Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya uhai, lakini pia nimshukuru sana Mheshimiwa Rais mama Samia Suluhu Hassan kwa kweli anafanyakazi kubwa pamoja na wasaidizi wake wote. Nimshukuru pia Waziri wa Afya kwa wasilisho zuri ambalo amelifanya pamoja na wasaidizi wake wote. Uchumi wa nchi yetu ukuaji wake unakwenda sambamba na masuala ya afya kwa wananchi wake. Kwa hiyo, kama afya haitatiliwa mkazo maana yake hata zile juhudi ambazo tunazifanya za kukuza uchumi wa nchi yetu hazitaleta matunda ambayo tunayatarajia. Kwa hiyo, afya ni kitu muhimu tuwekeze tuisimamie ili tuweze kupata tija ile ambayo Taifa inalitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niende sasa kwenye changamoto. Changamoto ya kwanza kama ambavyo wametangulia kusema waliotangulia ni suala la uhaba wa watumishi katika kada za afya. Maeneo mengi hasa ya pembezoni watumishi wa kada hii ni wachache hali ambayo inaleta changamoto katika uletaji wa huduma zenye ufanisi katika maeneo hayo. Kwa mfano, ukienda kwenye Jimbo la Newala Vijijini tunao watumishi 119 tu ambao ni sawa na asilimia 19 ya mahitaji wa watumishi wa afya wanaohitajika katika Halmashauri ya Wilaya ya Newala Vijijini. Hii ni hatari kubwa kwa sababu kuna watu wanafanyakazi ambazo hawajasomea. Kutokana na uchache huo utamkuta Nesi anaandika dawa huyo huyo akachome sindano ni hatari, tunahatarisha usalama wa wananchi wa Jimbo la Newala na maeneo mengine ambayo yana shida kama za Newala Vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati mwingine inaleta uchonganishi kati ya wananchi na Serikali kwa sababu wananchi wanaohudumiwa wanaongea vibaya kwa sababu tu wanakosa huduma stahiki, lakini shida kubwa ipo kwenye uchache wa watumishi waliopo katika maeneo hayo. Nimuombe sana Mheshimiwa Waziri Ummy Mwalimu unafanya kazi kubwa sana kazi nzuri inaonekana umepata kibali cha kuajiri watumishi zaidi ya 10,000. Naomba sana angalia sana maeneo yale ambayo yana uhaba mkubwa wa watumishi ili na wao wakaweze kupata huduma kutokana na watumishi ambao watapelekwa katika maeneo yao ikiwemo pia na Newala Vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni uchache wa nyumba za watumishi wa kada ya afya. Sawa, watumishi wako wachache lakini hawana maeneo ya kuishi hawana nyumba za kuishi. Ugonjwa hauchagui muda wala dakika sasa kama mtumishi yuko mbali anapatikana mbali, anamuhudumiaje mwananchi ambaye amepata shida eneo X ambalo ni mbali kutoka pale anapoishi? Lakini hata hivyo hizo nyumba chache zilizopo kwa mfano ukienda kwenye Jimbo la Newala Vijijini, tuna mahitaji ya nyumba 184 lakini tuna upungufu wa nyumba 140. Zipo nyumba 44 katika hizo nyumba 44 ni nyumba nne tu ndizo ambazo zina nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nyumba ni chakavu hazistahili kwa kweli kuishi watumishi wale wakati mwingine wanakata tamaa, kwa namna ambavyo wanaishi yale maeneo ambayo wanatoka kwenda kuhudumia wananchi wetu. Nimuombe sana Waziri na timu yake tuangalie miundombinu ya nyumba kwa watumishi wetu wa Idara ya Afya ili na wao waishi sehemu nzuri na salama wapate moyo wa kwenda kutuhudumia, ili kupata ufanisi baadaye wa zile fedha ambazo Serikali imekuwa ikitenga fedha nyingi kupeleka huko lakini inakutana na watumishi waliokata tamaa ambao wanashindwa kutoa tiba vizuri kutokana na mazingira ambayo wanaishi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo hilo haliko Newala Vijijini peke yake liko pia Newala Mjini liko pia na maeneo mengine ya Mtwara. Suala lingine ni mahitaji ya vifaa tiba pamoja na vitenganishi katika Jimbo la Newala Vijijini tunazo zahanati tatu ambazo zimekamilika, tunayo zahanati ya Mpwapwa, tunayo zahanati ya Nakahako, tunayo zahanati ya Hengapano. Zahanati zile tunaishukuru Serikali imesaidia kukamilisha maboma zimekamilika, tunaomba sasa kupatiwa vifaa tiba ili zikaweze kutoa huduma kwa wananchi wetu. Pia tunayo majengo ya OPD na maabara katika Hospitali ya Wilaya nayo tunayaombea dawa pamoja na vifaa tiba, ili ikaweze kutoa huduma katika maeneo ambayo yanahitajika kutoa huduma hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninalo pia linalohusiana na MSD niombe sana MSD iwe na dawa wakati wote ili kuondoa mkanganyiko kwa sababu, zahanati pamoja na hospitali zinapoomba dawa basi ikute MSD ina dawa kiasi ambacho haitagharimu tena suala la kwenda kutafuta Alternative Way ya kupata hizo dawa. Kuchelewa kupatikana kwa dawa kunaigharimu sana maisha ya wananchi wetu kiasi kwamba wengine inawezekana tungeweza kuokoa maisha yao, lakini kwa sababu dawa hazipatikani vituoni kutokana na ukosefu wa dawa kwenye MSD inakuwa ni changamoto ambayo wananchi wengi wanakwenda kupata shida jambo ambalo lingeweza kutatuliwa kama MSD ingekuwa na dawa wakati wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kuomba katika Kituo chetu cha Mkwedu ambacho kipo katika Jimbo la Newala Vijijini, tunayo Ultrasound iko pale lakini haina mfanyakazi/mtaalam tulishaomba muda mrefu. Pia Makamu wa Rais alishatoa maagizo mtaalam apelekwe pale mpaka leo tunavyoongea mtaalam hajapelekwa kile kifaa kimekaa pale kama mapambo hakifanyi kazi, wakati uhitaji wa wananchi wa kutumia kifaa hicho ni mkubwa sana sasa inasababisha kero na inawezekana pia kikaenda kuharibika kwa sababu hakitumiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)