Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia jioni ya leo. Kwanza niseme kwamba siungi mkono bajeti hii kwa sababu haitekelezeki.
Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya TAMISEMI na nilisema kwenye Kamati kwamba baadhi ya Mikoa iliyoleta bajeti kwenye Kamati, bajeti yao walipunguza kwa zaidi ya asilimia 60. Kwa hiyo, kwa maoni yangu, bajeti hii haitekelezeki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie suala zima la Shirika la Usafiri la Dar es Salaam (UDA) pamoja na mradi wa mabasi yaendayo kasi ya DART. Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na kikao cha Baraza la Madiwani cha Kamati ya Uongozi cha Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam na Serikali yenyewe na Msajili wa Hazina, zimejiridhisha kwamba hisa za UDA ziliuzwa kinyume cha taratibu kwa anayejiita mwekezaji Kampuni ya Simon Group Limited. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, rasilimali za UDA zinazohamishika na zile zisizohamishika, zimetapakanywa katika mabenki mbalimbali kwa kuwekwa dhamana. Naye Mwanahisa mkubwa Hazina, hakuridhishwa na uamuzi wa kuuzwa UDA. Mkutano Mkuu wa Wanahisa wa tarehe 10 Juni, 2011, uliosimamiwa na aliyekuwa Meya wa Jiji la Dar es Salaam kuidhinisha uuzaji wa UDA haukuwa halali. Serikali inalijua hili, Bunge la Jamhuri wa Muungano linalijua hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkutano uliitishwa na watu wanne, haukutimiza akidi na ulisimamiwa na mtu mmoja anayeitwa Didas Masaburi, aliyekuwa Meya wa Jiji la Dar es Salaam; Robert Kisena, Mkurugenzi wa Simon Group; Mwanasheria wa Jiji, Issack Nassoro na Mkurugenzi wa Jiji, Philips Mwakyusa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mkutano huo, ndipo ikatangazwa kwamba UDA, Simon Group imetimiza masharti. Taarifa ya Serikali ya Agosti 3, mwaka 2011, kwenda kwa Kamati ya Bunge ya Miundombinu, naomba niinukuu na inasema: “Mkutano ulikuwa batili kwa kuwa ulikiuka Katiba ya UDA Kifungu 45 kutokana kwa kutotimia kwa akidi na kukosekana kwa Msajili wa Hazina. Serikali inakiri kikao hicho hakikuwa na mamlaka ya kufanya maamuzi na maazimio yoyote yaliyofikiwa yalikuwa batili.” Mwisho wa kunukuu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa zaidi wakati kikao cha kugawa hisa za UDA kinafanyika, Meya wa Jiji alipokea barua ya tarehe 28 Februari, 2011 kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, iliyomwagiza kusitisha mara moja mchakato wa kuuza hisa za UDA ambazo hazijagawiwa. Barua kutoka Serikalini (Ofisi ya Waziri Mkuu) ilibeba Kumb. Na. 185/295/07/27.
Barua hii ipo Ofisini mwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali na ipo Hazina, lakini Serikali imeendelea na mchakato wa uuzaji wa UDA kinyume cha taratibu; Serikali imeendelea kumilikisha mali ya umma kinyume cha sheria. Wanakiri katika nyaraka zao zote kwamba mbia hakutimiza masharti yote ya mkataba, lakini bado Serikali inaridhia na tayari Simon Group amelipa shilingi bilioni tano kwenye akaunti ya Jiji la Dar es Salaam kwa ajili ya kumiliki hisa za UDA. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme kwamba maamuzi yaliyofikiwa na Kikao cha Kamati ya Uongozi na Fedha, kilichofanyika juzi cha kuzuia hisa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kuuzwa ninaunga mkono kwa asilimia mia moja. Fedha zilizowekwa katika akaunti ya Jiji hazitarudishwa mpaka hapo Jiji la Dar es Salaam litakapofanya hesabu zake na kuona Simon Group ametumia leseni ya UDA na mali za UDA, ameweka Benki, amepata faida. Tufanye ukaguzi wa ndani kujua ni kiasi gani cha faida alichopata, hapo ndipo tunaweza tukarudisha hizo hela. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli uuzaji wa hisa za UDA na UDA yenyewe na DART yenyewe imegubikwa na udanganyifu, ulaghai, utapeli na Serikali inakiri katika nyaraka zake; na Waziri anakiri na anajua kwamba mchakato wa UDA haukufuata taratibu; lakini wanaendelea na mradi wa uendeshaji wa mabasi yaendayo kasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu umetokana na mkopo wa fedha ambazo Serikali imekopa kutoka Benki ya Dunia, lakini anayetumia barabara zile ni mtu mmoja. Kampuni ya UDA inaulizwa hawa wenye daladala watatumia nini? Wanasema tutawaingiza katika huo mradi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Waziri anapojibu alieleze Bunge hili Tukufu kwa nini mkopo huu ubebwe na Watanzania wote wakati barabara zinatumiwa na mtu mmoja? Ni vizuri mkopo huu ukabebwa na yule anayetumia barabara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nimeona hapa Bungeni, baadhi ya Wabunge wenzangu wanasimama macho yakiwatoka, wakiunga mkono juhudi za Mheshimiwa Rais za kupambana na vita dhidi ya ufisadi. Baadhi yao ukiwaangalia, hawafanani na wanachokisema. Wengine sisi hatukuvamia hili treni la ufisadi, records zipo! Tumepambana Mwenyekiti unajua na Bunge hili Tukufu linajua. Kwa hiyo, sisi wengine tupo tayari kupambana na vita hii hadi mwisho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja hapa imejitokeza na inazungumzwa sana na Waheshimiwa Wabunge, juu ya kuzuia vyombo vya habari kurusha matangazo ya moja kwa moja ya Bunge. Naomba niseme machache mawili na moja, naona Waheshimiwa Wabunge wanamtupia mzigo mkubwa, ndugu yangu Mheshimiwa Nape. Mheshimiwa Nape hahusiki na hili jambo, mnambebesha mzigo asiohusika nao; siyo wake! Tafuteni mwenye mzigo huu. Huu ni uamuzi uliofanywa na vikao vya juu, Mheshimiwa Nape ni wakala tu hapa. Shikeni hao! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaambiwa kwamba Bunge hili linafuata nyayo za Bunge la Uingereza, lakini chini ya Bunge hili, TBC ndiyo ambayo inaendesha hii studio ya Bunge. Kinachoitwa studio ya Bunge ni koti la TBC lililovaa Bunge. Wafanyakazi 15 waliopo hapa nawajua kwa majina, ni waajiriwa wa TBC.
Kwa hiyo, ni hatari sana kuona kwamba Bunge letu linaacha utaratibu wake wa kawaida. Hata huko Uingereza, Bunge linaonyeshwa live, vyombo vya habari vinaonyesha Bunge Live. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalize kwa kusema kwamba mimi nadhani uamuzi huu ni lazima uangaliwe vizuri na busara itumike kuutekeleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, jana Mheshimiwa Zitto amezungumza juu ya hoja ya watu ambao wanapata…
MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa!.....
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ulinde muda wangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee nimalize...
Mheshimiwa Mwenyekiti, namaliza kwa kusema kwamba Mheshimiwa Zitto jana…
MWENYEKITI: Mheshimiwa Kubenea, muda wako umekwisha.