Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

Hon. John Peter Kadutu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 20 16/2017 - Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora

MHE. JOHN P. KIDUTU: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kukushukuru wewe mwenyewe kunipa nafasi hii kuchangia mchana huu hoja mbili zilizopo ya TAMISEMI pamoja na Utawala Bora.
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijachangia nichukue fursa hii kuipongeza timu yetu ya Bunge kwa ziara nzuri kule Zanzibar, ni katika kuuimarisha Muungano wetu. Nitoe wito kwa niaba ya uongozi wa timu ya Bunge, Wabunge pamoja na Mawaziri tuungane kufanya mazoezi kila asubuhi pale uwanja wa Jamhuri. Mfano mzuri ni wewe Mheshimiwa Naibu Spika umekuwa unatutia moyo kuwepo pale. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo niwapongeze Mawaziri wawili hawa, Ndugu yangu Mheshimiwa Simbachawene pamoja na dada yangu Mheshimiwa Angellah.
Mheshimiwa Naibu Spika, TAMISEMI ni dude kubwa, ukishakabidhiwa Wizara ya TAMISEMI lazima utambue ni dude kubwa na bahati nzuri Mheshimiwa Simbachawene unalijua hilo kwamba TAMISEMI ni dude.
Kwa hiyo, niwapongeze sana kwa hotuba zenu nzuri. Pia nichukue fursa hii kuwapongeza wafanyakazi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua kwa kazi nzuri iliyofanyika mpaka tumepata hati nzuri ndani ya miaka miwili na hasa kwa sababu mimi ndiye nilikuwa naongoza Halmashauri ile kama Mwenyekiti wa Halmashauri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sasa Waziri wangu Mheshimiwa Simbachawene pamoja na Waziri Mkuu wanisikilize kwa makini, iko hoja nilianza kuizungumza wakati nachangia hotuba ya Mheshimiwa Rais, bahati mbaya muda haukuwa rafiki, nayo inahusu waraka aliokuwa ametoa Katibu Mkuu, TAMISEMI wa wakati ule akikataza Mabaraza ya Madiwani kuhoji yale yaliyokuwa yamefanyika wakati Mabaraza yakiwa yamevunjwa. Tarehe 10 Novemba alitoa waraka wa kukataza jambo hilo wakati akielezea taratibu za kuitisha mikutano ya kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ruhusa yako naomba nisome kipengele (g) cha waraka aliokuwa ametoa Katibu Mkuu, TAMISEMI na bahati nzuri mimi niseme ni bahati nzuri kumuondoa pale kunatusaidia kwenye TAMISEMI kukaa vizuri maana makatazo mengine haya hayafai.
Anasema, moja ya kazi za mkutano ule wa kwanza, kipengele (g) anasema; “Kupokea taarifa ya Mkurugenzi wa Halmashauri kuhusu kumbukumbu ya maamuzi ya utekelezaji wa shughuli za Halmashauri zilizofanyika katika kipindi ambacho Baraza la Madiwani lilivunjwa.” Akaweka msisitizo kwenye maandishi; “Wajumbe wa Baraza watapokea taarifa hiyo ya utekelezaji na kuijadili bila kubatilisha maamuzi yaliyofikiwa.” Maneno haya siyo mazuri kwa kazi nzuri inayofanywa na Halmashauri. Tukiwa na watendaji ambayo si wazuri maneno haya wanaweza kuyatumia kufanya wanalotaka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa nini Baraza la Madiwani lizuiwe kuhoji yale yaliyofanyika? Tunao ushahidi kesho yake Madiwani wanarudi yamefanyika jana yake. Sasa kama umewakataza wasijadili maana yake unawakataza haki yao. Kwani kuna ubaya gani Bunge hili likajadili kazi ya Bunge iliyofanyika huko nyuma? Kwa hiyo, kazi kubwa lazima ifanyike hapa. Niombe Mheshimiwa Waziri toa tu tamko ili kufuta Waraka huu nadhani watu wengine huwa wanalewa madaraka, hilo lilikuwa la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kuna ahadi ya Rais Mstaafu, Mheshimiwa Jakaya Kikwete wakati wa kampeni za mwaka 2010, eneo letu lilikumbwa na mtafaruku katika kulizimazima jambo lile, Mheshimiwa Kikwete akaahidi Ulyankulu kuwapatia Wilaya pamoja na Halmashauri. Bahati mbaya mtani wangu huyu Mkwere kaondoka hatujapata Halmashauri kule na wala Wilaya haijapatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wakati Mheshimiwa Rais anapita kwenye kampeni za uchaguzi uliopita na yeye akasisitiza jambo hili kuwapatia wananchi wa Ulyankulu Wilaya pamoja na Halmashauri. Kwa kweli wananchi wana imani hiyo kwamba upo utaratibu wa kuhakikisha jambo hili linakamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niombe basi Serikali ije na majibu wakati wa kujibu suala hili limefikia wapi ikizingatiwa kwamba ahadi zimetolewa toka mwaka 2010. Wapo watu hapa wanasema tuzuie kuanzisha maeneo mapya ya utawala. Zinaweza zikawepo sababu kule unapotoka wewe kuna kaeneo kadogo, ukitembea saa tatu umemaliza jimbo lako lakini kutembea Jimbo la Ulyakulu Mheshimiwa Waziri Mkuu unajua ni kati ya majimbo makubwa na lenye watu wengi. Kwa hiyo, tunahitaji jambo hili likamilike ili wananchi wawe na imani, tupate wilaya na Halmashauri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, maslahi kwa Madiwani. Jamani zile pesa Wabunge mnazopata mwishoni Madiwani wanapata shilingi milioni 11, ni kiasi kidogo mno, hebu tuwasaidie. Kama hatuwapi hizi stahili zao za kila siku, zile za mwisho basi wapate. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la magari, yapo magari yamekwishakuwa allocated, tulizungumza nina imani utakuja na majibu hapa. Watu wanashindwa kukagua miradi kwa sababu magari hakuna lakini magari yameshakuwa allocated muda mrefu yapo yard kwa nini yasiende site yakafanye kazi? Bila shaka jambo hili litakaa vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni juu ya fedha za Serikali Kuu kwenda kwenye Wilaya, speed ya pesa kwa maana ya bajeti ni ndogo sana. Kufikia Machi Halmashauri ya Kaliua ilikuwa imepelekewa asilimia 62 tu lakini kwa mwaka jana pesa zilizoletwa kwa ajili ya maendeleo ziliishia asilimia 30 asilimia 70 hazikuletwa. Kwa hiyo, jambo hili linafanya miradi mingine iende kwa kusuasua sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, liko suala lingine la hizi Sekretarieti za Mikoa kuingilia kazi za Halmashauri. Ni sehemu yao ya kazi lakini mara nyingine wanaingilia shughuli za Halmashauri katika hali ambayo inafanya hata ikosekane maana ya kuwepo Madiwani. Baraza linaamua hivi lakini Sekretarieti za Mikoa zinaingilia kati na maamuzi mengine yanakuwa ya hasara kwa Halmashauri. Kwa hiyo, niombe basi Mheshimiwa Waziri utupe mwelekeo mzuri lakini hizi Sekretarieti za Mkoa ziweze kuzuiwa na ziache mambo mengine ambayo yanaamuliwa na Halmashauri kwa maana ya Madiwani na Baraza lao waweze kutekeleza mambo yao yaende vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, michezo kwa shule za msingi na sekondari. Nimekuwa nikisema yupo mzee wetu mmoja nadhani alilewa au uzee au vipi alikataza michezo kwenye mashule. Nishukuru Serikali sasa michezo inachezwa, lakini iko haja ya kuongeza nguvu kwa maana ya bajeti ya ile michezo ya shule za msingi pamoja na sekondari kwa maana ya UMISETA. Pesa inayopelekwa kwa ajili ya michezo hii ni ndogo mno kiasi kwamba michezo haina tija yaani mafanikio ya michezo hii yanakuwa madogo kuliko kawaida. Kwa hiyo, niombe Mheshimiwa Waziri ulitolee ufafanuzi jambo hili ili mambo yaende vizuri.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa muda wako umekwisha.
MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi hii, niseme tu naunga mkono hoja.