Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti ya Wizara ya Afya. Kwanza napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu Mheshimiwa Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya kuliletea maendeleo Taifa letu la Tanzania ikiwemo kwenye sekta hii ya afya.

Mheshimiwa Spika, pili, napenda kuwapongeza Mheshimiwa Waziri wa Afya, dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu kwa kazi nzuri. Niseme tu kwamba, Mheshimiwa Waziri alipokuwa ametoka kwenye Wizara hii kwa kweli tulimkumbuka sana, amerudi mambo mengi yanakwenda vizuri kama yalivyokuwa wakati ule alipokuwepo, wakati ule wa mwanzo. Pia nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri, rafiki yangu Mheshimiwa Mollel kwa kazi nzuri na namna ambavyo anachapa kazi katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo katika kupongeza katika kuthibitisha mambo yanavyokwenda vizuri, napenda niseme katika Wilaya yetu ya Kilwa yenye Kata 23 tumepata fedha nyingi ndani ya kipindi cha mwaka mmoja na nusu uliopita. Jumla ya zaidi ya shilingi Bilioni 1.5 zimewekezwa kwenye miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa wodi maalum Sh.300,000,000 katika Hospitali ya Kilwa Kivinje ya Kinyonga. Pia tumepewa fedha Sh.500,000,000 kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya pale Mandawa na vile vile tumepewa fedha Sh.250,000,000 kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya pale Kipindimbi, Kata ya Njinjo na pia tumepewa zaidi ya Sh.400,000,000 kwa ajili ya umaliziaji wa Zahanati katika Vijiji nane vya Miumbu, Mtepela, Nakindu, Pungutini, Kisongo Namakongoro, Kiswele pamoja na Songomnara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali pia ilifanya kazi nzuri na wadau wa maendeleo wa PAN AFRICA na wametuwezesha kushirikiana nao na kujenga Vituo vitatu vya Afya, Chumo, Somanga pamoja na Songosongo na pia Zahanati moja imejengwa kwa kushirikiana na hao wadau wa PAN AFRICA pale katika Kijiji cha Nahama na Mayunu. Pamoja na mafanikio hayo, bado kumekuwa na changamoto zinaendelea. Changamoto ya kwanza ni kutokuwepo kwa ambulance, ambulances zetu nyingi zililetwa zaidi ya miaka 10 iliyopita katika Wilaya ya Kilwa na hivyo sasa hivi haziwezi kufanya kazi ya kuweza kubeba wagonjwa na kuwaharakisha kwenda hospitali.

Mheshimiwa Spika, naishukuru Serikali imekuja na mpango wa kuleta katika kila Halmashauri angalau ambulance moja, lakini sisi Kilwa tuna majimbo mawili kwa hiyo itapendeza kama Mheshimiwa Waziri atatuletea ambulance mbili, moja ikaenda Kilwa Kaskazini na nyingine ikaenda Kilwa Kusini. Vile vile tuna changamoto ya vifaa tiba, kutokana na ujenzi wa vituo vingi vya Afya na Zahanati vifaa tiba vimekuwa adimu au vichache. kwa hiyo, tungeomba Serikali itusaidie vifaatiba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna changamoto kubwa ya watalaam au watumishi katika Wilaya yetu ya Kilwa tunauhitaji wa watumishi 1,315 waliopo ni 357 tu. Kwa hiyo, tuna uhaba wa watumishi 958 sawa na asilimia 76 ya uhitaji. Kwa hiyo, ningeshauri Serikali kupitia zile ajira ambazo zimetangazwa hivi karibuni basi watupunguzie huu uhaba ili shughuli ziweze kwenda tiba iweze kutolewa kama ambavyo inatakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hospitali yetu ya Wilaya ya Kinyonga pale Kilwa Kivinje ni ya zamani sana imejengwa tangu wakati wa ukoloni wa Waingereza imechakaa sana inahitaji ukarabati mkubwa ningeomba Serikali itenge fedha kwa ajili ya ukarabati wa ile hospitali ya Wilaya ya Kilwa ya Kinyonga pale Kivinje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna shida katika baadhi ya vijiji vyetu kuna vijiji kama Tisa Jimbo langu peke yake bado havina zahanati. Kwa hiyo, wanalazimika wananchi kutembea umbali mrefu kwenda kusaka tiba katika zahanati za vijiji vya jirani au Vituo vya Afya ambavyo vipo mbali. Kuna kijiji cha Kinywanyu, Ingerito, Namayuni, Namakoro, Ngorongoro, Bugo, Nambondo na Naipuli havina zahanati, pia kati ya Kata 23 za Wilaya ya Kilwa tuna vituo vya afya Saba tu, Kata 16 hazina Vituo vya Afya. Kwa hiyo, ningeshauri Serikali itenge fedha za kutosha ili kupunguza uhaba wa Vituo vya Afya na Zahanati katika Wilaya yetu ya Kilwa ili wananchi waweze kupata huduma katika maeneo ya jirani huduma ambayo ipo bora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nasema naishukuru Wizara, narudia kusema naishukuru Wizara kwa kazi kubwa wanayoifanya, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuzungumza.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)