Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Awali ya yote nampenda kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametufanikisha kujadili mjadala huu muhimu sana kwa mustakabali wa maisha yetu kwani maji ni uhai na ni haki ya msingi kwa mwanadamu yeyote yule.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo ameweza kutuheshimisha Wizara ya Maji. Kwa mara ya kwanza tayari tumeweza kufikia asilimia 95 za kupata fedha za mwaka wa fedha tunaoelekea kumaliza, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, na tunasema hatutaacha kufanya kazi usiku na mchana kuhakikisha dhamira yake njema ya kumtua mama ndoo kichwani inakwenda kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipende kukushukuru wewe binafsi kwa namna ambavyo umeweza kutuongoza vyema na hata leo hii ndani ya Bunge lako tukufu bajeti hii imeweza kujadiliwa kwa mapana.

Mheshimiwa Spika, nipende kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa umoja wetu, mmeweza kutupongeza, tumepokea pongezi zote; mmeweza kutupa changamoto, yote tumeweza kuyapokea. Tunaahidi haya yote ambayo mmeweza kuyajadili kwa siku mbili ndani ya Bunge hili Tukufu ni deni kwetu.

Mheshimiwa Spika, mmetupongeza tumepokea kama deni. Kazi ambayo tumeweza kuifanya kwa mwaka mmoja ambao tunaelekea kuumaliza tunaahidi tutaongeza ushirikiano kwenu kuhakikisha majimbo yote tunayafikia na huduma ya maji inakwenda kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, michango ni mingi na tunashukuru sana kwa michango yote. Ninakwenda kuongea tu kwa uchache kwa sababu Mheshimiwa Waziri ataongea kwa marefu.

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kuongea kwenye Jimbo la Chemba; Mheshimiwa Monni ameongea mengi lakini nipende tu kusema kwamba Wizara inatambua changamoto zote ambazo Wilaya ya Chemba inaishi nazo.

Mheshimiwa Spika, lakini changamoto hizi kulingana na upendo wa Mheshimiwa Rais ambavyo ameweza kutupatia fedha za kutosha tutaendelea kuhakikisha changamoto iliyoko chemba tunakwenda kuifanyia kazi. Tayari tunakwenda kuchimba Bwawa la Farkwa ambalo maji yatakwenda mpaka Chemba, hiyo nayo itasaidia kwa sehemu kubwa sana kuwa na chanzo cha uhakika na mradi kuwa endelevu kwa sababu tunatamani mradi utakapokamilika basi mradi huo uwe na manufaa kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitaongelea pia kidogo kwa Mheshimiwa Dunstan Kitandula, Mbunge wa Mkinga. Naye pia tumepata hoja yake kuhusiana na matumizi ya Mto Zigi. Tumezingatia, tumepokea, na tutakwenda kuhakikisha tunatumia Mto Zigi ili uweze kupeleka maji Mkinga katika maeneo yale ambayo imeshindikana kupatikana mabwawa yakiwa yanakauka, sasa Mto Zigi utakwenda kuwa suluhu.

Mheshimiwa Spika, pia nitaongelea kidogo Mbeya Mjini; hili ni jimbo lako wewe. Umetuongoza hapa Wabunge wote tunafanikiwa, ni kwa sababu ya umahiri wako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pale Mbeya Mjini tunafahamu tatizo la maji suluhu yake ni Mto Kiwira. Tayari Mhandisi Mshauri ameshaleta andiko lake la awali sasa hivi tunamsubiria aweze kukamilisha andiko ambalo litatupatia gharama nzima ya mradi na tayari sisi kama Wizara tunaendelea kufanya shortlisting ya kupata wakandarasi ili tuweze kumpata mkandarasi sahihi ambaye ataweza kumudu mradi ule mkubwa, mradi ambao Mbeya Jiji unautegemea.

Mheshimiwa Spika, mradi ule hautakuwa kwa ajili ya Mbeya Jiji tu, ni mradi ambao maeneo ya pembezoni mwa Mbeya Vijijini pia yanakwenda kunufaika; maeneo ya Chunya tunarajia yaje yanufaike na mradi huu; maeneo ya Mbalizi yanakwenda kunufaika; maeneo ya Rungwe pia yatakwenda kunufaika. Ni mradi ambao una tija hivyo, kwa heshima kubwa sana tunaliyonayo juu yako tutakwenda kufanya hili na wananchi watakwenda kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa Mkoa wa Mbeya, nipende kumpongeza sana Mheshimiwa Suma Fyandomo, jana amechaniga kisomi sana, naamini sote tumesikia. Mradi wa Tukuyu Mjini nao pia tutakwenda kuuzingatia; ushauri tumeupokea na tutaufanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, lengo la kuona kwamba force account huenda inachelewesha mradi, tutazingatia kuona namna tutaweza kushirikiana labda ya wakandari ili kuona mradi ule unakamilika. Na maeneo yote ambayo uliyataja kwa Tukuyu Mjini pamoja na kule alikotokea Mheshimiwa Spika wetu, basi yatakwenda kupata maji. Na haya tunayaongea siyo kama siasa, ila tunasema tunakwenda kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunamshukuru Mungu katika hoja zote zilizotolewa zipo ndani ya uwezo wa Wizara na tunaweza kuongea haya yote kwa sababu Mheshimiwa Rais yupo tayari kuwa begabega na sisi. Tumejionea wenyewe kwa matendo, mliongoea hapa bajeti iliyopita lakini matendo na utekelezaji wa miradi sisi sote ni mashahidi. Hivyo, haya yote ambayo ninayaongea tutakwenda kuyafanyia kazi kadri Mungu atakavyotuongoza na namna ambavyo Mheshimiwa Rais ataendelea kutuwezesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nihamie Jimbo la Magu kwa kaka yangu, Mheshimiwa Boniventura Kiswaga. Jana ameongelea hapa kuhusu maji katika eneo lake. Sisi kama Wizara tumesema miradi ambayo inaendelea na utekelezaji ndani ya jimbo lake tutaisimamia kuhakikisha inakamilika; lengo ni kuona maji yanatoka bombani.

Mheshimiwa Spika, tunaposema mradi ukamilike tunahitaji kuona akina mama wanapata maji bombani yakiwa safi na salama na yakutosha na katika umbali rafiki. Tunahitaji kuona kwamba dhamira njema ya Mheshimiwa Rais inakwenda kuokoa ndoa za akina mama wengi.

Mheshimiwa Spika, akina mama wamekuwa wakiamka usiku wa manane na hii sasa tunaelekea ukingoni. Akina mama watapumzika nyumbani mpaka kunapambazuka, shughuli za nyumbani zitakamilika na maji yatakwenda kupatikana karibu na makazi ya wananchi. Na hili tutalitekeleza kuendana na mradi wake wa Butimba na miradi yote ambayo ipo ndani ya jimbo lake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia basi pia naomba niongelee kidogo kwenye Jimbo la Biharamulo, Mheshimiwa Engineer Ezra ameweza kutuelekeza hapa hitaji la matumizi ya maji ya Ziwa Victoria. Sisi kama Wizara tumesema Biharamulo inakwenda kupata maji kupitia Ziwa Victoria. Na hii tutaifanya, tutafika kuhakikisha tunaleta msukumo mkubwa ili maji yaweze kupatikana na ya kutosha.

Mheshimiwa Spika, kwa ufupi nipende tena kuwashukuru Wabunge wote. Wabunge tunaomba mtusaidie kupitisha hii bajeti, lengo ni kwamba tuweze kukutana site, Sisi ombi letu kwenu ni kupitisha bajeti tuje tusimamie miradi, kama ambavyo tumefanya tuna uhakika tutafanya zaidi na zaidi kwa msaada wa Mwenyezi Mungu. Ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)