Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa nafasi hii ya kuniwezesha na mimi kutoa mchango mdogo katika Wizara hii ya Afya. Kabla sijaendelea ninaomba niunge mkono hoja iliyopo mezani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba nitumie nafasi hii kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wenzangu wameweza kumpongeza kwa kuongeza mishahara ya Watumishi wa Umma jambo ambalo linaenda kupelekea ongezeko la mzunguko wa fedha ndani ya nchi yetu. Pia nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa jinsi ambavyo anaendelea kuipa kipaumbele sekta hii ya afya na hasa kibajeti. Tunaona bajeti ya afya jinsi ambavyo Mheshimiwa Waziri amei-present imekuwa na mambo mengi ambayo yanatoa tumaini la sekta hii kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba pia nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimwia Waziri Ummy Mwalimu Dada yangu kwa jinsi ambavyo anaendelea kuchapa kazi yeye pamoja na timu yake ya Wizara ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mnamo tarehe 12 mwezi wa Nne mwaka huu niliweza kuuliza swali lakini pia Januari mwaka huu niliweza kuuliza swali nikitaka kufahamu mpango wa Serikali ni jinsi imejipanga kuona kwamba inaandaa vyumba maalum vya kujifungulia wanawake wenye ulemavu. Ninaishukuru Serikali kwa jibu ambalo lilitolewa lakini mpango ambao ulitolewa ni mpango wa muda mrefu kutokana na umuhimu na unyeti wa jambo hili niiombe Serikali iliangalie jambo hili kwa jicho la tatu, kwa kuja na mpango wa muda mfupi ambao utawezesha upatikanaji wa vyumba hivi vya kujifungulia wanawake wenye ulemavu kwa haraka, tofauti na ambavyo sasa kwenye jibu lile ilisema kwamba wameandaa ramani ambazo zimeandaliwa sasa hivi kwa maana ya vituo vya afya ama hospitali ambazo zitajengwa basi zitazingatia jambo hili, ninaiomba sana Serikali iliangalie jambo hili kwa jicho la tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kumpongeza Mkurugenzi Mtendaji wa CCBRT Ndugu Brenda Msangi jambo hili aliposikia tu nilipouliza kazi swali yeye alilifanyia kazi kwa haraka sana na hivyo pale CCBRT sasa hivi wanawake wenye ulemavu wanajifungua vizuri na wanafurahia kuleta viumbe duniani kama wanawake wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba pia nichangie kwenye eneo la wagonjwa wa akili lakini mimi nipo tofauti kidogo na wachangiaji ambao wamepita. Kwa kadri ambavyo nilikutana na kundi hili ambalo pia ni kundi ambalo ninaliwakilisha, waliweza kuzungumzia changamoto ya upatikanaji wa dawa za wagonjwa wa akili. Dawa hizi kuna changamoto kubwa ya upatikanaji wake lakini hata zinapopatikana zinapatikana kwa gharama kubwa, hivyo niiombe sana Serikali iweze kuangalia kwamba dawa hizi ziweze kupatikana kwa gharama nafuu lakini pia ziweze kupatikana kwa wingi kwa kadri ambavyo wamekuwa wakizihitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la mwisho ambalo ninaomba nilichangie ni kuhusiana na upatikanaji wa matitabu kwa watu wenye ulemavu. Hata mwaka jana kwenye bajeti niliweza kuchangia lakini pia Mheshimiwa Waziri alipokuwa anawasilisha bajeti yake mwaka jana aliweza kuongelea mpango mzuri ambao umeandaliwa kwa wazee na mimi nikatumia nafasi hiyohiyo kwamba Serikali sasa inaonaje kwenye ule mpango mzuri wa wazee, alisema zimeandaliwa t-shirt wazee kwanza, nikasema kwa nini Serikali sasa isiongeze neno ikawa kwamba wazee na watu wenye ulemavu kwanza ili kuweza kuleta huduma hii ya matibabu kiurahisi kwa watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina ufahamu mpango mzuri ambao unaandaliwa na Serikali, Serikali ya Awamu ya Sita kuhakikisha kwamba Watanzania wote wanakuwa na Bima za Afya hili ninalitambua lakini kwakuwa bado tupo kwenye mchakato katika kipindi hiki cha mpito basi Serikali iweze kuona utaratibu mzuri wa kundi hili kuweza kupatiwa matibabu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa nafasi, ahsante sana. (Makofi)