Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nianze kuishukuru Wizara kwa sababu nimepitia na nimeona asilimia kubwa naona Mkoa wa Songwe kwa sehemu tumeguswa kwenye bajeti hii. Kwa hiyo niwapongeze kwa kweli na sisi Wanasongwe tunaona bajeti hii imetugusa kwa sehemu, kwa sababu ukiona kutoka Barabara ya Mbarizi mpaka Mkwajuni tumetengewa kilometa 86, siyo kidogo; japo bado lakini naamini wataendelea kutufikiria zaidi na zaidi.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia kwenye Barabara ya Mlowo mpaka Kamsamba kilometa 50 wametutengea. Ukiangalia Barabara ya Mpemba mpaka Ileje, kilometa 50 na maeneo mengine wametugusa. Niombe tu kwamba bajeti hii tunaomba iwe inatekelezeka na itekelezeke kweli kwa sababu Wanasongwe tumetegemea hasa kwa sababu asilimia kubwa barabara hizi ni barabara za kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo bado tuna changamoto kwenye maeneo mengine kwenye barabara hasa ukizingatia Barabara ya kutoka Mlowo inayopita Isansa – Magamba mpaka Mkwajuni. Tunaomba Wizara waliangalie hili. Barabara hii tumekuwa tuna changamoto kubwa sana hasa kwa wananchi wa Wilaya ya Songwe. Tumeendelea kulizungumza mara nyingi, wananchi wa Wilaya ya Songwe hapo wanapohitaji huduma za mkoa inawalazimu kwenda kupitia Mkoa wa Mbeya. Wakitoka Mkoa wa Mbeya ndiyo wanapata usafiri mwingine kuelekea Mkoani Songwe. Kwa hiyo tuombe Serikali waliangalie jambo hili kuweza kututengenezea barabara ya kutoka Mlowo itakayopita Isansa – Magamba mpaka Mkwajuni ili kurahisisha huduma kwa wananchi wa Wilaya ya Songwe.

Mheshimiwa Spika, pia kuna barabara nyingine ambayo pia imekuwa ni changamoto ni Barabara ya kutoka Chapwa inayopita Chindi mpaka Chitete. Tunaomba barabara hii Wizara iiangalie. Tunajua jinsi wananchi wa Momba ambavyo wanajishughulisha na shughuli za kilimo, ufugaji na mambo mengine. Tunaomba barabara hii waikumbuke kwenye bajeti zao ili tuweze kuwakomboa na kuwarahisishia huduma wananchi wa Wilaya ya Momba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, naomba nizungumzie, ni kweli tunatenga bajeti sana kwenye Wizara hii, lakini tunaona changamoto kubwa miradi mingi inachelewa kutekelezeka na kuchelewa kutekelezeka kwa miradi kunapelekea miradi mingi kuongezeka gharama. Gharama za miradi zinaongezeka kutokana na miradi mingi kuchelewa kutekelezeka. Tunaomba Wizara iliangalie hili ili mwisho wa siku tusiwe tunatumia fedha nyingi kwa ajili ya mradi ambao pengine unaweza kutekelezeka kwa fedha kidogo na fedha zingine zinaweza kusaidia kwenda kwenye maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna jambo lingine la wakandarasi kuchelewa kulipwa malipo yao. Tumeona sisi sote kwenye taarifa hata zilizopita wakandarasi wanavyocheleweshwa kulipwa malipo yao mara nyingi imetokea faini kwa Serikali, tunalipa fedha nyingi kwa sababu ya kuchelewesha malipo ya wakandarasi. Tunaomba Wizara iliangalie, tumeona maeneo mengi wakandarasi wanachelewa kukabidhi miradi, lakini hatuoni wao wakilipa zile asilimia ambazo wanatakiwa kukatwa pale wanapokuwa wamechelewesha mradi. Kwa hiyo tunaomba Wizara pia iliangalie hili ili tuende kwa usawa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, naomba nizungumzie suala la bandari kavu ndani Mji wa Tunduma. Sisi sote tunajua 70% ya mizigo yote inayoshuka katika Bandari ya Dar es Salaam inapita ndani ya Mji wa Tunduma na tumeendelea kusema, tumezungumza sana, tunaomba Serikali waangalie umuhimu wa kujenga bandari kavu ndani ya Mji wa Tunduma ili kurahisisha huduma.

Mheshimiwa Spika, wote tunajua ya kwamba Tunduma ni lango kuu la SADC. Mkoa wa Songwe ni lango kuu la SADC, Wizara iangalie umuhimu wa kujenga bandari kavu. Sisi sote tunajua nchi yetu na maeneo mengine tuko katika ushindani wa kibiashara. Wizara izingatie na iangalie umuhimu wa kujenga bandari kavu ndani ya Mji wa Tunduma ili kurahisisha huduma na wakifanya hivi na wote wanajua kabisa Halmashauri ya Mji wa Tunduma tayari imejitahidi kwa sehemu yake kuhakikisha inapambana kupata zaidi ya ekari 2,000 kwa ajili ya kujenga bandari kavu ndani ya Mji wa Tunduma. Tunaomba Serikali waliangalie hili kwa umuhimu wake ili kuhakikisha Halmashauri ya Mji wa Tunduma inajengwa bandari kavu kama eneo la lango kuu la SADC na hiyo itakuwa imerahisisha huduma sana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie jambo lingine ambalo ni suala la Uwanja wa Kagera, Uwanja wa Ndege. Wote tunajua changamoto ambazo zimeendelea kutokea Kagera. Tumeona maafa, tumeona wananchi wamepoteza maisha, tumeona na changamoto hizi zinasababishwa na hali ya hewa.

Mheshimiwa Spika, niombe Serikali ione umuhimu wa kujenga uwanja mwingine mpya ndani ya Mkoa wa Kagera, kwa sababu sisi sote tunajua kuna uhitaji mkubwa wa usafiri wa anga kwenye Mkoa wa Kagera. Hebu Wizara waliangalie hili na waone umuhimu wa kujenga uwanja mpya ili kuepusha maafa zaidi yanayoweza kutokea kwenye Mkoa wa Kagera. Wananchi wetu tunawahitaji na huduma tunahitaji zitolewe, tena huduma zilizo sahihi zaidi. Wizara ione umuhimu wa kujenga uwanja mpya ndani ya Mkoa wa Kagera ili tuweze kurahisisha huduma kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nizungumzie suala la ATCL. Wamezungumza wengi sana, naomba niishauri Wizara, naomba niishauri Serikali, ni kweli watu wamezungumza sana ATCL, lakini Serikali ione namna gani ya kulisaidia Shirika la ATCL ili lisiweze kuingia hasara kama tunavyoiona sasa. Kwa asilimia kubwa naona hata Serikali wanasababisha shirika hili kuendelea kudidimia. Nasema hivyo kwa sababu Serikali wameikodishia ndege ATCL, ndege zinakamatwa lakini ATCL bado inaendelea kuwalipa Serikali. Serikali ikae chini ijitafakari na wao watakuwa ni sehemu ya kulididimiza hili shirika. Serikali iangalie namna ya kuisaidia ATCL ili iweze kuinuka kutoka mahali ilipo kwenda eneo lingine.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Ahsante. (Makofi)