Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nianze mchango wangu kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi nzuri wanazozifanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nichukue nafasi hii niwapongeze Mawaziri wote. Wahenga wanasema nyota njema huonekana asubuhi, mmeanza vizuri, msikate tamaa, songeni mbele, tuko pamoja. Pia nichukue nafasi hii kuwapongeza Mawaziri ambao wametoa hoja hii leo, Mheshimiwa Simbachawene, Mheshimiwa Kairuki na Mheshimiwa Jafo, hongereni sana. Kabla sijaendelea na mchango wangu niseme kwamba naunga mkono hoja zote mbili kwa asilimia mia moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa na maeneo yafuatayo katika mchango wangu. Kwanza nianze na maeneo mapya ya utawala. Hata kama Mheshimiwa Simbachawene wakati anajibu swali moja alituambia kwamba Waheshimiwa Wabunge tuwe wapole kuhusu maeneo mapya ya utawala, sisi Waheshimiwa Wabunge tutaendelea kuomba kwa sababu maeneo mengine tumeahidi na maeneo mengine kuna umuhimu huo wa kuanzisha maeneo mapya ya utawala. Hii haifuti jukumu la Serikali kufanya maandalizi ya kutosha, hapa suala ni Serikali kufanya maandalizi ya kutosha kabla ya kuanza kutangaza maeneo hayo ya utawala. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwangu tuna Halmashauri ya Mji wa Nanyamba, imeanzishwa hivi karibuni, ni miongoni mwa Halmashauri ambazo kama walivyosema Wabunge wengine hakukuwa na maandalizi ya kutosha ili Halmashauri hiyo ianze. Mkurugenzi na watendaji wake wamejibanza tu kwenye ofisi ambayo zamani ilikuwa ya Mtendaji wa Kata. Kwenye bajeti ya mwaka 2015/2016, hii ambayo inaendelea, zilitengwa fedha shilingi milioni 800 kwa ajili ya ujenzi wa ofisi mpya ya Mkurugenzi lakini hadi tarehe ya leo hata shilingi haijapokelewa kwa hiyo ujenzi huo haujaanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile si suala tu la miundombinu kuna suala la wafanyakazi. Kwenye Halamshauri ya Mji wa Nanyamba tuna upungufu wa watumishi 456 lakini tuna idara na vitengo sita ambavyo havina Wakuu wa Idara na kitengo kimojawapo ni Idara ya Maji ambayo ni muhimu na jimboni kwangu kuna tatizo la maji lakini idara hiyo inaongozwa na pump attendant. Sasa hebu fikiria tunapotengeneza mpango wetu wa kuivusha Nanyamba ipate maji kwa asilimia 85 mpago huo utasimamiwa na nani kama hiyo idara kwa sasa hivi inaongozwa na pump attendant? Kwa hiyo, naomba yale ambayo yanawezekana yafanywe haraka. Najua kuna tatizo la kibajeti kuhusu ujenzi wa ofisi ya utawala lakini hili la watumishi inawezekana kabisa kuwahamisha watumishi kutoka maeneo mengine na kupelekwa Halmashauri ya Mji wa Nanyamba.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili, Halmashauri hizi mpya huwa hazijaunganishwa katika mifumo iliyopo. Kuna mfumo wa EPICAR ambao upo kwenye Halmashauri zetu, Halmashauri ya Nanyamba bado haujasimikwa lakini kuna mfumo wa LAWSON ambao nao vilevile katika Halmshauri yetu ya Nanyamba bado haujasimikwa. Kwa hiyo, naomba sana ofisi ya TAMISEMI ishughulikie changamoto hizi ili Halmashauri ya Nanyamba iweze kwenda kama inavyokusudiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu nyingine ni kuhusu uboreshaji wa huduma za jamii na hapa nitajikita sana katika huduma ya afya. Kama nilivyosema Halmashauri yangu ya Mji wa Nanyamba ni mpya ina changamoto nyingi na naomba TAMISEMI i-take note na iangalie jinsi ya kushughulikia huduma hizi katika bajeti ya 2016/2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Halmashauri hii haina Hospitali ya Wilaya lakini pili hakuna kituo hata kimoja cha afya. Kati ya vijiji 87 tuna zahanati 24 tu kwa hiyo utaona changamoto kubwa tuliyonayo katika utoaji wa huduma za kijamii. Nafikiri TAMISEMI itatuunga mkono kwa sababu kwenye bajeti yetu kwenye own source tumetenga fedha kidogo kwa ajili ya uanzishwaji wa ujenzi wa vituo vya afya na ulipaji wa fidia eneo la ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. Ni matarajio yangu kwamba TAMISEMI itatuunga mkono ili kutatua changamoto hizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu mwingine utajikita kwenye uendeshaji wa Halmashauri za Wilaya. Sikuona kwenye kitabu alichowasilisha Waziri suala la kuwajengea uwezo Waheshimiwa Madiwani. Madiwani wetu wana majukumu mazito ya kuzisimamia Halmashauri lakini Madiwani hawa wanahitaji kujengewa uwezo. Sijaona kwenye kitabu cha Waziri, kwa hiyo, naomba sana TAMISEMI ilichukulie suala hili kwa uzito unaohitajika ili Madiwani wetu wajengewe uwezo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa umuhimu wa kipekee Wenyeviti na Mameya hawa wanasimamia uendeshaji wa shughuli za kila za Halmashauri. Kwa hiyo, wanahitaji taaluma mbalimbali kwa mfano uendeshaji vikao na ufuatiliaji wa miradi ya maendeleo. Tunacho chuo chetu cha Serikali za Mitaa Hombolo tunaweza tukakitumia kwa ajili ya kutoa mafunzo hayo kwa Waheshimiwa Madiwani.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile imefika wakati tujiulize kwenye Kanuni zetu za Kudumu za Uundaji wa Halmashauri, je, hizi kanuni zetu ambazo tumejiwekea hasa kuhusu uendeshaji wa vikao vya Halmashauri vikao hivyo vinakuwa na tija? Tufikirie kwenye Halmashauri kuna sekta zote maji, elimu, afya na kila kitu lakini Baraza la Madiwani wanafanya kazi kwa muda wa siku mbili, siku ya kwanza wanapokea taarifa toka kwenye kata, siku ya pili wanaendesha hilo Baraza wanazungumzia maji, elimu, afya na mambo mengine kwa muda wa saa nne tena Diwani mwingine yupo kwenye kikao anapigiwa simu kwamba gari ya kijiji inaondoka kwa hiyo anaomba aondoke mapema ili akawahi hiyo gari ya kijijini kwao. Muda umefika sasa hivi tufikirie kuendesha Halmashauri zetu kwa session kama tunavyofanya session za Bunge hata kama siyo muda mrefu, lakini wachukue siku tatu au nne waweze kujadili kwa kina maendeleo ya Halmashauri yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni la maji katika Jimbo langu. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Maji Engineer Kamwele kwa sababu nilimwambia tatizo langu na akafanya ziara amejionea. Kwa kweli Jimbo la Nanyamba kuna shida ya maji, ni takribani asilimia 35 tu ya wakazi wake wanapata maji ya uhakika. Sasa maji ni maendeleo, ni vigumu kuzungumzia maendeleo wakati huna maji kwa sababu akina mama wengi wanahangaika kutafuta maji badala ya kushughulika na shughuli za maendeleo lakini vilevile magonjwa mengi yanasababishwa na kutopatikana kwa maji safi na salama.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana kwenye bajeti hii upatikane ufumbuzi. Ufumbuzi wenyewe upo kwa sababu tatizo la maji Nanyamba ni miundombinu lakini tunavyo vyanzo vya uhakika kuna Mto Ruvuma, kuna mradi wa muda mrefu wa maji wa Makonde lakini tuna Bwawa la Kitele na miradi 18 ambayo ilifadhiliwa na AMREF ambayo ikikarabatiwa inaweza kupunguza kiwango cha watu wengi wanaokosa maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie mchango wangu kuzungumzia kuhusu sekta ya elimu. Niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuja na Sera ya Elimu Bure na hii imeongeza udahili katika taasisi zetu za elimu ya msingi, sekondari na vyuo lakini bado kuna changamoto. Kuna changamoto kuhusu miundombinu, madarasa na nyumba za Walimu kwa sababu mpango wa MMES na MMEM ulijenga miundombinu lakini sasa hivi kuna ongezeko la wanafunzi na walimu. Kwa hiyo, inahitajika tutenge fedha za kutosha kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za walimu na madarasa mapya, lakini kuna madarasa ya MMEM na MMES ambayo tulijenga mwaka 2002 sasa yanahitaji ukarabati mkubwa lazima fedha za kutosha zitengwe kwa ajili ya ukarabati huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naomba sana TAMISEMI na Wizara ya Elimu zijikite katika kufuatilia kile kinachofanyika darasani ili walimu wapewe motisha na vilevile tusiangalie matokeo…
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.