Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Dr. Amandus Julius Chinguile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nami niungane na wenzangu kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati nachangia Bajeti Kuu ya Serikali mwaka 2022 niligusa barabara ya Masasi - Nachingwea na Liwale. Wakati naendelea na mchango, alisimama Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, Waziri bingwa kabisa na Mcha Mungu akanipa taarifa ya kwamba haijaondolewa barabara hiyo, bado itajengwa kwa kiwango cha lami. Kadri miezi ilivyokuwa inaenda sasa kwenye ukomo wa mwaka wa Serikali, nilikuwa naendelea kupata shida, lakini leo ninayo furaha, wakati wa bajeti ya Mheshimiwa Waziri, ukurasa wa 11 nimeona ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami unakwenda kufanyika na mkataba utafanyika kabla ya mwezi Juni 30.

Mheshimiwa Spika, habari hii ni njema kwa wananchi wa Jimbo la Nachingwea. Barabara hii wanufaika siyo tu Jimbo la Nachingwea, ni majimbo manne; Jimbo la Nachingwea, Jimbo la Liwale, Jimbo la Masasi na Jimbo la Ndanda. Kwa niaba ya Wabunge ambao hawatapa nafasi ya kuchangia kwenye bajeti hii wanayotokea kwenye maeneo hayo, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa jambo hili jema. Barabara hii tulilia kwa miaka mingi, tulisema kwa muda mrefu, tulipiga magoti, lakini leo Mheshimiwa Rais anakwenda kujenga historia kujenga barabara hii. Tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi pamoja na Manaibu wake, pia na Katibu Mkuu anayeshughulikia ujenzi, Mhandisi Aisha na Katibu Mkuu mwingine na Naibu Katibu Wakuu na watumishi wote wa Wizara hii. Tunawashukuru na tunawapongeza sana kwa kazi hii ya kihistoria. Leo wananchi wa Nachingwea wameniambia niseme kwa unyenyekevu mkubwa, tunamshukuru Mheshimiwa Rais na kazi yetu ni kuendelea kumwombea. Sisi mwaka 2025, mguu kwa mguu na Mheshimiwa Rais. Kazi hii ni ya kihistoria na haijawahi kutokea na hatukuwahi kulala usingizini. Jambo hili ni kubwa. Waliniambia nisiseme sana, nisije nikapoteze madhari ya kushukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeagizwa pia nikumbushe jambo moja ambalo nimekwenda mara kadhaa kwenye ofisi yake. Tunao wananchi ambao walipisha upanuzi wa uwanja wa ndege wa Nachingwea. Namwomba sana Waziri, jambo hili tumezungumza mara kadhaa alifuatilie kwa karibu ili wananchi wale ambao walipisha kwa nia njema upanuzi wa uwanja wa ndege wa Nachingwea, kwa sababu tathmini imeshafanyika waweze kulipwa ili waweze kuendelea na shughuli zao.

Mheshimiwa Spika, kwa unyenyekevu mkubwa, baada ya kusema maneno hayo, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Nachingwea, nashukuru sana na ninaunga mkono kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.