Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na mimi kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu, hoja ya Wizara ya Maji, Wizara yenye umuhimu mkubwa sana katika maisha ya watanzania. Nitumie nafasi hii kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu kwa kazi kubwa ya kutoa fedha kwenda katika wizara hii ili kuweza kumtua ndoo mwanamama lakini kuhakikisha kwamba maji ni uhai yanatekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nitumie nafasi hii kumpongeza ndugu yangu Aweso msaidizi wake mama yangu Christina, Engineer Sanga Mtendaji Mkuu wa Wizara lakini kubwa zaidi Meneja wa RUWASA Mkoa wa Morogoro na Mhandisi Meneja wa Wilaya, Wilaya ya Morogoro Vijijini kwa kazi kubwa wanayoifanya katika Wizara hii katika kukamilisha kiu ya Watanzania katika kupata maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, ni mtu ambaye hana akili au asiyeona, lakini kwa yoyote anayeona kazi kubwa ya mapinduzi katika sekta ya maji ndani ya kipindi kifupi anakila sababu ya kujua kwamba kuna mambo mazuri yanafanyika. Nitumie nafasi hii cha kwanza mfano kwenye jimbo langu la Morogoro Kusini kuna mradi wa Bwakila juu tumepata milioni 680, kuna mradi wa Lundi tumepata milioni 492, kuna mradi wa Mvuha huu ni mradi kupitia UVIKO tumepata milioni 680, ukijumlisha kuna bilioni 1.772. Kwakweli tunakila sababu ya kuipongeza Serikali na kuipongeza Wizara kwa kuhakikisha kwamba haya mambo ambayo Serikali inataka yanafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vile vile kwenye jimbo langu kuna ukarabati wa mradi wa Singisa tumepata milioni 60 ahsante sana Mheshimiwa Waziri, lakini mradi wa Matombo
- Lugeni tumepata milioni 100 kwaajili ya kukarabati, tunakila sababu ya kupongeza.

Mheshimiwa Spika, lakini kubwa zaidi nimpongeze waziri kupitia mradi wa Bonde tumejengewa mabirika 10 na vizimba zaidi ya 20 kwa ajili ya kunyweshea maji mifugo lakini vile vile wale wananchi wa jamii ya wafugaji kupata maji safi na salama tuna kila sababu ya kupongeza. Tumechimbiwa visima viwili virefu Kata ya Milengwelegwe na Mngari tunakila sababu ya kupongeza, mimi kama mbunge wao napongeza kwa kazi kubwa nakupongeza ahsante sana mdogo wangu Aweso kwa kazi kubwa ambayo unaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu pamoja na pongezi bado tunachangamoto za maji. Katika Kata ya Selembala, kuna Vijiji vya Kiganyira, Magogoni, Mji Mpya na Bwira Juu. Huko ndiko kwenye Bwawa la Kidunda tunapokwenda kujenga. Tumewatoa wananchi kwenye maeneo ambao walikuwa na maji yao sasa hivi wanakwenda mtoni kuchota maji wanakumbana na adha ya kukamatwa na mamba. Ninakuomba tupatiwe visima. Lakini vile vile Kata ya Bwakila chini kuna Vijiji vya Dakawa, Sesenga, Vigolegole, Kichangani Kata ya Kisaki na Nyalutanga tunaomba mtusaidie visima vya maji ili wananchi wetu wapate maji safi na salama na sisi tufikie azma ya Serikali ya kupata maji safi na salama tutakapofikia mwaka 2025 kama vile Serikali inavyosema.

Mheshimiwa Spika, nimuombe Waziri wa Maji; kuna vijiji vya Mtombozi, Lugeni, Kisemu, Gozo Kibangile na Mtamba kuna matatizo makubwa ya maji. Idara ya Maji kupitia RUWASA na mkoa tayari walishafanya upembuzi yakinifu. Kuna mto unaitwa Kibana una uwezo wa kusababisha vijiji vyote hivi vikapata maji safi na salama. Tayari walishaandika proposal na ipo kwenye Ofisi ya Mkoa inahitaji kama bilioni tatu tu. Nikuombe Waziri angalia kwa namna moja au nyingine unaweza kutusaidia vipi tuondokane na adha hii ya maji. Mimi naamini kabisa miradi hii ikikamilika wananchi wetu watapata maji safi na salama, lakini kubwa zaidi wataweza kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vile vile nikuombe Mheshimiwa Waziri umetusaidia katika kupitia mradi wa UVIKO mradi wa mvua ambao ndiyo Makao Makuu ya Wilaya yetu ya Morogoro Vijijini, pale tayari kuna mradi ambao unatakiwa ufanyike lakini kama mkiweza kutuongezea fedha kiasi kama cha milioni 200 mradi ule kwa kujenga tank kubwa, ambapo lililokuwa designed ni dogo, utaweza kufanikisha maji kufika katika Kijiji cha Sangasanga, Tulo, Lukulunge na hapo tutaenda kuwasaidia wananchi wetu kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze mdogo wangu Aweso na Wizara kwa safari hii kuhakikisha kwamba tunakwenda kujenga Bwawa la Kidunda. Ni uhalisia suluhisho la upatikanaji wa maji wa Jiji la Dar es salaam, Pwani na hata baadhi ya maeneo katika Mkoa wa Morogoro ni kujenga Bwawa la Kidunda. Bwawa la Kidunda lipo katika Jimbo la Morogoro Kusini katika Kata ya Selembali.

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa Serikali, tunakwenda kujenga mradi mkubwa ambao unatakiwa ulete matokeo chanya; sijui Serikali tumejipangaje katika uhifadhi wa mazingira ili kuruhusu vyanzo vya mito ambayo inajaza maji katika Mto Mvua iendelee kuwa endelevu.

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwako Mheshimiwa Waziri katika hatua za muda mfupi na katika mabonde walivyoonyesha katika jitihada za kutengeneza mabirika ili mifugo isiende mtoni tungeweza kusaidia mkachimba mabwawa ng’ombe wakaenda kupata hifadhi ya maji kwenye mabwawa badala ya kwenda mtoni kuharibu kingo za mto, lakini wakati wa kiangazi wakapanda juu kwenda kwenye vyanzo vya mito ambavyo wataenda kuharibu mazingira. Matokeo yake, nataka tu kuthibitisha, kama hatukuangalia hili hata huu mradi tutakuwa tumepoteza fedha bure ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimuombe tu Mheshimiwa Waziri, nimetoa angalizo kwa sababu ya uzoefu wangu kama Mbunge katika eneo lile. Na ushuhuda wewe mwenyewe unajua; mwaka huu huu Dar es Salaam walikosa maji. Lakini walikosa maji si kwa sababu Mto Ruvu ulikauka, hapana, ni kwa sababu vyanzo vya mito mitano ya Ngazi, Mto Mvua, Mto Dutumi, Mto Mgekakafa ilivamiwa na wafugaji juu kwa ajili ya kuokoa mifugo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo Mheshimiwa Waziri nikuombe tu, katika huu mradi wa mabirika 10 karibu tunamaliza, ambao umejengwa na bonde, nikuombe wewe nawe ukipata muda twende tukazindue wote kwa pamoja ili kazi iendelee kuwa nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini mwisho zaidi kabisa nikushukuru kwa kazi kubwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)