Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Mwanne Ismail Mchemba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Tabora Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nitangulize shukurani za pekee kwa kupata nafasi hii kwa muda huu wa asubuhi. Pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kunifikisha siku hii ya leo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie kwa kutanguliza pongezi lakini nitachangia kwa kuanza na TAMISEMI na badaye Utawala Bora. Tuliponadi sera mwaka 2015 tulikuwa na wasiwasi mkubwa sana kuhusu Mheshimiwa Rais wetu kwa sababu wakati anazunguka Tanzania nzima alinadi na alikuwa na uhakika bila uwoga. Kwa hiyo, nampongeza sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kumpongeza huko niseme alisema hivi, naomba Watanzania wenzangu mnipe nafasi niweze kuongoza nchi hii kwa uchungu niliokuwa nao na Watanzania kwa umaskini wao. Sasa hiyo ilitia mashaka kwamba watu wangemnyima kura kwa sababu alisema atapambana na mafisadi, bandari, rushwa na ubadhirifu wa aina yoyote katika nchi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa basi kwa sasa kiongozi huyo ametimiza matakwa yake kulikuwa na wasiwasi wakati ule kwamba angenyimwa kura lakini alisema itakavyo kuwa na iwe lakini niwatendee haki Watanzania wangu. Hivyo basi, nichukue nafasi hii kumpongeza sana, naomba aendelee hivyo hivyo, jina lake kubwa na Watanzania wana imani kubwa naye.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimpongeze Makamu wa Rais, mwanamke anaweza na amejipanga. Pamoja na kwamba ni mwanamke ameweza kuzunguka nchi nzima, nampongeza sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini si hilo tu, nawapongeza sana Mawaziri pamoja na Manaibu wote wasiogope, kazi wanayofanya wananchi wanaiona na wanamsaidia Rais ipasavyo. Mawaziri hawa wanafanya kazi kiasi ambacho hata sisi tunaona na tunawapenda na tunawaamini kwamba watafanya kazi hiyo hadi miaka mitano na 20 ijayo. Wasiogope kama mahali pa kutumbua majipu watumbue haiwezekani hata kwenye Halmashauri Rais akatumbue majipu wao ndiyo watumbue majipu hayo kama walivyoanza na watumishi hewa, walikuwepo kweli lakini Mheshimiwa Rais anawatumbua.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia niwapongeze Marais waliotangulia wa Awamu zote Nne kazi waliyofanya imeonekana mpaka tumefika hapa leo. Kwa hiyo, nawapongeza sana Marais wote, Rais wa Awamu ya Nne kazi aliyofanya imeonekana na leo Mheshimiwa Rais ameipokea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuchangia kuhusu TAMISEMI. Kazi kubwa tumeifanya kwenye Kamati kwa sababu na mimi ni Mjumbe wa Kamati hii, kwa hiyo niwapongeze Waziri wa TAMISEMI na Naibu wake kwa ushirikiano waliotuonyesha lakini ninayo machache ya kuongezea.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna miradi ya Awamu ya Kwanza na ya Pili ya TASAF ambayo haijakamilika. Kwa sababu iko chini yao naomba waikamilishe ipasavyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia wenzangu wamezungumzia kuhusu posho ya Madiwani, kweli ni ndogo. Naomba yatolewe maelekezo kwa sababu posho anayolipwa Diwani hailingani na kazi anayofanya, pesa yao ni ndogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine, Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji, hawa nao waangaliwe kwa jicho la huruma. Watu hawa kazi wanazofanya wanatuwakilisha pia sisi Wabunge tuliomo humu ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia 10 inayotengwa na Halmashauri zetu na Manispaa haijatiliwa mkazo pamoja na kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu aliizungumzia alipokuwa Lindi. Asilimia 10 inatolewa kama zawadi wakati si kweli. Ningemuomba Waziri asichoke, asisitize, atoe waraka mgumu ili watu wajue kwamba ni haki ya Watanzania wote kupata asilimia 10 bila kujali itikadi za watu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika vikundi hivyo vinavyopata hiyo asilimia 10 ningeomba Serikali iangalie vikundi vya akina mama wajane. Fedha hii wanapewa tu vikundi vyote lakini kuna vikundi ambavyo vimesajiliwa vya akina mama wajane navyo viangaliwe kwani wanatia huruma kwa sababu wengine wamenyimwa haki zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, si hivyo tu, hata hii shilingi milioni 50 ilenge pia kwenye vikundi hivyohivyo ambavyo vipo lakini mkisema kwamba vianzishwe harakaharaka kuna vingine vitaanzishwa ambavyo havistahili kupewa. Ningeweza kuchanganua sana lakini kwa sababu ya muda naomba niseme asilimia 10 haitolewi kama inavyotakiwa. Mtu anatoa asilimia 2, asilimia 3 kama mfano tu. Kwa hiyo, naomba Wizara husika iweze kutia mkazo katika jambo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kuhusu ukusanyaji wa mapato. Tulishazungumzia sana kuhusu masuala ya minara, mabango, ushuru huo umeachiwa tu wananchi, wao wamepata mwanya wa kwenda kukusanya kule kodi zao lakini wanapeana kienyeji mno, sheria ya Halmashauri ingeweza kutumika katika suala hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu bima ya afya, kuna vituo vingine vya afya na zahanati zake havina umeme na bado REA haijafika. Naomba katika maeneo hayo basi kuwe na utaratibu wa kuweka solar.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende kwenye Menejimenti ya Utumishi wa Umma. Naomba Mheshimiwa Waziri azisaidie ofisi zote ambazo ziko chini yake, Tume ya Utumishi na kadhalika, kwa mfano, Idara ya Kumbukumbu za Nyara za Serikali, asipotimiza hili nalolisema nitaishika shilingi ya mshahara wake. Tulitembelea eneo hilo tukakuta wafanyakazi wako katika mazingira magumu sana, hakuna AC, kuna chombo ambacho kimeharibika takribani miaka miwili inahitajika shilingi milioni 26 tu lakini mpaka leo haijatolewa. Sehemu ile ni nyeti, ina kumbukumbu nzuri za Taifa hili ambazo ni za kizazi na kizazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tulitembelea masuala ya TASAF III, tumekwenda Kigoma, Mwanza, watu waliopewa sio walengwa na hawa wote wako chini ya TAMISEMI. Ofisi zao ziko chini ya TAMISEMI, watendaji wako chini ya TAMISEMI, wamepewa ambao sio walengwa. Kwa hiyo, nashauri pia hili nalo liangaliwe vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine, Tume hizi za chini ya Ofisi ya Rais mpaka leo zinapanga na wanalipa kwa dola, ni hasara. Ni vyema Serikali ikajipanga wawe na majengo yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niiombe Serikali inapofanya marekebisho mbalimbali ya kupandisha vyeo, mishahara iende sambamba na kupewa pesa zao. Kuna watu wamepandishwa vyeo lakini mpaka wamekufa hawajapata hela zao na hao walioachiwa sio rahisi kufuatilia. Kwa hiyo, ucheleweshwaji wa ongezeko la mishahara nayo ni kero kwa Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kuhusu uhamisho. Uhamisho unapotolewa ni vyema basi uambatane na pesa inayokuwepo kwenye bajeti. Kama tusipofanya hivyo ina maana bado tutaendelea kuwa na madeni na malimbikizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingineā€¦
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa heshima na taadhima, naunga mkono hoja asilimia mia kwa mia. Ahsante sana.