Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuchangia Wizara hii muhimu. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa afya na nguvu kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa.

Mheshimiwa Spika, nianze kwanza kupongeza, Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yako, mnafanya kazi nzuri mimi nimekuwa Mwanakamati wa Wizara yako, hivyo ninajua kazi nyingi na kubwa unazozifanya. Wewe pamoja na timu yako tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nianze kuongelea barabara zangu, Barabara ya Mlushaka kwenda mpaka Murongo; Mheshimiwa Waziri umeandika mwenyewe na hayo umeyasoma mbele ya Bunge, Barabara ya Mlushaka kwenda mpaka Mrongo itasainiwa kabla ya Mwezi wa Saba. Barabara ya Mgakorongo kwenda mpaka Murongo umeahidi itasainiwa kabla ya Mwezi wa Saba. Mheshimiwa Waziri ninakuheshimu sana na nisingependa niongee maneno magumu. Maneno haya umeyasema ndani ya Bunge hili na umeyasema mbele ya Mungu na Mungu amesikia. Niombe sana, hakuna cha kusainia Dodoma, barabara hii ikasainiwe Kyerwa ili Wanakerwa waone kazi kubwa ambayo anaifanya Mama Samia lakini pia waone kazi kubwa anayoifanya Mbunge wao ambaye amekusumbua mara kwa mara. Kwa hiyo ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri uzingatie, tunapomaliza bajeti twende Kyerwa tukasaini barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine kwa upande wa barabara, mimi nipongeze sana Meneja wetu wa Mkoa anafanya kazi nzuri sana. Kijana huyu ni mtulivu na ni msikivu sana. Lakini bajeti ambayo inatengwa kwa Mkoa wa Kagera ni ndogo. Mkoa wa Kagera una vipindi virefu vya mvua, takriban miezi saba yote tuna vipindi vya mvua. Kwa hiyo unakuta barabara za Mkoa wa Kagera hazipitiki kwa sababu bajeti inayotengwa ni kidogo sana. Kwa hiyo niombe sana Mheshimiwa Waziri mnapokuwa mnatenga bajeti angalieni hii mikoa ambayo ina changamoto ya vipindi virefu vya mvua ili iweze kupewa bajeti na barabara ziweze kupitika hasa hasa zile barabara za udogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee suala la uwekezaji kwenye bandari. Bandari yetu mimi niseme ndio moyo wa Taifa, lakini bandari hii ni lango kwa nchi zinazotuzunguka kwa sababu ya umuhimu wake. Hakuna nchi ambayo inatuzunguka haihitaji Bandari ya Dar es Salaam. Lakini bado mimi niseme sijaona nguvu kubwa na juhudi kubwa ambazo mmeziweka kama Serikali kuhakikisha bandari hii inaleta tija katika Taifa letu. Leo hii kila Mbunge anayechangia hapa anaomba maji, anaomba barabara, anaomba umeme na mambo mengine lakini tunachokitega uchumi kimekaa tu. Sasa niombe sana Mheshimiwa Waziri kelele hizi achana nazo. Mimi ninaamimi Serikali kwa kipindi ambacho mmekaa na TICTS mmejifunza mambo mengi, mmeona mapungufu yaliyokuwepo, wapi kama Serikali walikosea sasa ni wakati wa kutafuta mwekezeji ili tuingie ubia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ninaamini ndugu zangu kuna wengine wameshauri wanasema Serikali iwekeze, hivi tutawekeza kwenye vitu vingapi? Na mwisho wa siku tutakachoenda kukifanya lazima tuende kukopa. Leo hii tumekopa kwa ajili ya Mradi wa Mwalimu Nyerere, tumekopa kwa ajili ya SGR na miradi mingine. Tukiendelea kukopa mwisho wa siku yatatokea mambo mengine ambayo tunayasikia kule Kenya. Sasa niombe sana Mheshimiwa Waziri simama imara pamoja na timu yako, tunaamini yule kijana, Mkurugenzi wa Bandari yuko vizuri sana na tumeanza kuona maboresho ambayo ameyafanya. Sasa msije mkasema mambo hayafanyiki, hayafanyiki kwa sababu bado hatujaweza kuwekeza vya kutosha. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana wekeza hapo nguvu tafuta mtu ambaye anafaa tuwekeze ili bandari yetu hii iweze kuinua uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii tumejenga SGR na wanafanya vizuri sana, nimpongeze sana Mkurugenzi wa TRC, anafanya kazi nzuri, amesimia miradi inakwenda vizuri. Lakini SGR hii mnategemea ni ya kubeba abiria? Hii si ya kubeba abiria ili tuweze kupata faida na SGR lazima tuwe na mzigo utakaotoka nje na kuingia. Kwa hiyo niombe sana Serikali iendelee kuweka nguvu ili tuone faida ya kujenga SGR. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana, hili usimame imara, vita ya kiuchumi inahitaji kujikunja, inahitaji kuwa imara. Ukizubaa kidogo tu kelele hizi zinazopigwa usifikiri watu wanapiga kelele kwa sababu wanakutakia mafanikio. Jambo ambalo tunashauri sisi kama Wabunge tuombe sana hii timu ambayo inatafuta mtu wa kuwekeza ijipange vizuri, tutafute wanasheria ambao ni wazuri. Huyu mwekezaji tutakaye mleta atakaposhindwa pawepo na vifungu ambavyo vitambana akishindwa aondoke, lakini lazima tuweke nguvu sana kwenye bandari yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi niendelee sana, nirudie sana kumpongeza sana Mheshimiwa Rais anafanya kazi kubwa, na mmesikia Waheshimiwa Wabunge bado hajaona faida, na ninyi Wabunge ni mashahidi, bado hatujaona faida kwenye banda hili. Sasa Mheshimiwa Rais kama ameliona hilo leo hii wanaleta wazo la kuwekeza, kwa nini tusiā€¦

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Bilakwate kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Festo Sanga.

TAARIFA

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, nataka kumpa taarifa mzungumzaji kwamba amezungumzia utendaji wa Bandari ya Dar es Salaam kwamba ni mzuri na ni kweli ni mzuri na kwenye ripoti iliyotoka leo ya World Bank inaonesha kabisa Bandari ya Dar es Salaam ndiyo inaongoza sasa kwa Afrika Mashariki kufanya kazi vizuri ikiwa ni bandari ya 312 na wenzetu wa Mombasa wako 326, tumeshawapiku. Kwa hiyo, ni kazi nzuri ambayo anafanya Mkurungenzi wa Bandari, Ndugu Mbossa tunampongeza sana sana kwa kile anachokifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

SPIKA: Mheshimiwa Bilakwate unaipokea taarifa hiyo?

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo naipokea na mimi naendelea kumpongeza lakini ili tumpongeze zaidi lazima tulete uwekezaji ambao una tija na tuone matunda ya bandari yetu.

Mheshimiwa Spika, niendelee kusema ndugu zangu, kazi hii inayofanyika katika Taifa hili mnaona uwekezeji mkubwa tulionao, ukienda kwenye umeme, ukiangalia miradi ya barabara iliyotajwa hapa, ukiangalia miradi ya maji ni miradi mikubwa. Mheshimiwa Rais amejipanga kuhakikisha Watanzania wanapata huduma. Niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge na hili nataka niongee kwa upole sana; kazi hii ina vita katika ulimwengu wa roho na katika ulimwengu wa mwili. Inawezekana msinielewe; lakini vita hii ili tuweze kushinda na Mheshimiwa Rais aendelee kufanya kazi vizuri niombe sana mumuombee, muombeeni, Mheshimiwa Rais ana maono makubwa. Mimi juzi nilivyoenda pale Ikuu, Hayati John Pombe Magufuli wakati anaiacha ile Ikulu haikuwa vile lakini ninyi mmeona. Ukienda kwenye Mradi wa Mwalimu Nyerere unakwenda vizuri, ukienda SGR miradi ambayo iliachwa na Hayati leo hii inakaribia kumalizika na ameongeza miradi mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe sana tuendelee kumuombea, tuendelee kumtia moyo lakini pamoja na wasaidizi wake ili Tanzania yenye neema iweze kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.