Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nichangie hoja iliyopo mezani. Nami nianze kwa kumpongeza dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu kwa kazi nzuri anayoifanya; pili, kwa Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Mollel kwa kazi nzuri ambayo anaifanya. Mawaziri hao kwa kweli ni wasikivu na ni miongoni mwa Mawaziri ambao wanapokea simu hadi saa 8:00 za usiku, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee nampongeza Katibu Mkuu wa Wizara hii, Mheshimiwa Prof. Makubi, Naibu Katibu Mkuu Dkt. Shekilage na Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Sichwale. Watendaji hawa wanafanya kazi vizuri na tunaona muda mwingi wanahangaika kutatua kero katika sekta yetu ya afya. Hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika mjadala wa leo, watu wengi wanachangia sana kwenye suala la dawa na utumishi kwa sababu ndiyo maeneo makuu ambayo yatasaidia kuboresha sekta yetu ya afya. Nami nitatumia muda huu kujikita kuhusu suala la upatikanaji wa dawa.

Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeze Waziri, kwenye kitabu chake ukurasa wa 44 amekuja na takwimu za uhalisia. Huko nyuma tulikuwa tunapewa takwimu ambazo siyo za uhalisia kwamba kuna upatikanaji wa dawa asilimia 90, au asilimia 80. Nampongeza Waziri na hata kwenye kamati yetu alikuja akasema takwimu nyingine za dawa siyo sahihi. Hapa katika ukurasa wa 44 ameonesha uhalisia kwamba kwenye MSD upatikanaji wa dawa ni asilimia 51, hakutaka kuficha. Nakupongeza sana Waziri, na unachokifanya Mwenyezi Mungu atakulipa. Badala ya kuwadanyanya Watanzania unaamua kusema ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa maagizo yake aliyotoa kuhusu MSD na kipekee nimpongeze Waziri Mkuu kwa kazi kubwa aliyoifanya MSD. Nakuomba dada yangu sasa Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Rais ameshatekeleza kwa upande wake, kuna kazi sasa ambazo Waziri, Katibu Mkuu na Mtendaji Mkuu lazima mzifanye. Mafanikio ya taasisi hayaletwi na management peke yake, kuna wafanyakazi wa kati na wafanyakazi wa chini. MSD ifumuliwe ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wafanyakazi wa kati wanaweza kumkwamisha CEO wa taasisi. Madereva wanaweza kumkwamisha mpaka CEO wa taasisi. MSD wanasambaza dawa, tukiwa na timu ya madereva ambao wanataka kufanya sabotage, wanaweza kumwambia Afisa Utumishi kwamba, mimi ni CEO wa nane hapa kwenye taasisi, hamnibabaishi, na akashindwa kupeleka dawa kwa wakati. Kwa hiyo, overhaul ya MSD isiwe kwa CEO na bodi tu, twende mpaka kwa madereva, watumishi wa kati na watumishi wengine ili MSD sasa tuipe muda iweze kutekeleza majukumu yake.

Mheshimiwa Spika, suala lingine, kuna upotevu wa dawa. Hili nalo lazima lidhibitiwe. Sehemu kubwa kuna mgongo ambao watu wanajificha kwamba kuna suala la msamaha. Hili nalo liangaliwe. Hii fedha ya dawa ambayo tunasema kwamba inaingia kwenye msamaha: Je, ni kweli zimeenda kwenye msamaha? Kwa sababu tulitarajia kwamba fedha tunazopeleka kwenye dawa iwe revolving fund, tunapeleka kila mwaka, na kule dawa hazitolewi bure, zinauzwa. Kwa hiyo, lazima zile fedha zizunguke. Otherwise kila mwaka tutakuwa tunapeleka fedha na matokeo hatuyaoni. Kwa hiyo, lazima tufuatilie zile fedha ambazo zinapatikana kwenye vituo vyetu vya kutolea huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni kuhusu bajeti ya MSD. Lazima hawa tuwaongeze fedha. Baada ya kufanya overhaul tuwaongeze fedha sasa. Pia tumefanya mabadiliko kuhusu Sheria ya MSD kwamba sasa wanaruhusiwa hata kujenga viwanda kutengeneza dawa. Wana mradi wao pale Keko na wana kiwanda chao pale Keko Pharmaceutical, tuwaongezee mtaji ili waweze kuzalisha dawa zenye ubora ili tuweze hata kuuza nchi majirani. Kwa hiyo, naomba tuwaongezee mtaji ili waweze kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala langu la pili ni kuhusu upungufu wa watumishi. Mheshimiwa Waziri amesema kinagaubaga kabisa katika ukurasa ule wa 75 kwamba watumishi waliopo kwenye sekta ya afya ni asilimia 47 ya mahitaji yao na asilimia 55 ni upungufu. Kwa hiyo, hapo utaona wazi kwamba lazima tuwe na jitihada za makusudi za kuajiri watumishi wa afya ili kupunguza hii nafasi iliyopo. Ndiyo maana kila Mbunge hapa akisimama anazungumzia upungufu wa watumishi wa sekta ya afya. Kwa hiyo, naomba kibali maalum kitolewe ili kupunguza changamoto hiyo. changamoto hii ni kubwa sana tunapokwenda kwenye maeneo ya vijijini. Kwa mfano kwenye Jimbo langu mimi la Nanyamba tuna upungufu wa asilimia 79. Mahitaji ya watumishi wa sekta ya afya ni 425, waliopo ni 106 tu. Kwa hiyo, utaona hapo tuna upungufu wa asilimia 79. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba tutoe kibali maalum, kwa sababu kuna vituo vingine vya afya kama Kiromba na Majengo, hakuna madaktari, ni wauguzi tu wanaendesha vile vituo. Sasa hii ina madhara makubwa sana. Tutoe kibali maalum, watumishi waajiriwe ili wakatoe huduma kule ambako tumeshafanya uwekezaji mkubwa kwa kujenga vituo vya afya, hospitali za Halmashauri na zahanati zetu.

Mheshimiwa Spika, nimalizie mchango wangu kuhusu suala la hospitali yetu ya Kanda ya Kusini Mtwara. Naipongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa kutoa fedha nyingi za kumalizia ujenzi kwa phase one hospitali yetu ya kanda ya Kusini inayojengwa pale Mikindani, Mtwara, tunawashukuru sana. Isipokuwa sasa hivi tuna changamoto ya watumishi kama nilivyosema hapo awali. Ilipofunguliwa ile hospitali ya kanda walitolewa watumishi kutoka katika maeneo mbalimbali wakapelekwa pale watumishi 42. Sasa hivi idara inayofanya kazi ni moja tu ya OPD. Naomba Mheshimiwa Ummy na timu yako muongeze idadi ya watumishi ili mtumishi akienda kwenye hospitali ya rufaa apate zile huduma za kibingwa ambazo anazitarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza naipongeza Serikali kwa kutenga fedha, Shilingi bilioni saba kwa ajili ya kununua, vifaa muhimu; CT-Scan na MRI. Naomba sasa vifaa hivyo msambazaji avilete kwa wakati ili tuweze kutoa huduma iliyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kuipongeza Wizara hii na ninaunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)