Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi jioni ya leo nami nitoe mchango wangu katika hoja iliyopo mbele yangu. Lakini leo nitajikita kushukuru kwa yale tuliyofanyiwa katika Jimbo la Meatu.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa namna anavyofanya kazi na kwa namna alivyoiendeleza miradi iliyoanzishwa Awamu ya Tano na sasa mingi amekwenda kuikamilisha, likiwepo Daraja la Tanzanite, anaendeleza ujenzi wa Daraja la Magufuli la Kigongo – Busisi ambapo kazi inaendelea na mwaka huu tunaokwenda kuuanza ametenga bilioni 15 kwa ajili ya kuendeleza ujenzi huo.

Mheshimiwa Spika, nimshukuru Mheshimiwa Waziri na Naibu Mawaziri na Watendaji wote kwa kazi nzuri wanazofanya. Mheshimiwa Waziri hana maneno mengi lakini ana utekelezaji mkubwa nae nimshukuru. Miradi ambayo mimi binafsi niliongea na Mawaziri watangulizi wake ilikuwa haijaanzishwa lakini yeye ameianzisha na inaendelea, nakushukuru sana Mheshimiwa Profesa na Naibu Mawaziri.

Mheshimiwa Spika, nimshukuru pia Meneja wetu wa TANROADS Mkoa wa Simiyu kwa kazi nzuri anazofanya za kiwango kwa barabara nzuri zinazojengwa, zinanyanyuliwa juu kiasi kwamba hakuna sasa kukatikakatika kwa barabara wakati wa mvua, lakini pia kwa usimamizi wa fedha mpaka unaona thamani ya pesa inakuwepo.

Mheshimiwa Spika, ninashukuru katika mpango huu ahadi ya kujenga barabara ya Karatu – Mbulu – Haydom – Mto Sibiti – Lalago – Maswa ni ahadi ya muda mrefu, ilikuwa katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi, na sasa Serikali imekwenda kufunga mkataba unaotarajiwa kusainiwa kabla ya mwisho wa mwezi wa Juni kwa mfumo wa EPC+F, lakini imetengwa bilioni 5.5 kwa ajili ya kuanzisha ujenzi huu. Mimi nashukuru kwa sababu hata hiyo bilioni tano itafanya kazi za awali ikiwemo kulipa malipo ya awali.

Mheshimiwa Spika, niendelee kushukuru, tarehe 14 mwezi huu wa Mei, Mheshimiwa Waziri akiwa Itigi wamefunga mkataba wa kilometa 25 katika maingilio ya Daraja la Sibiti kwa shilingi bilioni 21.77. Mimi nashukuru sana, ilikuwa ni kilio cha muda mrefu cha watu wa Jimbo la Meatu, Wilaya ya Meatu na Mkoa wa Simiyu kwa ujumla kwa sababu ni watumiaji wakubwa wa barabara hii wanapokuja Dodoma. Nikuombe tu utakapofunga mikataba ijayo katika hii barabara niliyoitaja mwanzo basi uje ufungie katika maeneo husika ya urefu ule ikiwemo Meatu na wananchi wafurahi kuona, lakini sisi tunafurahi kwa sababu mkataba umeshafungwa na ujenzi utaanza wakati wowote.

Mheshimiwa Spika, nishukuru kwa ajili ya daraja la Itembe tumetengewa bilioni 8.4 na Mkandarasi ameshalipwa advance payment ya bilioni 1.2, lakini sasa hivi tayari ana certificate ya kwanza, ninaombe tu malipo ya awali yalichelewa na mkataba huu ni wa mwaka mmoja leo tumebakiza miaka mitano tu lakini bado iko chini. Niombe Serikali iongeze kasi ya ulipaji. Pia madaraja yaliyobaki ya Lyusa, Chobe na Nkoma, naomba na yenyewe pia yawekwe kwenye mpango wa kuyajenga.

Mheshimiwa Spika, ninashukuru tuliomba lami kilometa mbili pale Mjini Mwanuzi, mmetupatia bilioni moja kwa ajili ya kujenga kilometa 1.25. Barabara hii inakwenda kuwasaidia akina mama kufanya biashara zao usiku na mchana kwa sababu pia inaweza kuwekewa mataa, lakini inakwenda kupunguza mavumbi yaliyokuwa yanachafua maduka ya watu, yalikuwa yanasababisha ajali wakati wa misafara.

Mheshimiwa Spika, ninashukuru daraja la Paji ambalo lilikuwa ni kilio cha muda mrefu, milioni 389 lilishatekelezwa. Watu wa Meatu hatukutarajia kama daraja la chini litaweza kujengwa, lakini Serikali imetoa milioni 90 kwa ajili ya kufanya usanifu, mimi nashukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri ninakuomba tuna barabara yetu ya TARURA ya kilometa 45 inayotoka Mwanuzi kwenda Mwabuzo, tunaomba ipandishwe hadhi imekidhi vigezo, barabara hii ni muhimu kwa uchumi wa Meatu, Wilaya ya Maswa na Mkoa wa Simiyu kwa ujumla. Wataalam kutoka ofisi yako walikuja kuiangalia iweze kuunganishwa na Wilaya ya Igunga, basi naomba uridhie upandishe zile kilometa 45. Nikuombe Meneja wa TANROADS Shinyanga na TANROADS Tabora na wenyewe basi tuungane pale, kwa sababu wafanyabiashara wengi wa Meatu wanaelekea kule Igunga na kusisimua biashara na uchumi wa pale Igunga.

Mheshimiwa Spika, ninashukuru Serikali kwa jitihada inazofanya daraja la Mwamanongu ambayo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais Samia ya 2015 akiomba kura akiwa mgombea mwenza aliahidi kujenga daraja. Daraja lile lina mita 120 ni daraja la TARURA, uhakiki umeshafanyika litagharimu bilioni saba. Naomba sasa upande wa TARURA na wenyewe walitekeleze kwa sababu sikupata muda wa kuongea kwenye Wizara ya TAMISEMI. Naomba sasa na lenyewe litekelezwe, liko katika hii barabara kilometa 45.

Mheshimiwa Spika, nimalizie sasa kwa kuwaambia wananchi na kuwashukuru Serikali kwa kupewa fedha za bottleneck kutoka katika Mfuko wa Fedha wa Dunia, shilingi milioni 400, ambapo tunakwenda kujenga Daraja la Mang’wina kwenda London na Mwajidalala.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)