Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili nami nipate wasaa wa kuchangia kwenye Bajeti iliyoko mbele yetu. Namshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehma kwa kunipa tunu ya uhai. Kwa namna ya kipekee niwashukuru wananchi wa Mkinga kwa heshima waliyonipa ya kuwa mtumishi wao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kugusia eneo la afya. Mwezi Februari, tulizindua taarifa ya tathmini ya utoaji wa huduma za afya nchini. Taarifa ile ukisoma inakupa matumaini kweli kweli. Ni taarifa inayosema kwenye vituo vya afya vya private sector, huduma za afya za mtoto zinatolewa kwa asilimia 80, lakini kwenye vituo vya Serikali huduma za kisasa za huduma ya mama na mtoto zinatolewa kwa asilimia 97. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali lakini napongeza yale yaliyomo kwenye taarifa ile. Nilipokuwa nikiisoma taarifa ile nikasema hapa barabara, kwenye suala la universal health tunakwenda vizuri; lakini nikapata mashaka makubwa nilipokuja kuiona hotuba. Nilipokwenda ukurasa wa 32, ukajaribu kunionyesha mambo tofauti. Ukurasa ule utuambia katika Halmashauri 181, Halmashauri 84 ndiyo zina hospitali za Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri 97 zinapata kudra ya Mwenyezi Mungu ya huduma kutoka kwa Taasisi za Mashirika ya Dini na kadhalika. Hili likanishtua kwa sababu Mkinga leo hii tunapozungumza, Wilaya iliyoanza mwaka 2005 na kupata hadhi ya kuwa Halmashauri mwaka 2007 mpaka leo hatuna Hospitali ya Wilaya. Tunapata huduma kutoka Tanga kwenye Hospitali ya Bombo, tunapata huduma kwenye Hospitali ya Wilaya ya Muheza. Tumekuwa tukitenga kwenye bajeti fedha kwa ajili ya ujenzi tangu mwaka 2011, fedha haziji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ndani utaambiwa kwamba nendeni mkatenge kwenye bajeti. Tunatenga, fedha haziji! Tusaidieni! Tusaidieni ili watu wetu waweze kupata huduma hizi, maana Serikali ina wajibu wa kulinda maisha ya watu wake. Wananchi wametuamini, tuwatendee haki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma hotuba hii ukurasa wa 32 ule, unatuonyesha kwamba tunatakiwa kuwa na direction mpya ya kuhudumia mambo. Sweeping statement kwamba tunataka kila kijiji kiwe na zahanati, tunataka kila kata iwe na kituo cha afya, pekee haitoshi tunatakiwa tufanye zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zile ukiziangalia zinaogopesha! Vituo vya afya 484 katika kata 3,506. Maana yake, tumeweza kujenga vituo vya afya 12% tu katika maeneo yetu, hii haikubaliki hata kidogo! Tuna vijiji 12,500 na kitu, vijiji 8,043 havina zahanati. Maana yake nini? Maana yake tumeweza kupeleka huduma hii kwenye vijiji siyo zaidi ya asilimia 36. Lazima tubadilike! Mkakati wetu wa kutufikisha kwenye kutoa huduma hizi una walakini. Mawaziri mliopo kwenye Wizara hizi, tunawaamini, tunaamini mtatoa uongozi utakaotutoa hapa twende mbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni uwezeshaji wa wananchi kiuchumi. Nataka ni-declare interest, mimi nimetoka kwenye huduma hizi za fedha. Kumbukumbu zangu zinanionyesha, zimekuwepo jitihada mbalimbali za kupelekea huduma za kifedha kwa wananchi, kuwawezesha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumbukumbu zangu za haraka haraka zinaniambia tumekuwa na miradi takribani 17 yenye lengo la kutoa huduma za kifedha kwa wananchi. Utazungumzia SELF, utazungumzia PRIDE, utazungumzia mradi wa huduma za kifedha vijijini, utazungumzia miradi ya vijana; miradi karibu 16, yote hii inafanyika kwa lengo zuri la kuwawezesha wananchi, lakini changamoto tuliyonayo, mitaji hiyo haitoshi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakuja na Shilingi milioni 50 hizi kwa kila kijiji; tusiende kichwa kichwa. Wapo wenzetu walikwenda hivi wakaumia. Uganda walianzisha mradi wa namna hii wakiuita Entandikwa. Mwaka 2000 nilikuwa Uganda nikaenda kuungalia, repayment 0%, hakuna hela ilirudi. Wenzetu wa Thailand walifanya kitu cha namna hii, lakini wao walikuwa makini kidogo, mambo yao yamekwenda vizuri. Tusiwe na haraka ya kutoa fedha hizi bila ya kuwa na utaratibu makini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mifumo yetu ya kifedha, Bunge lililopita tulikuwa tunalalamika hapa, tunasema tupewe mitaji ya kuwezesha kuanzisha community bank. Leo hii community bank ukitaka kuianzisha, unazungumzia shilingi bilioni mbili. Kama tungekuwa makini, tungeweza kujipanga. Mimi nina vijiji 85, ukiniambia unapeleka shilingi milioni 50 kwenye kila kijiji, ni shilingi bilioni nne na kitu. Ningeweza kukwambia peleka Shilingi bilioni mbili ifunguliwe community bank ambayo kila mwananchi katika Wilaya yangu atakuwa na hisa kwenye benki hiyo na hizi fedha nyingine tuweze kuzikopesha. Tungekuwa na uhakika kwamba fedha hizi zitawafikia wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimeambiwa mtakuwa na pilot katika kugawa fedha hizi. Twendeni kwenye hiyo pilot, lakini tuangalie vile vile uwezekano wa kuanzisha community bank kupitia fedha hizi. Wale tutakaoweza kuwa na regional bank, tukikubaliana mimi na Mheshimiwa January na wenzangu wengine wa Tanga tuwe na regional bank katika Mkoa wa Tanga, tukikubali kwamba mafungu yatoke kwenye fedha hizo ambayo inafikia shilingi bilioni tano kwa kuwa na regional bank, mtukubalie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maji. Makao Makuu ya Wilaya ya Mkinga hayana maji. Kuna mradi pale tumebuni chanzo cha Kinyatu, tumeambiwa tutapata ufadhili wa Benki ya Dunia. Tumepeleka maandiko yanayotakiwa tupate mshauri mwelekezi tangu mwaka 2011, hakuna kitu! Tusaidieni watu wa Mkinga tupate huduma ya maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.