Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha uendelezaji wa miradi ya kimkakati na pia utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (national competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha miezi kumi ya bajeti inayoishia Juni, 2023 Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano imetekeleza miradi mingi ya miundombinu ya barabara, reli, bandari na uimarishaji wa safari za anga ikiwemo ujenzi na uboreshaji wa viwanja vya ndege. Naipongeza Serikali kwa hatua nzuri za utekelezaji wa mradi wa kihistoria wa ujenzi wa reli ya kisasa ya SGR pamoja na uboreshaji wa bandari utaimarisha kwa kiasi kikubwa uchumi wa nchi yetu. SGR na bandari ni nguzo imara ya kiushindani katika biashara ya usafirishaji wa ndani na nchi za Maziwa Makuu na hata za Kusini mwa Afrika na Kati. Bandari za Tanzania ni lango la usafirishaji kwa Zambia, Malawi, DR Congo, Uganda, Burundi, Rwanda, Sudan ya Kusini na hata Zimbabwe na Msumbiji.

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya kazi kubwa kuhakikisha ujenzi wa SGR unaendelea kwa kasi ile ile na pia napongeza jitihada za kuendelea kutafuta vyanzo vya fedha vya masharti nafuu kugharamia ujenzi huo. Pamoja na ujenzi wa reli ya kisasa, Serikali imefanya maboresho makubwa ya miundombinu na huduma katika bandari zetu hususana bandari ya Dar es Salaam ili kukabiliana na ushindani mkubwa wa bandari zingine za ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika. Bandari ya Dar es Salaam inakumbana na ushindani mkubwa toka bandari za Mombasa (Kenya), Beira (Msumbiji), Nacala (Msumbiji), Durban (Afrika Kusini), Lobito (Angola) na Walvis Bay (Namibia). Maboresho ya bandari zetu iendane na kuondoa changamoto zingine ambazo zinasababisha gharama kubwa za usafirishaji kwa bandari zetu na kusababisha kupoteza biashara ya usafirishaji kwa bandari shindani. Ufanisi wa bandari unategemea pia maboresho ya barabara, Reli ya Kati (TRL), Reli ya TAZARA, utendaji wenye tija wa wadau wote wa bandari na hata watumishi ili kupunguza gharama za usafirishaji kwa wateja wa bandari zetu.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa karibu asilimia 70 ya mzigo wote wa nchi za nje unasafirishwa kwa kupitia Dar es Salaam Corridor ambapo DR Congo ni asilimia 38, Zambia asilimia 26, na Malawi asilimia 6. Pamoja na fursa za kijografia ya bandari zetu, mzigo unaopita sasa kwenye bandari ya Dar es Salaam, ni chini ya asilimia 50 ya biashara yote ambayo kwa sasa sehemu kubwa inashikiliwa na bandari shindani.

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa za kiushindani zinatokana na ufanisi usiokidhi ushindani na gharama kubwa za bandari na watoa huduma wa Bandari ya Dar es Salaam. Pia kuna changamoto za kiutendaji kwa mashirika ya reli ya TAZARA na hata reli ya kati (TRL) inayopelekea gharama kubwa ambazo siyo za kiutendaji, kwa ajili ya kunusuru biashara hii inayopotea kwa bandari shindani, Serikali ichukue hatua za haraka kuboresha huduma za TAZARA ikiwa ni pamoja ya maboresho ya miundombinu ya reli, ununuzi wa vichwa vya treni, mabehewa na vitendea kazi vingine.

Mheshimiwa Spika, napendekeza Serikali kwa haraka ishughulikie maboresho ya Mkataba wa TAZARA na kisha kufuta fedha ya masharti nafuu angalau kiasi cha shilingi bilioni 200. Katika kipindi hiki cha ushindani mkubwa na hata mfumuko wa bei wa mafuta ya petroli, mbolea na bidhaa mbalimbali, usafirishaji wa reli ni mojawapo ya suluhisho kubwa kupunguza mzigo wa bei kubwa kwa wateja wa bandari zetu na hata wananchi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na maboresha ya reli ya TAZARA, napendekeza kuendelea na ujenzi wa Bandari Kavu Mbeya ambayo ina fursa kubwa katika kipindi hiki katika kuwezesha kupunguza gharama za kusafirisha kwa wateja wa bandari na hata kupunguza bei za mafuta ya petroli, pembejeo na mazao ya kilimo. Bandari Kavu ya Mbeya ni njia panda kwa wateja wa nchi za Malawi, Zambia, DRC Lubumbashi na hata kwa Zimbabwe na Msumbiji. Serikali ichukue hatua za haraka kuinusuru reli ya TAZARA hata ikibidi kurekebisha mikataba ya umiliki na uongozi ili mradi iendeshwe kwa tija. Kuna kuchukua hatua za makusudi kwa kutumia zaidi TAZARA kusafirisha mizigo ambayo imeelemea hata uwezo wa barabara zetu.

Mheshimiwa Spika, usafirishaji wa mizigo kwa kutumia TAZARA ilenge kupunguza gharama za mafuta ya petroli, pembejeo kwa wakulima na wakati huo kupunguza gharama za kusafirisha mazao ya wakulima. Pamoja na kuboresha TAZARA, napendekeza kukamilisha taratibu za ujenzi wa Bandari Kavu ya Mbeya ambapo Mamlaka ya Bandari kwa kipindi kirefu wamewahakishia wananchi kulipa fidia ya eneo lao wanalolichukua.

Mheshimiwa Spika, napendekeza Bandari ya Dar es Salaam kuingia makubaliano na TAZARA na TRL ili iweze kumiliki mabehewa yake kwa lengo la kuongeza ufanisi na kupunguza gharama ambazo sio za kiushindani. Pamoja na hatua hiyo, kuna fursa kubwa ya kutafuta mwekezaji mwenye uzoefu mkubwa ikiwemo mtandao wa bandari kwa lengo la kuboresha utendaji hasa kwenye upande wa makontena. Serikali ifanye jitihada ya kupata mwekezaji ikiwemo kwa mfumo wa PPP kwa lengo la kuongeza biashara ikiwemo kurudisha biashara iliyopotea kwa bandari shindani.

Mheshimiwa Spika, kwa siku za hivi karibuni kuna mahitaji makubwa ya kusafirisha makaa ya mawe kwenda soko la nje na pia uingizwaji wa Sulphur kutoka nje lakini imepelekea kuthibitisha upungufu mkubwa wa gari kubwa hasa aina ya tiper. Upungufu huu unapelekea kuzorota kwa ufanisi wa huduma ya bandari.

Mheshimiwa Spika, napendekeza Serikali iendelee na mkakati wa kutafuta mwekezaji wa Bandari ya Mbegani – Bagamoyo ambayo ina lango lenye kina cha asili cha mita 18 na haina kikomo cha upana wa meli ambazo zinaweza kuingia na kutoka bandarini hapo. Kutokuwepo kwa ukomo katika lango, bandari hiyo inaweza kuhudumia meli ambazo zinahudumiwa kwenye bandari kubwa duniani zenye urefu wa mita 400 na uwezo wa kubeba makasha hadi TEUs 22,000. Aidha, uwezo huu ni mkubwa katika eneo la Afrika Mashariki na Kati kwani kwa sasa hakuna bandari yenye uwezo kama huo. Hivyo, uendelezaji wa Bandari ya Mbegani, Bagamoyo utasaidia kupunguza msongamano wa shehena katika Bandari ya Dar es Salaam na kupelekea bandari zote kuwa shindani.

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto za mfumuko wa bei za mafuta na pembejeo, kuna fursa kubwa na hasa mahitaji makubwa ya mazao ya kilimo kwa soko la ndani na nje. Uzalishaji kwa tija unategemea kwa kiasi kikubwa ubora wa miundombinu ya barabara, reli na hata anga. Serikali iweke msukumo zaidi kwenye kuboresha miundombinu ya barabara ili kurahisisha usafirishaji wa pembejeo na mazao ya kilimo. Kutokana na fursa za uzalishaji mkubwa kwa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, napendekeza mwendelezo wa uboreshaji wa barabara za TANZAM kipande cha Igawa - Tunduma; barabara ya bypass ya Uyole - Songwe; barabara ya bypass ya Iwambi - Mbalizi; barabara ya Mbalizi – Shigamba – Isongole kutokana na uzalishaji wa mazao ya kilimo; barabara ya Mbalizi – Galula – Makongorosi kutokana na uzalishaji mkubwa wa mazao ya kilimo na madini; na pia barabara ya Isyonje – Kikondo – Makete ambayo ni muhimu sana katika kusafirisha mazao ya kilimo ikiwemo maua, parachichi na viazi kwa soko la nje.

Mheshimiwa Spika, uboreshaji wa barabara hizi pamoja na uwanja wa ndege wa Songwe ni muhimu sana kwa usafirishaji wa mazao yetu kwa soko la ndani na nje, na kwa kiasi kikubwa utaongeza mapato ya fedha za kigeni. Maboresho ya uwanja wa ndege wa Songwe uende sambamba na ujenzi wa maghala mahususi wa maua, mbogamboga, parachichi, nyama, viwanda vya kuengeza thamani za mazao na madini, na EPZ/Industrial Park.

Mheshimiwa Spika, kutokana na ajali za mara kwa mara za Mlima Iwambi, Mbalizi na msongamano wa magari yakiwemo malori ya mizigo na mafuta ya petroli, tunashukuru kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuchukua hatua za haraka kuanza ujenzi wa barabara ya njia nne kwa barabara ya TANZAM kipande cha Uyole mpaka Uwanja wa Ndege wa Songwe. Katika vipindi mbalimbali, viongozi wa Kitaifa waliagiza upanuzi wa kipande hiki cha TANZAM pamoja na ujenzi wa bypass ya Uyole – Songwe kilometa 40 na bypass ya Mbalizi – Iwambi kilometa 6.5. Ujenzi wa barabara hizi utanusuru wananchi kuendelea kupoteza maisha kwa ajali za mara kwa mara katika eneo hilo. Hatari zaidi ni kwa magari makubwa yanayosafirisha mafuta kupita barabara yenye msongamano mkubwa katikati ya Jiji la Mbeya. Msongamano wa magari makubwa katika barabara ya TANZAM ni sehemu ya changamoto zinazopelekea bandari zetu kupoteza biashara kwa bandari shindani.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.