Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyoko mezani.

Mheshimiwa Mwneyekiti, kwanza nichukue fursa hii kuipongeza sana Wizara hii ya Ujenzi inafanya kazi kubwa sana. Sisi tumefanya ziara na Kamati, iko miradi mikubwa inayosimamiwa na TANROADS. Daraja la Kigongo – Busisi shilingi bilioni 716 fedha za ndani, kazi inaendelea vizuri sana. Iko barabara kubwa ya Kabingo – Kasulu – Manyovu kilometa 260.6 wakandarasi wako site na itafungua sana Mkoa wa Kigoma. Pongezi nyingi Wizara, Dkt. Samia Suluhu Hassan na wenzetu wa TANROADS. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kule Jimbo la Ukonga na Dar es Salaam, barabara ya BRT Awamu ya Tatu, kuanzia Gongo la Mboto mpaka Kariakoo, mkandarasi yuko site na kazi kubwa ya mradi huu inafanyika, ni kazi ya kupongezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitachangia maeneo matatu; eneo la kwanza ni reli katika ukurasa wa 74.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali, wakati Dkt. Samia Suluhu Hassan anaingia madarakani kulikuwa na vipande viwili vya reli ya SGR vinajengwa; Dar es salaam - Morogoro na Morogoro – Makutupora, lakini bajeti hii inavyowasilishwa hivi sasa tayari vipande vyote vitano vya kuanzia Dar es Salaam mpaka Mwanza kilometa 1219 vina wakandarasi, kilometa 506 Tabora – Kigoma ina mkandarasi yuko site. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini naomba niseme jambo moja, Tanzania ndio nchi inayojenga reli ya SGR kwa gharama nafuu zaidi kuliko nchi zote Afrika. Wakati Tanzania iko kwenye dola milioni 4.3 kwa kilometa anayefuatia ana dola milioni 5.9 kwa kilometa, ni kazi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikataba hii haina eneo la ongezeko la bei, whether kuna inflation hakuna variation, bei iliyosainiwa kwenye mkataba ndio bei atalipwa mkandarasi mpaka mwisho. Hili linatufundisha nini? Linatufundisha kwamba suala kubwa kwenye miradi mikubwa ya ujenzi ni uadilifu na sio njia ya kumpata mkandarasi. Hizi nchi ambazo zinajenga kwa milioni sita, saba zilifanya competitive bidding, lakini Serikali ya Awamu ya Sita kwa njia yao ya single source bado ndio nchi ya Afrika ambayo inajenga reli kwa gharama ya chini zaidi. (Makofi)

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jerry, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kingu.

TAARIFA

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mchangiaji kwamba anachokisema hata ukiangalia BOQ zilizotumika katika kujenga standard gauge bado mkandarasi ameshinda tender chini ya kiwango cha BOQ zilizopitishwa. Kwa hiyo, ninaungana naye kwamba gharama tulizozitumia Tanzania kujenga SGR ni gharama za chini ukilinganisha na mataifa mengi duniani. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jerry, unaipokea taarifa?

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea, Mheshimiwa Kingu una akili nyingi, utafika mbali, una kitu ndani yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na niseme tu amesema vizuri engineers estimate ziko juu kuliko gharama ya reli inayojengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, ni eneo la bandari. Nchi yetu imepata kudra ya Mwenyezi Mungu ya kuwa strategically geographically located, kuwa nchi ambayo inahudumia nchi zaidi ya saba ambazo ziko land locked. Bandari yetu imekuwa na miradi mingi ya uboreshaji, Serikali imefanya lazi kubwa, lakini bado kuna suala la efficiency.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo bandari yetu wale wageni wa Dar es Salaam wakifika pale Coco beach usiku wanaona taa kule baharini wanadhani ni majengo, kumbe ni meli zinazosubiri kutia nanga kutokana na masuala madogo tu kiutendaji ya efficiency. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niishauri Serikali, yako mambo ambayo kuna watu wamebobea kuliko sisi. Tunapo invest kwenye miradi mikubwa masuala ya operations ni vema tukawaacha watu wenye tija kubwa ya operation, tija kubwa ya investment ili bandari iwe efficient. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeisemea reli ya SGR; reli ya SGR ikikamilika itahitaji mzigo mkubwa sana wa kupeleka Mwanza, Kigoma na nchi za Jirani na itahitaji mzigo mkubwa sana wa kuja bandarini na bila kuwa na efficient port tutatkuwa tumefanya kazi bure. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mambo matatu; jambo la kwanza ambalo linatutatiza sana Watanzania ni ujuaji, yaani tunakuwa wataalamu kuliko wataalamu wenyewe kwenye baadhi ya mambo ya maamuzi ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ni hofu; yaani mtu anakuwa na hofu ya jambo ambalo hajawahi kuliona na jambo la tatu ni imani. Niwaombe Waheshimiwa Wabunge wenzangu, tuwe na imani na Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan, itupeleke kwenye uendeshaji wa bandari ambayo tija yake ndiyo itakuja kujenga shule, barabara, elimu na afya kwenye majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kudra ya biashara Mwenyezi Mungu hajaijalia. Tufanye yale ambayo tunaweza kuyafanya kwa ubora zaidi lakini yale mengine ambayo yanafanywa na private sector, tuwaachie private sector.

MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jerry, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Catherine Magige.

TAARIFA

MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpa taarifa mchangiaji anechangia kuwa bandari kubwa duniani ya Singapore inaendeshwa na sekta binafsi pamoja na Serikali na ndio tegemeo la nchi hiyo.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jerry, taarifa unapokea?

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea mwanangu Catherine, hii ndio inaitwa beauty of brains, mwanangu uko vizuri. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu ni ATCL; Shirika la Ndege la ATCL lilipotoka na lilipo sasa ni kazi kubwa sana ambayo Serikali imefanya. Shirika limetoka kwenye ndege moja leo tuna ndege 11. Shirika limetoka kwenye mapato ya bilioni 23 leo tuna mapato ya bilioni 254; Shirika hili linafaida nyingi. Leo Babu Tale enzi hizo yuko Tiptop Connection tunakuja na ndege hapa Dodoma nauli shilingi milioni moja. Leo kuna flight tatu zinakuja Dodoma, leo kuna flight inakwenda Mpanda, watalii waliokuwa wanakwenda Mbunga ya Katavi walikuwa wanalazimika kukodi ndge leo wanakwenda kwa commercial flight. Shirika hili lina faida ya biashara, faida ya utalii, limeifungua nchi, linaitangaza nchi. Leo wapo Watanzania na wageni wanaokwenda kupata matibabu India, watu wanakwenda China wanapata direct flight kutoka nchini kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukisoma vitabu vyake vya hesabu, sasa hapa ni eneo la kuwa makini, utasoma vitabu vya hesabu utaambiwa kuna hasara. Ni kweli? Ndio kuna hasara, hasara ni nini? Hasara ni revenue ukiondoa expenditure ndio unapata hasara. Kwa nini kuna hasara? Kuna hasara kwa sababu shirika hili linazo changamoto nyingi. Moja kati ya changamoto ni kukodisha ndege kutoka TGFA ambalo Serikali imeliona, Rais amelitolea maelekezo, Kamati yetu sisi tumekwishatoa mapendekezo hapa Bungeni na tukaazimia na Serikali inalifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukichukua zile lease expenses za ATCL ukaweka na zile maintenance reserve na interest za yale madeni, yuko Mbunge mmoja hapa jana ameomba Serikali iendelee kulipa yale madeni. Kwa gharama ya mwaka wa fedha 2021/2022 zaidi ya bilioni 89 zimetumika kwenye maeneo haya. Ukisema uondoshe zile gharama maana yake kwa mwaka wa fedha 2021/2022 unaona hasara ya bilioni 35 kuna faida ya bilioni 54 kwenye Shirika hilo, tuwatie moyo. Mwenyekiti, wa Bodi Profesa Neema Mori anafanya kazi kubwa mwanamama huyu na wamesema hapa kwenye swali leo asubuhi wakina mama wakipewa nafasi hizi wanafanya kazi nzuri. Engineer Matindi na wenzake jana wametuletea hapa marubani. Shirika hili ni moja kati ya mashirika Afrika yenye watumishi ambao ni wazawa wa nchi zao. Tunao marubani wanawake, wako ma-cabin crew wazuri walikuja hapa ningewataja majina, lakini nitapata tabu nyumbani, lakini wanafanya kazi nzuri, tuwapongeze na tuwatie moyo shirika hili linakwenda kuifungua nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo haya ya kibiashara ni vema tunavyoyafanyia analysis, tuyafanyie analysis kwenye uwanda mpana zaidi kuliko kuangalia items chache kwenye financial statements ambazo zinaweza zikakatisha tamaa watu wanaolitumikia Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninaamini Serikali kwenye bajeti hii imesema inanunua ndege nne mpya. Ndege hizi zikija na hizi zilizopo na matatizo haya yakitatuliwa, matatizo ya Covid yamekwisha, shirika hili linakwenda kuingiza faida na kuwa shirika kubwa sana hapa nchini. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jerry, ahsante sana.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nusu dakika niseme tu kwamba hata hiyo mikataba ya kukodisha ndege ni mikataba ile ambayo inakwenda kwa style ile ya Mandonga. Ndege ikiruka inalipa, ndege isiporuka inalipa. Kwa hiyo, kipindi cha Covid wakati ndege ziko chini, zilikuwa zinaingiza hasara kwa matumizi makubwa ya lease wakati mapato ya tiketi na usafiri yalikuwa chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana naunga mkono hoja, naipongeza Wizara hii, niwatie moyo waende wakatekeleze majukumu yao. Nakushukuru sana. (Makofi)