Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, nishukuru sana kupata nafasi ya kuchangia. Nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwakutoa fedha ambazo zimetekeleza miradi mingi ya maendeleo ndani ya wilaya yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri. Mheshimiwa Waziri ni miongoni mwa Mawaziri ambao ni wasikivu wanasikiliza Wabunge na wasikiliza wananchi kwa ujumla. Kazi anayoifanya pamoja na wasaidizi wake ni mfano mzuri wa kuigwa kwani anawatendea haki Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nimuombe sana Mheshimiwa Waziri; Mkoa wa Katavi, Mkoa wa Kigoma, Mkoa wa Rukwa wote tuna kilio cha aina moja. Sisi tuna chanzo cha uhakika cha maji cha Ziwa Tanganyika, ziwa ambalo linakina kirefu na ziwa ambalo lina maji safi ambayo ni mengi na yanaweza kutumika kwa mikoa yote na mpaka kutoa ziada kwenye maeneo mengine. Tunachoomba ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kile chanzo kianze kupeleka maji kwenye mikoa hiyo mitatu ikiwemo Mkoa wa Katavi ambao mimi ni sehemu ya jimbo na Mheshimiwa Waziri alishafika mpaka kwenye eneo ambako chanjo kinachopendekezwa kutoa maji kuyatoa eneo la Karema kuyapeleka Makao Makuu ya Mkoa pale Katavi, Mpanda Mjini inaweza ikasaidia sana kupeleka huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi bila kupata chanzo cha maji cha kutoka Ziwa Tanganyika tutaendelea kupata miradi midogo midogo ambayo haitasaidia sana. Pamoja na jitihada zinazofanywa na Serikali kutupatia fedha kwaajili ya miradi midogo midogo lakini mwarubaini wa suluhisho la maji kwenye Mkoa wa Katavi ni kuyatoa maji Ziwa Tanganyika na kupeleka eneo la Makao Makuu ya Mkoa Mpanda Mjini. Niombe sana Mheshimiwa Waziri ninachokizungumza wewe mwenyewe ni shuhuda na unajua, na nikupongeze sana. Umefika kwenye eneo la chanzo cha maji na umetoa ushirikiano mkubwa sana kwa watendaji na niwapongeze Watendaji wa Mkoa kwa ujumla wa Katavi na meneja wa MRUASA wa Wilaya ya Tanganyika kwa ubunifu ambao na wewe mwenyewe ulishuhudia mpaka ukafika ukaona umuhimu wa yule meneja ukatoa fedha za kwako kumpa kama zawadi ambayo ni motisha kwa ufanyaji kazi mzuri.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni wakandarasi ambao wanateuliwa na Serikali kwaajili ya kujenga ile miradi ya maendeleo. Tunaye mkandarasi ambaye alipewa kazi ya kujenga Mradi wa Katuma mkandarasi huyu Hema-Tec anamuda mrefu toka amesaini mkataba ambao ulitakiwa kuwa amekamilisha huu mradi ifikapo tarehe 21 mwezi wa sita. Wenzie ambao walisaini pamoja huu mkataba walishatekeleza miradi yao na imekamilika na maji yameanza kutoka; lakini huyu tangu aliposaini huo mkataba hata kwenda kwenye site hajafika na alishasaini huo mkataba.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba sana Mheshimiwa Waziri aingilie kati mkataba wa Hema-Tec usimamishwe ili tutafute mkandarasi ambaye anauwezo anayeweza kwenda kufanyakazi kuliko kuwarundikia kazi ambao hawana uwezo wa kufanya kazi. Eneo hili ni muhimu na naamini si Mpanda tu peke yake au Katavi kwa ujumla; wapo wakandarasi wabovu ambao wanapewa miradi ya Serikali wanashindwa kuitekeleza kwa wakati. Niombe muwapime na muangalie vigezo ambavyo mnapowapa kazi wahakikishe wanaenda kutekeleza kazi ambayo inaweze ikawasaidia wanananchi kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lipo eneo lingine ambalo Serikali ilifanya kwa nia njema tulipoanzisha jumuiya za watumia maji. Jumuiya hizi zinafanya kazi nzuri, lakini kwa bahati mbaya sana kuna waraka ulitoka wa Serikali uliokuwa unataka kila jumuiya za watumia maji wawe angalau wana elimu ya kuanzia kidato cha nne, na huko nyuma Serikali iliwapa elimu ya mwanzo waliokuwa wanasimamia ile miradi huko nyuma, ambao walikuwa ni vijana wazalendo wa kutoka kwenye maeneo husika ya miradi husika. Kwa bahati mbaya sana tangu mlipotoa ule waraka mkaleta vijana wengine wapya ukweli usimamizi umekuwa si mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niombe muwarejeshe wale ambao mliwapa elimu, mliwasaidia mkawapa elimu na wakajitolea wamefanya kazi na ilikuwa na ufanisi. Na ukichunguza waliokuwa huko nyuma walisimamia miradi vizuri na mapato ya jumuiya za maji yalikuwa yakijiendesha vizuri. Sasa hivi mmeongeza gharama kwa kuwajaza hao vijana ambao ukweli miradi mingi imeshindwa kufanya kazi ile iliyokusudiwa ni eneo hilo ambalo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa sekunde 30 malizia.

MHE. MOSHI S. KAKOSO: ...ni eneo hilo ambalo tunashukuru, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri, ahsante. (Makofi)