Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze sana Waziri wa Afya Ndugu Ummy Mwalimu na Naibu wake Dkt. Godwin Mollel na wataalamu wa Wizara kwa kazi nzuri wanazofanya.

Mheshimiwa Spika, mimi nitachangia kuhusu changamoto zifuatazo nikianza na changamoto ya matibabu kwa wazee wenye ugonjwa wa kisukari na kuishia kukatwa viungo kama miguu. Pia sheria inayokataza uwepo wa maduka ya dawa mita 500 kuzunguka Hospitali za Serikali

Mheshimiwa Spika, wazee wanaougua ugonjwa wa kisukari na kukatwa miguu hupitia changamoto kubwa ya gharama kwa kutakiwa kulipia fedha nyingi kununua miguu ya bandia. Gharama za miguu miwili ni kubwa. Kuna mgonjwa amenilalamikia kuwa mwaka wa 2019 alinunua miguu bandia kwa thamani ya shilingi milioni tano ikiwa na silicone liner. Mgonjwa huyu huyu mwenye umri wa miaka 68 ameniambia kuwa mwaka huu wa 2022 anatakiwa alipe shilingi milioni tatu kuikarabati.

Mheshimiwa Spika, wazee waliokumbwa na ugonjwa huu na kukatwa miguu wanakuwa hawana uwezo wa kushiriki tena katika shughuli za uzalishaji na kujipatia kipato. Kwa gharama hizi, huu ni mzigo mkubwa kwa wagonjwa wa kisukari na wanaoshindwa kulipia huishia kufa kwa mateso.

Mheshimiwa Spika, kuna sheria inayokataza uwepo wa maduka ya dawa mita 500 kuzunguka hospitali za Serikali. Uwepo wa sheria iliyo kwenye GN 269 ya Aprili, 2020 ulitoa kipindi cha mpito cha miaka miwili kuitekeleza, na sasa iko kwenye hatua za utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, sheria hii inayokataza uwepo wa maduka ya dawa mita 500 kuzunguka hospitali za Serikali kwa hisia kwamba baadhi ya wataalamu wa Wizara ya Afya wanaihujumu Serikali kwa kuiba dawa na kuziuza maduka ya karibu au huwa na maduka karibu na hospitali za Serikali na huishia kuyakuza maduka yao.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni Waziri wa Afya Mheshimiwa Ummy Mwalimu alitoa agizo la kuondolewa kwa maduka yote ya dawa ambayo yapo mita 500 ndani ya eneo la hospitali za Serikali kwa kile kinachodaiwa kuhujumu upatikanaji wa dawa katika hospitali hizo. Tangazo hili lilisababisha taharuki kubwa nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa mawazo yangu, sheria hii ilipotungwa haikuzingatia maslahi ya wagonjwa wa Kitanzania na wamiliki wa maduka binafsi ya dawa yaliyo karibu na hospitali. Maduka haya yapo kusaidia upatikanaji wa dawa na vifaa vya tiba kwani Serikali yenyewe bado haina uwezo wa kusambaza dawa zote na vifaa tiba kwa wagonjwa.

Mheshimiwa Spika, hii sheria ina mapungufu, mimi naona hakuna mwananchi anayependa kwenda nje ya hospitali kutafuta dawa au vifaa tiba bali changamoto za uhaba wa dawa na vifaa tiba zilizopo ndani ya hizo hospitali ndio zinafanya waende nje.

Mheshimiwa Spika, madhumuni ya kuanzisha sheria hii yanakinzana kabisa na uhalisia uliopo. Tatizo kubwa lililopo Wizara ya Afya ni katika mfumo mzima wa ugavi, usambazaji na usimamizi wa dawa na si uwepo wa maduka ya watu binafsi ya dawa karibu na hospitali za Serikali. Watumishi wasio waaminifu wakiiba na kutoa dawa nje ya hospitali, dawa inaweza kwenda popote nje ya hospitali na hata mikoa ya mbali kwa haraka kwa kutumia mbinu mbalimbali zikiwemo bodaboda. Ninachokiona si kweli kwamba maduka yaliyo karibu na hospitali ndio wateja wa wizi wa dawa kutoka hospitali za Serikali.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu, napenda kuishauri Serikali yafuatayo; Serikali igharamie viungo bandia (kama miguu bandia) pamoja na ukarabati wake kwa wahanga wa kisukari waliokatwa miguu hususan wazee; gharama za viungo bandia kwa wagonjwa wa kisukari viingizwe kwenye bima ya afya; na Waziri wa Afya kwa kushauriana na Waziri wa Katiba na Sheria wafute sheria inayokataza uwepo wa maduka ya dawa mita 500 kuzunguka hospitali za Serikali.

Mheshimiwa Spika, kwa kufanya hivyo tutawapunguzia wananchi adha ya kutafuta dawa na vifaa tiba wanazoandikiwa kwenda kununua nje ya hospitali za Serikali; Wizara ya Afya itambue kwamba ilitoa vibali mbalimbali vya kuanzisha maduka ya dawa. Kufunga biashara zao kutasababisha hasara kubwa kwa hawa wawekezaji wazalendo na kuikosesha Serikali mapato; maduka ya watu binafsi ya dawa hasa yale yaliyo karibu na hospitali husaidia upatikanaji wa dawa kirahisi kwani Serikali yetu yenyewe bado haina uwezo wa kutoa dawa zote na vifaa tiba; na kufuta hii sheria kutaonesha hawajali wafanyabiashara na wawekezaji wa biashara ya dawa na vifaa tiba hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.