Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na mimi kwa kunipa fursa hii ya kuchangia Wizara hii muhimu ambayo inafanya kazi nzuri. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, kwa kweli kwa kazi nzuri anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri nakupongeza ulipokuja Mbeya uliweza kutusainia mkataba wa barabara muhimu ya njia nne kuanzia Uyole mpaka Songwe licha ya wewe unasema kutoka Uyole mpaka Ifisi. Mheshimiwa Waziri hiyo ni hatua nzuri sana. Kwa sababu uchumi wa Tanzania kwa kiasi kikubwa unategemea zaidi barabara hizi za TANZAM. Vilevile jana umeongelea kuhusu kujenga barabara hiyo ya TANZAM, kipande cha Igawa mpaka Tunduma kwa EPC + Finance. Hiyo ni hatua muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba sana Mheshimiwa Waziri, alipokuwa anasaini mkataba pale Mbeya aliwaahidi wananchi wa Mbeya Vijijini kuwa bajeti hii atahakikisha kuwa barabara ya Mbalizi – Shigamba inakuwemo kwenye bajeti hii ili ijengwe kwa kiwango cha lami. Mheshimiwa Waziri ninakuamini sana na ninaimani kabisa kuwa ile ahadi yako kwa wananchi sio wa Mbeya tu, lakini Tanzania nzima ni ahadi muhimu utaitekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Waziri kuna bartabara ambazo ni kiunganishi kikubwa kwa nchi zetu zinazotuzunguka Malawi pamoja na Zambia, lakini na kulisha uwanja wa ndege. Kuna barabara Isyonje – Kikondo – Makete ni barabara muhimu sana. Mheshimiwa Waziri hebu chukulia hiyo umuhimu wa kipekee na kuipa kipaumbele ili iweze kujengwa haraka. Kwa sababu uchumi wa mikoa yetu Mbeya, Njombe, Ruvuma na Iringa inategemea zaidi usafirishaji wa mizigo ili iweze kubebwa na kupelekwa nje na Tanzania iweze kupata pesa za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini barabara nyingine ambayo ni muhimu ni barabara ya Mbalizi – Chang’ombe – Mkwajuni kwenda mpaka Makongorosi. Kwa umuhimu wake namuona Mheshimiwa Mulugo amekuja kukaa hapa karibu ili nisije nikasahau kuizungumzia. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri hii barabara ni ahadi ya muda mrefu sana, lakini imekuwa haipewi umuhimu. Nakuomba sana katika bajeti hii, barabara hii ipewe kipaumbele cha pekee iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wamezungumzia umuhimu wa nchi yetu kijiografia. Kiushindani Tanzania Mwenyezi Mungu ametupa neema ya sisi kiushindani akatupa jiografia nzuri, tuna bandari, tuna maziwa, lakini bado hatujazitumia vizuri hizi kwa upendeleo ambao Mwenyezi Mungu ametupa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bandari yetu ya Dar es Salaam ufanisi wake ukilinganisha na bandari nyingine inawezekana sisi ni wa pili kutoka mwisho na wa mwisho nafikiri ni Mogadishu – Somalia. Sasa hatuwezi kuanza kujilinganisha namna hiyo. Tuchukue hatua za haraka ili tuboreshe ufanisi wa bandari yetu. Pia sio kuboresha bandari tu lakini tuboreshe na reli zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali na Mheshimiwa Rais kwa pesa nyingi alizozipeleka kwenye SGR, lakini tunakuomba Mheshimiwa Waziri, kwa umuhimu huo huo hebu iboreshe Reli ya TAZARA. Reli ya TAZARA ni muhimu sana kwa ushindani wa Bandari yetu ya Dar es Salaam, lakini vilevile Bandari ya Katanga kwa ajili ya soko la DRC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tunapoteza biashara zetu kwa kiasi kikubwa kwa nchi jirani kwa bandari jirani kutokana na ufanisi tulio nao kwenye bandari yetu ya Dar es Salaam. Mfano mdogo tu, kwa kupitisha mizigo yetu Zambia, Tanzania inapoteza karibu shilingi bilioni 60 kwa kipande hicho tu cha Tunduma mpaka Zambia ili mzigo ufike Congo, hii sio pesa ndogo. Pesa hii ukiijumlisha kwa miaka mitano inatosha kabisa kuboresha Bandari ya Katanga na hata kujenga barabara kwenda Lubumbashi. Hiyo itaongeza ufanisi na vilevile itanongeza ushindani.

Kwa hiyo, nakuomba sana Mheshimiwa Waziri, toa umuhimu kwenye Bandari yetu ya Dar es Salaam ipate wawekezaji wazuri na biashara sio ifanye Serikali, biashara tuwaachie watu binafsi. Mfano ni TAZARA watu binafsi wafanya vizuri na TAZARA imepata pesa nyingi kwa sababu ya wale watu mliokodisha wafanye biashara ndogo ya TAZARA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna changamoto nyingine ambazo ziko bandarini kutokana na ufinyu wa bandari yetu. Mimi binafsi naona Bandari ya Bagamoyo itatuweka Tanzania mahali pazuri zaidi na tusifikirie kujenga wenyewe, tufikirie uwekezaji wa wenzetu kwa PPP. Ninaimani bandari ya Bagamoyo ambayo ina kina cha asili cha mita 18 ina uwezo wa meli kubwa kuja Tanzania zenye ukubwa wa mpaka mita 400. Hiyo itatufanya sisi tuweze kufanya biashara vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile nilikuwa naangalia Shirika letu la Ndege la Tanzania; wenzangu wameongelea ni namna gani tuliweke katika position ambayo inaweza kufanya vizuri zaidi. Mimi ningejikita zaidi kuhakikisha kwamba tuna nunua ndege za mizigo, lakini tunajenga viwanja vya ndege vingi zaidi na hivyo vilivyopo tuviboreshe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nakuomba Serikali inunue ndege za ziada za mizigo ili mizigo yetu iweze kufanya vizuri kwenye soko la dunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)