Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Maida Hamad Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi hii ili na mimi nichangie machache katika bajeti hizi za Wizara mbili. Kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia jioni hii ya leo kusimama katika Bunge hili na kuchangia bajeti iliyoko mbele yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie kuhusu ufinyu wa bajeti. Takribani Wizara zote katika bajeti hii zimekabiliwa na ufinyu mkubwa wa bajeti. Kwa hiyo, ni vyema Serikali katika vyanzo vyake vya mapato vilivyopo na vile ambavyo inaendelea kuvibuni siku hadi siku ndani ya bajeti hii iweze kufikiria Wizara tofauti tofauti, hizi tunazozijadili na kuwaongezea ili ziwe na bajeti za kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua majukumu waliyonayo Wizara hizi lakini pia nataka nijikite katika Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma pamoja na ile Tume ya Ajira. Tume hizi zimekuwa zikifanya kazi kwa nguvu zote kwa maslahi ya wananchi na viongozi wa umma walioko katika nchi hii. Tume hizi zimekuwa zikikabiliwa na ufinyu wa bajeti mkubwa na zaidi majengo au ofisi wanazofanyia kazi ni za kupangisha kwa bei ya juu. Vitendea kazi vya kutosha hawana na ukiangalia bajeti yao ilivyo na ukiangalia mahitaji ya fedha ambazo zinatakiwa kulipwa kwa ajili ya ofisi wanazofanyia kazi basi utashangaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunatembelea ofisi hizi, kuna Mheshimiwa mmoja wakati wanatoa changamoto zao alijitolea kuchangia kompyuta pamoja na vifaa vyake. Hii ni aibu jamani, sisi tunakwenda kule kuwapa ushauri na mambo mengine lakini pia sisi sio watu wa kuchangia vifaa vya ofisi hizi wakati ofisi hizi ni muhimu sana katika Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma imekuwa ikifanya kazi kwa nguvu zote, lakini pia cha kusikitisha bajeti yake yote ikiwemo mishahara ya watumishi ni ufadhili kutoka nje, inasikitisha sana. Ni vema Serikali ikajitahidi na ikajikita katika suala la kuongeza bajeti katika ofisi hizi. Mara nyingi tumekuwa tukiwalaumu, tukiwakosoa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwamba hawatekelezi majukumu yao lakini kumbe hawana bajeti, hawana ofisi ya kufanyia kazi, wana-share ndani ya ofisi, wanakaa nje, hawana sehemu nzuri za kufanyia kazi, hawana vifaa vya kutosha lakini pia yote haya yanatokana na ufinyu wa bajeti unaozikumba ofisi hizi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niende moja kwa moja katika mikoa na Halmashauri husika. Waheshimiwa Wabunge wengi hapa wamechangia na kusema kwamba asilimia 30 ya kodi ya majengo ndani ya Halmashauri hazirejeshwi. Wanajitahidi kukusanya kodi hizi lakini pia mrejesho unakuwa hauwafikii. Serikali imewapangia makusanyo kupitia vyanzo vyao vya mapato asilimia 30 kwa mujibu wa bajeti na Halmashauri zimekuwa zikijitahidi sana kukusanya lakini leo kutokana na kuwa hawana mrejesho katika makusanyo kama haya au kodi hizi kwa hiyo imefikia hatua hawawezi kutumia au hawawezi kufaidika na fedha hizi. Pia Halmashauri zetu zina upungufu wa Maafisa Ugani, zina upungufu wa wataalam wa kilimo na hakuna watafiti wa kilimo. Kwa hiyo, ni vyema tukazipa uhuru Halmashauri hizi ili ziweze kujitegemea na kile wanachokikusanya pia tusiwabane sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuweka mfumo sahihi wa matumizi ya electronic kwa kusambaza vifaa vya electronic katika Halmashauri zote ili kuhakikisha kwamba mapato ndani ya Halmashauri hayawezi kuvuja. Yote yanatokana na kuwa hakuna mashine za electronic na ndiyo maana tukaona mapato yanapotea siku hadi siku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie suala la wastaafu. Mara nyingi wastaafu wamekuwa wakiilalamikia Serikali kwamba wanapata usumbufu mkubwa katika kufuatilia haki zao. Baadhi ya changamoto wanazozieleza wastaafu moja ni kutokana na kuwa waajiri hawatekelezi wajibu wao kwa wale wafanyakazi ambao wamejiunga na Mifuko ya Hifadhi jamii ambapo wanakuwa hawafikishi fedha zile mpaka inafikia mfanyakazi anafikia kustaaafu. Pia kuna tatizo la kuchelewa kufikisha nyaraka Hazina. Yote haya inawasababishia wastaafu kuchelewa kupata haki zao na kuja kupata usumbufu baada ya kustaafu. Niiombe sana Serikali kuwafikiria kwanza wastaafu hawa au wastaafu watarajiwa na kuwaomba hizi ofisi kwamba itakapofikia mtu karibu na kustaafu ndani ya miezi mitatu kabla basi nyaraka ziweze kufikishwa mapema kunakohusika ili wastaafu hawa itakapofikia kustaafu waweze kufaidika na wasipate usumbufu. (Makofi)
Kuhusiana na suala la MKURABITA, niipongeze sana Serikali kwa jitihada zake za kufanikisha na suala hili. Pia nitoe pongezi kwamba imeenea katika maeneo mengi Tanzania Bara na kule Zanzibar, wengi wameweza kupimiwa maeneo yao na kupata hati miliki za kimila. Pia niombe sana Serikali kupitia hati hizi za kimila kwa vile tumefungua Benki ya Kilimo wananchi waruhusiwe kuzitumia kama dhamana pale wanapohitaji mikopo kwa ajili ya kuendeleza kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwenye TASAF, mfuko huu ni muhimu sana katika Taifa letu lakini cha kusikitisha pamoja na kazi kubwa inayofanywa lakini pia jamii ni pamoja na wananchi waliotuzunguka katika Majimbo yetu. Sisi Wabunge mara nyingi hatujui nini mfuko unafanya wala kushirikishwa maendeleo yanayopatikana na hata tukihoji basi inakuwa ni kazi ngumu kupata majibu. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali iwashirikishe Wabunge wote wa Jamhuri ya Muungano wawe wa Viti Maalum au wa Majimbo katika maeneo wanayotoka kushirikishwa kwa miradi yote na kwa namna yoyote au hata katika Kamati za TASAF zinazopanga utaratibu mzima kuhusiana na masuala yale ya kijamii na uwezeshaji wake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo, nakushukuru sana.