Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai na uzima lakini pia nitumie fursa hii kumpongeza na kumshukuru Mheshimiwa Waziri wa Maji na Naibu wake, ndugu zangu Aweso na Injinia Maryprisca kwa kazi nzuri sana mnayoifanya kwenye Wizara ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi watu wa Sumve tulikuwa tunahangaika kwa muda mrefu, na tulikuwa tuna kilio chetu, kwamba katika Mkoa wa Mwanza na Majimbo yake tisa, Jimbo la Sumve ndilo lilikuwa Jimbo pekee halina maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria; na kimekuwa ni kilio chetu humu. Tulikuwa kila mara tunajiuliza, hivi tatizo letu sisi ni nini? Hawa wenzetu kwa nini wanayo sisi hatuna mpaka yanataka kuletwa Dodoma? Kumbe tulikuwa hatufahamu siri ya urembo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siri ya urembo ni Mama Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Rais Samia Suluhu Hassan ndiye amekuja kutuletea maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria kwenye Jimbo la Sumve. Nafikiri ingekuwa tunaruhusiwa kujenga sanamu, alitakiwa ajengewe sanamu na watu wa Sumve. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa jambo hili lililofanyika ambalo nimeliona kwenye bajeti hii, kwa sababu tumeshajua siri ya kupata maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria. Tumeshajua siri ya maendeleo ya uhakika sisi watu wa vijijini, naamini wenzangu kule vijijini ikifika muda wanahitaji kuchagua, hawataacha kumchagua Rais Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Aweso mimi nimekuwa nikilalamika na Wizara ya Maji kuhusu vijiji vya Sumve kupata maji ya Ziwa Victoria lakini leo nikiangalia kwenye bajeti ninaona kwamba kuna maji yanatoka Hungumalwa yanapitia Mwankulwe yanaenda mpaka Malampaka kwenye Jimbo la Mheshimiwa Mashimba Ndaki, halafu kutoka Malampaka yanakuja Malya yanaenda kwenye vijiji vyote vya Kata ya Malya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watu wa Talaga, Mwitambu, Kitunga, Mwamembo na watu wa Kijiji cha Kiminza kwenye Kata ya Lyomo wanapata haya maji. Mheshimiwa Waziri nakushukuru sana na tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye Jimbo la Sumve maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria hayaishii hapo yanatokea Ukiliguru yanakuja kupita kwenye Kijiji maarufu cha Kolomije yanaenda kwenye Kijiji cha Mantale yanaenda kwenye Kijiji cha Ishingisha yanaenda kwenye Kijiji cha Sumve yanaenda kwenye Kijiji cha Bungulwa na Kijiji cha Isunga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili jambo kwa watu wa Sumve huu ni muujiza waliousubiri tangu dunia iumbwe. Kwa hiyo, nashukuru sana Serikali ya CCM kwa kazi kubwa walioifanya. Mheshimiwa Waziri amefikia kiwango akawaambia watu wa RUWASA wabadili design ili Jimbo la Sumve lipate maji. Walikuwa wanapeleka bomba lenye nchi nane lakini baada ya sisi kusema humu amewaambia wabadili design na tenda imecheleweshwa kutangazwa ili waweke bomba la nchi kumi na wiki ijayo Mheshimiwa Waziri wamesema wanatangaza hiyo tenda ili watu wa Sumve tupate maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria. Hii kwetu ni neema na ni jambo la kujivunia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Lakini Mheshimiwa Waziri sisi watu wa Sumve bado tunakushukuru. Upo mpango pia wa kupeleka maji ya Ziwa Victoria kutokea Nyamilama kwenda kwenye Kata ya Lyoma kwenye vijiji vya kina Mweli, Kunguru, Lyoma na Busule. Hili ni jambo la heshima sana kwa wananchi wa Sumve. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiacha haya mambo, Jimbo la Sumve lina kata 15. Hizi kata tunazozizungumzia ni kata tano. Kata 10 ili zipate maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria inabidi yatokee Magu. Naomba Wizara isiusahau mradi wa maji ya bomba kutoka Ziwa Victoria kuja kwenye kata 10 zilizobaki za Jimbo la Sumve kutokea Magu.

Mheshimiwa Spika, mbali na kuwakumbusha hilo bado tunashukuru. Mimi kwa kweli leo Mheshimiwa Waziri utanisamehe, itabidi leo niwe chawa, yaani nishukuru tuu kwa kiwango kikubwa kwa sababu umefanya kazi ambayo nilikuwa ninaililia kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna miradi kwenye karibu kila kata ya Jimbo la Sumve. Kuna mradi unaendelea kwenye Kijiji cha Ibindo Shilingi Milioni zaidi ya 500. Kuna mradi unaendelea kwenye Kijiji cha Mulya, kuna mradi umeshatangazwa tenda kwenye Kijiji cha Lyoma, kwenye Kijiji cha Wala, Kijiji cha Nkalalo, Kijiji cha Ligembe, Kijiji cha Mulula na Kijiji cha Ng’undya; vyote hivi vinaenda kutengenezewa mradi wa uhakika wa maji ya bomba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri watu wa Sumve umetupa heshima kubwa. Wewe ni Waziri pekee ambaye umekuja tumeanza kunywa na sisi maji ya kutoka Ziwani. Tunategemea tutaanza kuyanywa maana yake zamani ilikuwa ukitaka kuyanywa inabidi ubebe ndoo uende Mwaloni. Sasa hivi tutakuwa tunafungua kwenye mabomba yanatoka.

Mheshimiwa Spika, kitu ambacho nataka kukuomba Mheshimiwa Waziri. Uhakikisho wa hii miradi kufanyika na kusimamiwa vizuri. Tumekuwa tuna shida sana kwenye miradi ya maji. Sisi Sumve kuna mradi unaitwa Waisunga - kadashi na mwabalatulu. Mheshimiwa Naibu Waziri aliwahi kuja mwanzoni kabisa. Siku ile unakuja Mheshimiwa Naibu Waziri walifungua maji yakatoka, ulipoondoka wakafunga. Wakasema watamalizia kuweka mabomba kule Isunga ili yaanze kutoka, hawajamalizia Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwa hiyo, bado kunashida. Kuna watu baadhi hawako serious.

Mheshimiwa Spika, Kuna mradi wa Mwabilanda maji yanatoka kwa msimu. Kuna Kamati za Usimamizi wa Maji wanaiba pesa kama hawana akili nzuri. Inafika wakati wanashindwa hata kulipia bili za umeme. Kwa hiyo, iko miradi chechefu ambayo mnatakiwa mtusaidie. Hata hii miradi inayokuja bila kuwa na usimamizi wa uhakika inaweza isiwe na tija.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri najua wewe ni mchapakazi, Jimbo la Sumve sisi tunataka tukuone tu, tukushukuru lakini tukuoneshe pia ambapo panavuja. Kwa hiyo, nikuombe sana ukipata nafasi uje Sumve tukushukuru, tukuoneshe panapovuja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja.