilometa nane. Tunaishukuru Serikali kwani kwenye bajeti ya mwaka 2023/2024 Serikali imepanga kujega kwa kiwango cha lami kipande cha kilometa 0.9 kwa kutumia shillingi milioni 266.2 kwa kutumia Mfuko Mkuu wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Rau - Uru - Shimbwe yenye urefu wa zaidi ya kilometa 13 ilikuwa kwenye ahadi ya kujengwa kwa kiwango cha lami. Tunaishukuru Serikali kwani ujenzi umeanza na mwaka huu wa fedha wa 2023/2024 Mfuko Mkuu wa Serikali utajenga kwa kiwango cha lami urefu wa kilometa 1.1 kwa kiasi cha shilingi milioni 325.05, na Road Fund watakarabati kilometa 2.9 kwa kutumia shilingi milioni 105.00.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Uru - Kishumundu Parish - Materuni iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, kwa mpango wa kuijenga kwa kiwango cha lami. Tunaishukuru Serikali kwa kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami. Lakini mwaka huu wa 2023/2024 zimetengwa shilingi milioni 79.86 kukarabati kilometa 1.4, na mfuko wa barabara wametenga shilingi milioni 150.00 kuweka lami.

Mheshimiwa Spika, Kata ya Mabogini inakojengwa Hospitali ya Wilaya kuna changamoto kubwa ya ubovu wa miundombinu ya barabara. Hii inajumuisha barabara ya TPC - Mabogini - Kahe yenye urefu wa kilometa 11.4. Barabara hii imekuwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi toka mwaka 2010 ambapo waliahidi kuitengeneza kwa kiwango cha lami, lakini hadi leo ujenzi haujatekelezwa. Kwa kuwa iko chini ya TARURA na kwa kuzingatia bajeti finyu ya TARURA hadi leo ahadi hiyo haijatekelezwa.

Mheshimiwa Spika, ni kutokana na hali hiyo, nikiwa kama mwakilishi wa wananchi hawa nilipeleka ombi kwa Baraza la Maendeleo la Mkoa wa Kilimanjaro (RCC) kuipandisha hadhi na kuiombea ihudumiwe na Wakala wa Barabara (TANROADS). Ombi hili liliridhiwa na RCC na bodi toka mwaka 2021.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo ya hapo juu, naishauri Serikali ifanye yafuatayo; kwanza, naishauri Serikali iweke kwenye mipango kujenga barabara ya mchepuo (bypass) kwenye ilikokuwa barabara ya zamani ya Moshi - Arusha. Upande wa Moshi barabara hii inaanzia keep left ya Arusha kuelekea barabara ya International School kuelekea Daraja la Muitaliano, Magereza, Kijiji cha Eka, Kwa Akwilini, Weruweru Sekondari kutokea Lambo Estate.

Mheshimiwa Spika, pili, ninaiomba Serikali itenge fedha za kutosha na ianze kujenga kwa kiwango cha lami kipande cha barabara ya Kibosho Shine - Mto Sere kinachojengwa na TANROADS. Vilevile ninaishauri Serikali ifikirie kujenga kwa kiwango cha lami kipande cha Sere hadi gate la Umbwe la kupanda Mlima Kilimanjaro. Barabara hii ni mbovu mno pamoja na kwamba hutumika kusafirisha watalii wanaopanda Mlima Kilimanjaro kupitia njia ya Umbwe na kuingizia Serikali kipato kupitia sekta ya utalii.

Mheshimiwa Spika, tatu, ninaiomba Serikali itenge kiasi cha fedha za kutosha na kukamilisha ujenzi wa barabara ya Kiboriloni - Kikarara - Tsuduni - Kidia kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, nne, ninaiomba Serikali ikamilishe ujenzi wa barabara ya Kibosho Shine - Kwa Raphael - International School kwa kiwango cha lami kama ilivyoainishwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi toka mwaka 2005. Ujenzi wa barabara hii umechukua zaidi ya miaka 13.

Mheshimiwa Spika, tano, ninaishauri Serikali itenge fedha za kutosha na kukamilisha ujenzi wa barabara ya Rau - Uru - Shimbwe kwa kiwango cha lami yenye urefu wa zaidi ya kilometa 13 kama wananchi walivyoahidiwa wakati wa kampeni.

Sita, ninaishauri Serikali itenge fedha na kukamilisha ujenzi wa barabara ya Uru - Kishumundu - Materuni.

Mheshimiwa Spika, saba, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi iingize barabara ya TPC - Mabogini - Kahe yenye urefu wa kilometa 11.4 kwenye mtandao wa TANROADS kwani RCC na bodi walikubaliana na ombi hili toka mwaka wa 2021. Ninaiomba Serikali itenge fedha za kutosha na ujenzi wa barabara hii uanze mara moja kwani Hospitali ya Wilaya inajengwa eneo hili.

Mheshimiwa Spika, baada ya ushauri nilioutoa hapo juu, naunga mkono hoja.