Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, niungane na Watanzania wenzangu wote kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia baraka zake katika nyanja mbalimbali sisi Watanzania wote na Taifa letu kwa ujumla, sisi kama Taifa hatuna cha kumlipa muumba wetu zaidi ya maombi na sala kila wakati.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kuungana na wananchi wa Jimbo langu la Mbulu Mjini kumpongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali nzima ya Awamu ya Sita kwa jinsi tunavyotekeleza Ilani ya CCM ya mwaka 2020-2025 kwa kila sekta, tuendelee kuiombea Serikali yetu amani, upendo, mafanikio na mshikamano kwa Mwenyezi Mungu wetu.

Mheshimiwa Spika, kwa moyo wangu wa dhati nachukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Profesa Makame Mbarawa Waziri wetu wa Ujenzi, Naibu Mawaziri wote wawili, Mheshimiwa Balozi Asha – Katibu Mkuu Ujenzi, Mheshimiwa Joseph Migire, Katibu Mkuu - Uchukuzi, Naibu Makatibu Wakuu wote, Wakurugenzi wote wa Wizara, Ndugu Rogatus Mativila - Mtendaji Mkuu wa TANROADS na timu yake ya watendaji wote makao makuu na Meneja wa Mkoa wa Manyara kwa jinsi wanavyotekeleza majukumu yao na kutusikiliza changamoto zilizoko kwenye majimbo yetu na kuzitatua kwa kadri ilivyowezekana.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba kutoa mchango wangu kupitia mapendekezo ya bajeti ya Wizara hii muhimu sana kupitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri ambayo imewasilishwa katika Bunge letu na taarifa ya Kamati yetu ya kudumu ya miundombinu.

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu kupitia Wizara ya Fedha ijitahidi kutoa fedha za malipo ya wakandarasa wanaojenga miradi ya barabara na miundombinu mbalimbali ya ujenzi kwa wakati ili kuepuka gharama za malipo zinazoongezeka nje ya mikataba na wananchi kupokea huduma iliyotarajiwa kwa mujibu wa mikataba.

Pia Serikali iangalie utaratibu wa kuongeza bajeti ya dharura kwa Wakala wa Barabara TANROADS kwa ajili ya madhara yanayosababishwa na mabadiliko ya tabianchi hali inayofanya barabara nyingi kujifunga na kuleta adha kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, Serikali itusaidie mpango kabambe wa kujenga kilometa tano za zege katika barabara ya Mbuyu wa Mjerumani – Magara - Mbulu sehemu ya Mlima Magara kwa kuwa mpango wa zege katika eneo la Mlima Magara imekuwa ahadi ya viongozi wetu wakuu kutoka Serikali ya Awamu ya Nne, Tano na Sita. Hivyo basi eneo hilo ni hatarishi sana na matengenezo yake yamekuwa na gharama kubwa yasiyo na tija.

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru sana Serikali yetu kwa mpango wa ujenzi barabara ya Karatu, Mbulu, Haydom, Maswa, Sibiti. Tunaiomba Serikali mkataba wake usainiwe haraka kwa kuwa ni kiu ya wananchi wa majimbo yote sita katika mikoa ya Arusha, Manyara, Singida, Simiyu mpaka Shinyanga. Mradi huu utagusa sana hisia ya wananchi walio wengi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja na naomba kuwasilisha.