Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuchangia katika hoja hii. Kwanza nianze kwa kusema naunga mkono hoja ambayo kwa kweli imesheheni namna ambavyo Serikali imetekeleza mipango ya maendeleo kwa ajili ya kuimarisha uchumi wetu na ustawi wa Watanzania. Pia hoja hii imeweza kuonesha Watanzania namna ambavyo Serikali imeendelea kujipanga na kuweka mipango ya mbele katika kuendelea kuimarisha uchumi na maendeleo ya Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii nimshukuru kwa dhati Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuniamini na kunipa nafasi ya kuwa msaidizi wake katika nafasi hii ya Waziri wa Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye ulemavu. Kipekee nimpongeze kwa dhati Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ametimiza miaka miwili ya uongozi wake na ni hakika ni miaka miwili ya mafanikio makubwa.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge ambao wamesimama kuchangia hapa kila mmoja ameelezea namna ambavyo katika maeneo yake katika jimbo lake ameguswa. Tanzania yote hii imeshuhudia uongozi uliotukuka wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Ni kiongozi bora, kiongozi imara, kiongozi shupavu na tunamwombea kwa Mwenyezi Mungu aendelee kumpa afya njema na maono zaidi ili aendelee kulitumikia Taifa letu na tuendelee kupata mafanikio. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nimshukuru Mheshimiwa Makamu wa Rais pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu. Viongozi hawa wawili pia wamekuwa wakinipa miongozo na maelekezo ambayo yameniwezesha kutekeleza majukumu yangu. Naomba niwaahidi viongozi wangu nitaendelea kuwa mtumishi mwaminifu na nitafanya kazi zangu kwa weledi kwa maslahi mapana ya Taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee naomba nikupongeze wewe, Spika wetu mahiri, Spika wa viwango kwa hakika unatuheshimisha sana Wabunge. Nakupongeza wewe pamoja na Naibu Spika pamoja na Wenyeviti wetu wa Bunge kwa kazi nzuri wanazofanya na Wenyeviti wote wa Kamati kwa kweli pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote ambao kwa hakika mnatupa ushauri na maoni na mapendekezo yenu yameendelea kuwa chachu ya sisi kujituma zaidi kwa sababu mnawakilisha wananchi. kwa hiyo, lazima tuwasikilize, lazima tufanyie kazi mapendekezo yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nishukuru kipekee Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii chini ya uongozi wa Mwenyekiti, Dada yangu Mheshimiwa Fatma Toufiq kwa namna ambavyo wanatupa ushirikiano, ushauri na maelekezo. Wakati wa kuchambua bajeti hii kuna mambo mengi walitushauri na tuliyazingatia wakati tunaandaa bajeti yetu.

Mheshimiwa Spika, naomba nimpongeze dada yangu, pacha wangu Mheshimiwa Jenista Joakim Mhagama kwa kuteuliwa kuwa Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu na nimwahidi kwamba tutafanya kazi kama ilivyo kawaida yetu, kwa weledi wa hali ya juu. Namshukuru kaka yangu Mheshimiwa Boniface Simbachawene ambaye tumefanya naye kazi vizuri mpaka hapo Mheshimiwa Rais alipomteua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee namshukuru Naibu Waziri wangu, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote wa Wizara kwa ushirikiano mkubwa wanaonipa, bila kuwaacha wadau wangu wa utatu; Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania pamoja na Chama cha Waajiri Tanzania kwa ushirikiano mkubwa wanaonipa, pamoja na washirika wa maendeleo; ILO, UNICEF, UNDFPA pamoja GIZ. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee niwashukuru pia wapiga kura wangu Jimbo la Kasulu Mjini ambao ndio wamenipa heshima ya kuwa katika Bunge hili, na niwaahidi kwamba nitaendelea kuwatumikia kwa moyo wangu wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya shukrani hizo, naomba sasa nijibu baadhi ya hoja za Wabunge. Naomba nianze na suala ambalo Waheshimiwa Wabunge wamechangia kuhusu maslahi ya wafanyakazi na hususan wakazungumzia maslahi ya wafanyakazi katika sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, niwaambie katika pongezi ambazo nimempa Mheshimiwa Rais katika miaka miwili ya uongozi, kama kuna eneo ambalo Mheshimiwa Rais ameligusa na ameweka alama ni kwenye suala la watumishi wa umma na kwenye sekta binafsi.

Mheshimiwa Spika, Serikali inawathamini wafanyakazi na mchango wao na kupitia Bodi ya Kima cha Chini cha Mishahara tumeweza kutoa amri kupitia Gazeti la Serikali Na. 687 ambalo lilichapishwa tarehe 25 mwezi wa 11 ambapo kima cha chini cha mishahara kwenye sekta binafsi kimeongezwa na utekelezaji umeanza tarehe 1 Januari, 2023.

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kuendelea kusisitiza waajiri ambao bado wana uzito wa kutekeleza amri hii ni kuwaambia kwamba ni haki ya wafanyakazi kupata mshahara kama ambavyo imeainishwa katika amri ya kima cha chini cha mishahara. Kwa hiyo, katika kaguzi zetu tutaendelea kufuatilia ili kuhakikisha kwamba wafanyakazi wanalipwa kama ambavyo Bodi ya Kima cha Chini cha Mishahara imependekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo jingine ambalo limezungumziwa ni masuala ya malipo ya mafao ya wastaafu na hata mchangiaji ambaye amezungumza asubuhi hii ya leo amezungumza pia kwamba kuna wastaafu ambao hawalipwi kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, naomba niseme kwamba ulipaji wa mafao kwa wastaafu umeimarishwa kwa kiwango kikubwa na changamoto zilizokuwepo ambazo zilikuwa zinasababisha wastaafu wasilipwe kwa wakati, Serikali hii ya Awamu ya Sita tayari imezifanyia kazi na changamoto kubwa iliyokuwepo ilikuwa ni ukwasi.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na deni la wafanyakazi waliorithiwa kutoka kwenye mfuko uliokuwa PSPF ambao wafanyakazi kabla ya mwaka 1999 walikuwa hawachangii. Kwa hiyo, Serikali ilivyowaingiza kwenye mfuko ikawa imeahidi kwamba itawalipia michango kiasi cha shilingi trilioni 4.6 na ninaomba niliambie Bunge lako tukufu. Serikali ya Awamu ya Sita tayari ukiangalia katika Hotuba ya Waziri Mkuu ukurasa wa 67 aya ya 124; Serikali imeeleza kwamba tayari kiasi cha shilingi trilioni 2.17 kimelipwa. (Makofi)

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, kwa sababu hoja ni ya Waziri Mkuu kwa hiyo Mawaziri chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu wanajikuta na wao wako katika mazingira ya kuchangia lakini hoja inapokuwa inahitimishwa na Waziri kikanuni haiwezi kupewa taarifa. Kwa hiyo, tuwe tumeelewana vizuri. Mheshimiwa Ndalichako kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ester Bulaya.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Ndalichako kwamba suala la ukwasi kwenye PSSF bado lipo na kama anasema limeisha niko tayari ku-resign Ubunge na mpaka sasa hivi kwa mujibu wa sheria ukwasi inatakiwa iwe 40%. Mpaka sasa hivi kwa taarifa latest bado 22% na suala la fedha ambazo unasema zimelipwa, ile ni hatifungani na bado mifuko iko kwenye hali mbaya.

SPIKA: Mheshimiwa Ester Bulaya, ukwasi huo wa kiasi ulichotaja wewe mwenyewe kabla sijarudi kwa unayempa taarifa unatosheleza kulipa watu mafao ama hautoshelezi, ukwasi huo huo wa asilimia ishirini na ulizozisema wewe.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, ukwasi huo kwenye hii mifuko hautoshelezi na ndiyo maana mifuko inaenda kuchukua mpaka kwenye fedha za michango. Mpaka fedha za michango unakwenda kukopa kwenye maeneo mengine. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Ndalichako unaipokea taarifa hiyo?

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, siipokei taarifa yake kwa sababu kwanza kazi ya michango ndiyo pamoja na kulipa mafao. Wanakusanya ili pia waweze kulipa mafao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nimeeleza deni ambalo Serikali imelipa kupitia hatifungani shilingi trilioni 2.16. Taarifa ya ukwasi anayoizungumzia Mheshimiwa Ester Bulaya ilifanyika mwaka 2020. Leo hii tuko mwaka 2023, kabla ya hapo deni lilikuwa halijalipwa na pamoja na hizi fedha hatifungani ya shilingi trilioni 2.17 lakini pia kulikuwa na madeni mengine ambayo yanatokana na uwekezaji Serikali imelipa shilingi bilioni 500 katika mifuko ya hifadhi ya jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba niendelee.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la ucheleweshwaji wa malipo kwa wastaafu, naomba nilihakikishie Bunge lako kwamba mifuko ya hifadhi ya jamii imeimarisha mifumo yake ya ulipaji wa mafao kwa wastaafu na inalipwa kwa wakati. Kama kuna ucheleweshwaji wowote, basi naomba tupate taarifa lakini niwahakikishie Bunge kwamba sasa hivi Mfuko wa NSSF, Mfuko wa PSSF unalipa mafao ya wastaafu ndani ya muda ambao umewekwa kisheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inawezekana ikatokea kuna tatizo la michango ya mtumishi ambaye anastaafu, hiyo itakuwa ni case tofauti. Nazungumzia mtu ambaye amestaafu, michango yake iliwasilishwa na taarifa zake zimekuja kwenye mfuko analipwa mafao yake ndani ya muda ambao umewekwa kwa mujibu wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge, naomba nichukue nafasi hii kutoa wito kama kuna mtu yeyote ana changamoto zozote za kulipwa kwa wakati atoe taarifa ili tuweze kuifanyia kazi lakini kwa maana ya mifuko, mifumo iko imara na wastaafu wanalipwa mafao yao ndani ya muda ambao umewekwa kisheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala ambalo lilizungumziwa la kuimarisha mahusiano kazini na kuhakikisha kwamba mabaraza ya wafanyakazi yana fanya kazi vizuri. Kwanza niliambie Bunge lako tukufu sasa hivi tumeimarisha usimamizi kuhakikisha kwamba mabaraza ya wafanyakazi yanaundwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nitoe wito kwa waajiri kuhakikisha kwamba mabaraza haya ya wafanyakazi ambayo yameundwa yanafanya kazi kwa mujibu wa sheria. Watoe nafasi kwa wafanyakazi kufanya vikao kama ambavyo inatakiwa kwa mujibu wa sheria na ofisi yangu kupitia kwa Kamishna wa Kazi tutaendelea kufuatilia ili kuhakikisha kwamba wanafanya kazi kama inavyotakiwa.

Mheshimiwa Spika, pia umetolewa ushauri kwamba tuendelee kuimarisha Baraza letu la Ushauri na Masuala ya Kazi, Uchumi na Kijamii LESCO ili liweze kufanya majukumu yake ipasavyo. Nikuhakikishie kwamba Serikali imejikita katika kuhakikisha kwamba inashughulikia masuala ya wafanyakazi kwenye Sekta ya Umma na Sekta Binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baadhi ya mambo ambayo yamefanyika kupitia LESCO katika kipindi cha mwaka wa fedha huu ambao tunauzungumzia. Kwanza ni kutoa ushauri kuhusiana na kima cha chini cha mishahara ambacho kimeshatangazwa kwenye Gazeti la Serikali cha mwezi Novemba na kimeanza kutekelezwa mwezi Januari.

Mheshimiwa Spika, pia LESCO imetoa ushauri katika kanuni za sheria ya usalama na afya mahali pa kazi ambazo nazo zinaanza kutumika. LESCO imetoa ushauri kuhusu viwango vya posho kwa madereva ambao wanasafirisha shehena za mizigo kwenda nje ya nchi. Waheshimiwa Wabunge mnafahamu kwamba kuna kipindi hali ya upande wa usafirishaji ilikuwa inakuwa tete kutokana na changamoto za madereva kutopata maslahi yao vizuri lakini kupitia LESCO tumeweza kufikia mahali ambapo kumekuwa na viwango ambavyo vimependekezwa na tayari vinatumika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie jambo jingine kuhusiana na kanuni ya mafao kwa watumishi wa umma almaarufu kama kikotoo. Kumekuwa na upotoshaji mkubwa kuhusiana na hii kanuni ya mafao kwa watumishi na labda hapa nitatumia muda kidogo ili tuweze kwenda vizuri na nitumie fursa hii pia kutoa elimu hata kwa wafanyakazi ambao watakuwa wanatufuatilia kwenye Bunge hili.

Mheshimiwa Spika, kanuni hii ya kukokotoa mafao kwa watumishi wa umma ambayo imeanza kutumika tarehe 1 Julai, 2022 imetokana na sheria Na. 2 ya mwaka 2018 ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii ambayo ndiyo ilianzisha Mfuko wa Watumishi wa Umma PSSSF na iliunganisha mifuko minne; Mfuko wa GEPF, LAPF, PPF na PSPF. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla ya kuunganisha mifuko hii, mifuko hii ilikuwa na kanuni tofauti za ulipaji wa mafao. Mfuko wa GEPF na PPF ulikuwa unalipa mafao ya mkupuo ya 25% na mfuko wa LAPF pamoja na Mfuko wa PSPF ulikuwa unalipa mafao ya mkupuo ya 50%.

Mheshimiwa Spika, vile vile tulikuwa na mfuko kwa ajili ya watumishi kwenye sekta binafsi, NSSF ambao ulikuwa unatoa mafao ya mkupuo ya 25%. Baada ya kuunganisha mifuko kulikuwa na ulazima wa kuiainisha kanuni. Huwezi ukawa na mfuko mmoja ambao unalipa wanachama wake kwa kutumia kanuni tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mwaka 2018 ziliundwa kanuni kwa ajili ya kutekeleza sheria hii ambazo ziliweka watumishi wote walipwe mafao ya mkupuo ya 25%. Sasa baada ya kutunga kanuni hizo waliokuwa wanapata mafao ya 50%.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Profesa Ndalichako kuna taarifa. Waheshimiwa Wabunge, kwa kutazama muda wetu taarifa hiyo itakuwa ya mwisho.

T A A R I F A

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nadhani Mheshimiwa Waziri kwanza anatakiwa akiri hapa, mifuko iliunganishwa kwa sababu Mfuko Mkubwa wa PSSF ulikuwa kwenye hali mbaya na ulikuwa unakufa. Huo ndiyo ukweli wa kwanza ambao aukiri kwa sababu anafahamu kabla mifuko haijaunganishwa, deni la PSSF kwa Serikali ya pre 1999 and past 1999 ilikuwa zaidi ya shilingi trilioni saba. Kwa hiyo, wakaenda kufanya uhakiki wakaja na shilingi trilioni 4.5 waliokuwa wanataka kuisema? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hilo la kwanza lakini la pili.

SPIKA: Haya ahsante sasa taarifa ni moja Mheshimiwa.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo akiri siyo anaongea vitu ambavyo havipo.

SPIKA: Mheshimiwa sasa wewe unampa taarifa au unamuuliza swali?

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nampa taarifa na ushauri.

SPIKA: Wewe umempa taarifa kwa hiyo ana uamuzi wa kupokea taarifa yako au hapana. Sasa ukimwambia akiri maana yake umemuuliza swali. Mheshimiwa Prof. Ndalichako unipokea taarifa hiyo au hapana?

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, siwezi kuipokea taarifa kwa sababu hata yeye mwenyewe mtoa taarifa naona hata haelewi anazungumza anataka sijui. Kwa hiyo, siipokei taarifa yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee kwa sababu nilikuwa naeleza na Waheshimiwa Wabunge naomba tuwe na utulivu tusikilize kwa sababu nilichokuwa naeleza na yeye anachoingilia sasa ilikuwa ni kitu tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mifuko hiyo baada ya kuunganishwa na kanuni zikatengenezwa zilikuwa zinalipa watumishi wote mkupuo wa 25%. Sasa baada ya kanuni hii kuanza kutumika ni dhahiri kwamba wale waliokuwa wanalipwa 50% kutoka 50% mpaka 25% walikuwa wanaona wameshushwa mahali pakubwa. Kwa hiyo, kukawa na malalamiko na Serikali hii ni Sikivu, Serikali ikasema kwamba isitishe kuendelea kutumia na hizo kanuni tukae chini tukutane na wafanyakazi na wadau wanaohusika tuje na kanuni ambayo…

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, kuna taarifa.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: …itawakutanisha watumishi katikati. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, baada ya majadiliano na kushirikishana, taasisi ambazo zinahusika na wafanyakazi ndiyo tumekuja na kanuni ya 33%. Kwa hiyo, kanuni hii lengo lake ilikuwa inataka kuwakutanisha katikati waliokuwa wanapata 50% na waliokuwa wanapata 25%. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niliambie Bunge lako tukufu, kanuni hii ambayo ya 33% imeongeza mafao ya mkupuo kwa wanachama 1,364,050 sawa na 81% ya wanachama wote, waliokuwa wanapata 25%. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, watumishi kwenye taasisi zote za umma mafao yenu yameongezeka kutoka 25% mpaka 33%. Watumishi kwenye sekta binafsi kupitia kanuni hii, mafao yenu ya mkupuo yameongezeka.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, kanuni hii kuna wafanyakazi 326,137 sawa na 19% ndiyo hao ambao walikuwa wana 50% wamekuja kwenye 33% lakini mafao yao ya pensheni kwa mwezi yameongezeka. Walikuwa wanlipwa 50% sasa wanalipwa 67%. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimeona nitoe ufafanuzi huo kwa sababu jambo hili linakuwa linaongelewa kana kwamba yaani wafanyakazi wote wameshushiwa. Wafanyakazi 81% mafao yao ya mkupuo yameongezeka. Wote waliokuwa wanachama wa PPF waliokuwa wanachama wa GEPF, NSSF mafao yao yameongezeka kutoka mkupuo wa 25% kwenda kwenye mkupuo wa 33%. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba nimalizie kwa kushukuru tena kwa nafasi hii ambayo nimeipata ya kuchangia na naomba niseme naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)