Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. PROF. PALAMAGAMBA J. A. M. KABUDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu Rahim kwa ruzuku ya uhai na afya. Nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika bajeti hii ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi. Nichukue fursa hii kuwapongeza kwa dhati kabisa Mheshimiwa Profesa Makame Mnyaa Mbarawa, Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi; Mheshimiwa Mhandisi Godfrey Kasekenya, Naibu Waziri Ujenzi; Mheshimiwa Atupele Mwakibete Naibu Waziri Uchukuzi; Balozi Mhandisi Aisha Amour, Katibu Mkuu Sekta ya Uchukuzi; Bwana Gabriel Migire, Katibu Mkuu Sekta ya Uchukuzi; Bwana Ludovick Nduhiye, Naibu Katibu Mkuu Ujenzi na Dkt. Ally Possi, Naibu Katibu Mkuu Uchukuzi. Nawapongeza kwa kazi nzuri wanayofanya katika Sekta hii muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu na kwa ustawi wa Watanzania wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba yangu na ya wananchi wote wa Jimbo la Kilosa, namshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa fedha nyingi za kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu katika Jimbo la Kilosa. Tunamshukuru sana kwa mabilioni ya fedha ambayo ameyaleta Kilosa kujenga barabara na madaraja kupitia TARURA na TANROADS. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa TARURA tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutupa shilingi bilioni nane na milioni 300 kwa ajili ya kujenga Daraja la Berega ambalo litaunganisha Wilaya ya Kilosa na Wilaya ya Kilindi ya Mkoa wa Tanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kupitia TARURA kutupa shilingi milioni 500 kujenga Daraja la Masombawe kule Mamboya, lakini shilingi milioni 800 kujenga Barabara ya Mvumi – Ngege ambaye baadaye itatuunganisha na Wilaya ya Gairo, lakini Barabara ya Parakuyo shilingi bilioni 150 na pia kutoa shilingi milioni 800 kwa ajili ya ukarabati wa barabara na mifereji katika Mji wa Kilosa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa TANROADS, namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutupa shilingi 4,714,000,000 kwa ajili ya kumalizia Madaraja ya Kobe, Kwa Ilonga na Mazinyungu na madaraja haya yatakapokamilika sasa Barabara ya Dumila – Ludewa – Kilosa itakuwa imekamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefarijika sana kuona katika ukurasa wa 287 wa bajeti ya sasa kwamba Wizara imetenga fedha kwa ajili ya feasibility study na detailed design ya Daraja la Mto Mkondoa. Daraja hili ambalo liliondolewa na mafuriko ni daraja muhimu sana na hasa ukizingatia kwamba kwamba sasa tutaanza kujenga Barabara ya Kilosa – Ulaya – Mikumi na daraja hili ni muhimu na kwa muda wote huu tulikuwa tunatumia daraja la reli kuvuka Mto Mkondoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maombi yangu kwa Serikali kwamba feasibility study hii na detailed design isihushishe Daraja tu la Mto Mkondoa, lakini lihusishe Kingo yote ya Mto wa Mkondoa kuanzia Mkadage kwenye Daraja la SGR mpaka Magomeni ili kuimarisha kingo za Mto Mkondoa unaohamahama lakini pia kuzuia mafuriko kwa ajili ya Mji wa Kilosa. Ifahamike Wajerumani walipojenga reli ya kati walijenga mabwawa matano ya punguza ikiwa ni pia pamoja na Bwawa la Kidete. Naomba pia bwawa hili Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi na Wizara ya Kilimo washirikiane ili Bwawa hili likikamilika litakuwa kinga nzuri kabisa ya mafuriko kwa Mji wa Kilosa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kuomba ujenzi wa Reli ya Kilosa – Kidatu kama ilivyoainishwa katika bajeti ufanyike. Reli hii ni muhimu sana kuunganisha Kilosa, Mikumi na Kidatu. Itaunganisha reli ya kati na reli ya SGR kutoka Kilosa kwenda mpaka Mlimba ambako itaunganisha na reli ya TAZARA. Maombi yangu huko mbele ya safari ikiwezekana reli yote hiyo ya Kilosa – Mikumi mpaka Mlimba ama iwe ya cape gauge au iwe ya SGR ili kurahisisha usafiri wa mizigo kati ya Reli ya TAZARA na Reli ya NGR na Reli ya SGR. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii sasa kuzungumzia maombi mengine ambayo nayaomba na hii ni ya ujenzi wa lami wa Barabara ya Chanzuru kupitia Kimamba kupitia Parakuyo kupitia Mkata station kwenda Melela. Barabara hii itakamilisha mzunguko wa Barabara ya Melela kuja Kilosa, Kilosa kwenda Mikumi na hivyo kuongeza ufanisi wa usafiri katika eneo hilo na kuufanya Mji wa Kilosa sasa kuwa ni Mji wa Kimkakati katika usafarishaji na uchukuzi nchini kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kikao cha G7 kilichofanyika Hiroshima Japan, Serikali ya Marekani imetangaza kupitia Parternship for Global Infrastructure and Investment, kwamba itatoa fedha sasa kufufua Reli ya Benguela the Lobito Corridor maana yake kutoka Ndola kwenda Lubumbashi kwenda mpaka Lobito. Huu ndio wakati sasa na wao wamesema wanaweza pia kuiunganisha Tanzania. Sasa tunapata fursa ambayo ni vizuri tukaitumia vizuri ya kuunganisha Bahari ya Hindi na Bahari ya Atlantic na ukiiangalia Afrika ni nchi mbili ambazo zinaunganisha bahari hizi mbili yaani DRC na Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa reli hii itakapoanza maana yake tunaweza tukaitumia fursa hiyo vizuri kutoa mizigo Dar es Salaam mpaka Lobito ikaenda Marekani na Nchi za Carribean na kutoa mizigo kutoka Nchi za Carribean zikaingia Lobito zikaja Dar es Salaam kwenda Nchi za Asia na Nchi za Mashariki ya Mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii maana yake nini? Ni lazima sasa tuimarishe Reli ya TAZARA ili iwe na ufanisi mkubwa sana bila kufanya hivyo ina maana mizigo mingi ya DRC na mizigo mingi ya Zambia sasa itakwenda Bandari ya Lobito badala ya kuja katika Bandari zetu za Tanzania. Kwa hiyo, tuna umuhimu wa kuongeza ufanisi wa bandari zetu, tuna umuhimu wa kuongeza ufanisi wa Reli ya TAZARA ili badala ya kupoteza mizigo, sasa tuweze kuunganisha Bahari ya Antlantic na Bahari ya Hindi kupitia bandari zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bandari hizi tusiimarishe Dar es Salaam tu. Tuimarishe Tanga, Mtwara na tuanze kujipanga kujenga bandari nyingine zaidi na katika bandari hizi ambazo tuzifikirie kuzijenga iko bandari moja tusiiache kuifikiria ni Bandari ya Kilwa. Tumeamua sasa Kilwa iwe Bandari ya Uvuvi, lakini tuangalie uwezekano wa baadaye Kilwa kuwa bandari ya mizigo mingi. Bandari ya Kilwa ina historia ndefu toka wakati wa Ibni Batuta na ndio bandari pekee katika upande huu wa magharibi wa Bahari ya Hindi yenye kina kirefu cha asili na ina milango miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo miaka ijayo Insha Allah Bandari ya Kilwa ndio inaweza kuwa Bandari ya trust shipment ya meli kubwa kuingia kushusha mizigo na baadaye kwenda bandari ndogo. Sisi tuna bahati kubwa sana, tuna uwezo pia wa kuifanya Pangani kuwa bandari. Kwa hiyo, katika master plan ya bandari pamoja na hizo zilizotajwa ya Tanga, Bagamoyo, Dar es Salaam na Mtwara lakini tuanze kufikiria pia kuimarisha Bandari ya Kilwa ili isiwe ya uvuvi tu. Bandari ya Kilwa ndio bandari ambayo miaka ijayo itakuwa bandari kubwa kuliko zote katika Afrika ya Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuifanyie bandari hiyo sasa maandalizi makubwa ili Kilwa ichukue nafasi yake na tuanze kufikiria kutoa Reli ya SGR kutoka Kilwa kuja kuunga ama Pugu au maeneo ya Pwani, ili baadaye mizigo ikitoka Kilwa iweze kwenda moja kwa moja katika Reli ya SGR na kwenda moja kwa moja mpaka sehemu nyingine. Kwa hiyo, tunaweza kuona utajiri mkubwa ambao Mwenyezi Mungu Subhanahu Wataala ameijalia Tanzania katika haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kuchangia, ni sasa Tanzania lazima tuanze kujiweka sawa kuanza kutumia magari na mabasi ya umeme. Dunia inahama kutoka kwenye magari ya mafuta, dunia inahama kutoka kwenye magari ya gesi, dunia sasa inakwenda kwenye magari ya umeme. Tuanze kufikiria mwendokasi Dar es Salaam badala ya kutumia gesi na petrol itumie umeme. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Profesa.

MHE. PROF. PALAMAGAMBA J. A. M. KABUDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwenyezi Mungu ametujalia vyote, naona muda wangu umekwisha, naunga mkono hoja asilimia 100 kwa Wizara hii, lakini Mheshimiwa Mbarawa asiisahau Kilosa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)