Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, WASANII NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti nakushukuru, ahsante kwa kunipa nafasi nami nichangie kwenye hoja. Kwanza nimpongeze sana Waziri wa Mambo ya Ndani na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayofanya. Najua, yako maneno mengi watawasema lakini sisi wenzako tunajua unafanya kazi nzuri na tunakuunga mkono endelea kufanya kazi hiyo.
Pili, nilipongeze sana Jeshi letu la Polisi kwa kazi nzuri waliyofanya na hasa wakati wa uchaguzi mwaka jana. Uchaguzi ule umekwisha kwa amani na utulivu kwa sababu ya kazi nzuri iliyofanywa na Jeshi la Polisi. Jeshi la Polisi endeleeni kufanya kazi hiyo, msisikilize kejeli zinazoelekezwa kwenu, Watanzania wanajua mnafanya kazi nzuri pamoja na mazingira magumu endeleeni kufanya kazi hiyo nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ambalo nilidhani ni vizuri tukaliweka sawa. Hapa pamefanyika utaratibu ambao ulifikia uamuzi wa Kamati ya Kanuni kwenda kushughulika na hotuba ya Kambi ya Upinzani Bungeni. Bahati mbaya sana ninachokiona hapa, kunatengenezwa upotoshaji kama vile kulikuwa na hoja ngumu, nyingi Serikali imeziona, ikaona tabu kuzijibu, kwa hiyo ikatengeneza utaratibu wa kukimbia. Utaratibu huu wa kupotosha mambo, unaendelea sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo liko wazi, kila mahali na hapa Bungeni pana utaratibu wake, wenzetu wamezoea kunyonga, wanapoambiwa kuchinja wanapata tabu. Mimi wala sipati tabu na kelele zao kwa sababu ndivyo walivyofundishwa, wasipoipenda hoja wanatakiwa wazomee, endeleeni kuzomea. Hata hivyo, nataka tuweke jambo hili sawa, kilichofanyika hapa ni utaratibu wa kawaida wa Kibunge, kuna kanuni zake, wamekwenda wamekaa wameshauriwa, hawataki walichoshauriwa wameamua wenyewe kuweka mpira kwapani na kuondoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni vizuri Watanzania wakaujua ukweli huu kwamba wenzetu hawapendi kufuata kanuni na taratibu ndiyo maana wanafanya walichofanya na ndiyo maana hata humu ndani wataendelea kuzomea kwa sababu ndiyo taratibu zao.
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, WASANII NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hili lilikuwa la kwanza na nadhani limeeleweka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, imetolewa hoja hapa kwamba, Serikali hii haina uwezo wa kuongoza nchi, lakini nataka nimwambie Mchungaji wangu Msigwa, Watanzania ndiyo wametupigia kura, wakatuamini, wakatuleta hapa na kwa muda mrefu siyo jana wala juzi, mmekuwa mkiwaomba wawaamini wamekataa kuwaamini. Wameendelea kutuamini siye na wanatuamini kwa sababu wanaamini tunaweza, tunajua na ndiyo maana wameendelea kutupa na wataendelea kutuamini kuturudisha hapa.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mmeendelea kutoaminiwa kwa sababu ya ukigeu geu mnaoendelea nao mpaka leo, kwa hiyo tupo hapa kwa sababu Watanzania wanataka tuwe hapa, wanatuamini na wataendelea kutuamini na kwa kazi nzuri tunayoifanya, wataendelea kutuamini, kwahiyo hili halina mjadala.
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, WASANII NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya mwisho. Imetolewa hoja hapa pia, inatuhumu kwamba Jeshi la Polisi limekuwa likitumiwa na Chama cha Mapinduzi hasa kwenye uchaguzi. Nadhani hili nalo si suala la kuliacha liendelee kuzungumzwa, kama Jeshi la Polisi na hapa maneno haya ni ya kulidharau na kulidhalilisha Jeshi la Polisi na ndiyo maana Mheshimiwa Lwakatare anasema, hawa jamaa laini sana maana yake Jeshi la Polisi laini sana. Hivi kama kweli…
MWENYEKITI: Order. Ahsante Mheshimiwa Nape.
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, WASANII NA MICHEZO: Naunga mkono hoja.