Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Charles Muguta Kajege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mwibara

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia hotuba hii ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi. Vile vile kama ilivyokuwa kwa watangulizi wangu, napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambayo anaifanya. Nataka niwahakikishie Watanzania kwamba kazi ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ndio ameianza, Watanzania tutegemee makubwa huko mbeleni tutakapokwenda. Pia, nachukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Mawaziri wa Wizara hii kwa utendaji wao wa kazi nzuri ambazo wanafanya mpaka muda huu. Wameweza sasa hivi kuifanya Tanzania ipitike kwa urahisi angani, ardhini na majini, nawapongeza sana. Lakini vile vile nampongeza Engineer Mativila Mtendaji Mkuu wa TANROADS na Meneja wa TANROADS Mkoa wa Mara Engineer Maribhe kwa kazi nzuri sana ambayo wamefanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naipongeza tena Wizara hii kwa kuweza kukamilisha ujenzi wa Barabara ya Nyamuswa – Bunda - Bulamba – Kisole kwa kiwango cha lami. Kwa sasa tunasafiri na kusafirisha mizigo yetu kwa raha mustarehe, nawashukuru sana. Vilevile naishukuru Wizara kwa kupanga kukamilisha vipande vya barabara kati ya Kibara na Kasaunga na pia Kisole na Kisole Kivukoni kwa kiwango cha lami. Ukamilishaji wa vipande hivi utasaidia kuunganisha barabara nzima kutokea Kisorya mpaka Nyamuswa kwa kiwango cha lami, nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile nitumie fursa hii kuiomba Wizara sasa kuipandisha hadhi Barabara ya Kisambala…

MHE. BONIPHANCE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. CHARLES M. KAJEGE: … Mugala na Musoma Vijijini. Barabara hii ina traffic kubwa sana ya watu pamoja na mizigo, na vile vile barabara hii ni shortcut ya watu waendao Musoma na vile vile watokao Musoma kwenda sehemu za Ukerewe naomba sana Wizara ifike kupandisha barabara hii.

SPIKA: Mheshimiwa Kajege, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Getere.

TAARIFA

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nilikuwa nataka kumpa taarifa mzungumzaji kwamba wakati anazungumza barabara ya ile ya kuunganisha Kisorya, amesahau kusema barabara ya kutoka Balili kwenda Mugeta nayo inapaswa kuunganisha.

Mheshimiwa Spika, ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Kajege, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, huyo ni Comrade, naipokea taarifa yake. Kuna changamoto ambazo bado Wizara inatakiwa kuzitatua ili kuweza kufanikisha malengo ya Serikali yetu. Kwa mfano, kuna Shirika la Air Tanzania Limited, shirika hili limekodisha ndege kutoka Shirika la TGFA, lakini nikiangalia kwa sababu nimepata bahati kwamba nipo katika Kamati ya PIC, na Viongozi Wakuu wa ATCL wamekuwa wanakuja katika Kamati yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini katika kuangalia tumekuta kwamba tatizo kubwa katika ATCL ni mkataba kati yake na TGFA, mkataba huu kwa kweli si rafiki. Ninaiomba sana Serikali iuangalie tena mkataba huu ili uweze kufanywa kuwa rafiki. Lakini tatizo lingine katika ATCL ni madeni iliyorithishwa, madeni hayo hayalipiki. Ningeomba Serikali iangalie namna nyingine ya kuweza kuchukua madeni haya. Vilevile kuna mwingiliano mkubwa wa Serikali kuipatia ATCL namna ya kufanya kazi, yaani waliache sasa Shirika la ATCL lifanye kazi kibiashara, lihudumie njia zenye faida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano siku moja nilikuwa Mwanza, ndege ya ATCL ilikuwa inatoka Chato. Ndani ya ile ndege nilipoingia niliikuta ina abiria watatu lakini utakuta abiria wengi wapo hapa Dodoma wanasubiri ndege za ATCL kuweza kuwasafirisha. Ningeomba sana Serikali iliache Shirika hili liweze kufanya kazi yake ya kibiashara.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ni utitiri wa vituo bubu vya ukaguzi wa malori na mizigo katika barabara zetu. Ukitoka Dar es Salaam mpaka kufika Tunduma kuna vituo bubu zaidi ya 100. Haya malori yenye mizigo yakitoka Bandarini yanasimamishwa kila sehemu, yanakaguliwa kila sehemu na wakati mwingine yanchukua muda mrefu. Mfano mmoja siku moja nilikutana na dereva mmoja ambaye alikuwa anatoka Dar es Salaam kwenda Tunduma saa mbili nikamkuta akiwa amesimamishwa pale Kibaha lakini wakati narudi saa 12 jioni kutoka Morogoro nilimkuta bado amesimama pale. Wahusika walikuwa wanadai kwamba kuna cheti ambacho kilikuwa kimesainiwa lakini aliyekuwa amekisaini yuko kwenye mkutano. Kwa hiyo hakumruhusu huyo dereva aendelee na safari mpaka tena wapate aliyesaini kile cheti (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi vituo ni mojawapo ya vikwazo vikubwa sana vya biashara kati ya Tanzania na nchi zingine, lakini vile vile ni chanzo vile vile cha kuwafanya watumiaji wengine wa bandari zetu washindwe kutumia bandari yetu. Kwa hiyo, naomba Serikali iangalie sana hivi vituo bubu, ikiwezekana viondoke vyote vinafanya nini? Kama mizigo ikishakaguliwa bandarini kwa nini iendelee tu kukaguliwa tena njiani? Itakaguliwa kule mwishoni. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, katika jimbo langu kuna Kivuko cha Mugala - Musoma Vijijini ni kibovu, hiki kivuko kimekuwa ni kibovu kwa muda mrefu. Wananchi wanaotaka kusafiri kwenda Musoma Vijijini na wanaotoka Musoma Vijijini kuja Jimboni kwangu Mwibara wanapata tabu sana. Naomba sana Serikali sasa ikamilishe ukarabati wa hicho kivuko.

Mheshimiwa Spika, kingine ni tunahitaji kivuko kwenda katika Kisiwa cha Nafuba. Kisiwa hiki kina watu wengi sana na ni kikubwa sana, watu wengi mahitaji yao wanachukua katika nchi kavu huku. Kwa hiyo, ningeomba sana Serikali sasa iweze kutafuta kivuko kwa ajili ya kusafirisha wananchi kwenda Nafuba na kuja sehemu zingine za Jimbo la Mwibara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo jingine liliopo ni vibali vya kusafirisha mitambo ya ujenzi, kwa mfano inapotokea mkandarasi anataka kusafirisha mtambo mmoja kwenda katika mkoa mwingine kibali lazima akipate kutoka Dodoma. Hiyo inachukua muda mrefu sana kuweza kupata hivi vibali, inapoteza muda wa biashara na inakuwa kabisa ni usumbufu mkubwa, naomba kuwa na decentralization ya kutoa hivi vibali vya kusafirisha mitambo ya ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ni malipo ya waliopisha Mradi wa Barabara ya Bulamba – Kibara – Kisorya. Barabara hii imeshakamilika muda mrefu lakini wahusika bado hawajalipwa. Jana wakati natoa taarifa kwa mzungumzaji mmoja niliomba Serikali iingilie kati kuweza kuwalipa wahusika fidia zao ili na wao waweze kuendesha maisha yao vizuri.

Mheshimiwa Spika, kwa kusema haya machache naomba niunge mkono hoja hii na nawapongeza sana Wizara na Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri. Ahsante sana. (Makofi)