Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya maji.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Jumaa Aweso pamoja na Naibu wake, Katibu Mkuu kwa namna ambavyo wanachapa kazi ya kumsaidia Mheshimiwa Rais katika kutekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa kuhakikisha kwamba huduma ya maji inawafikia Watanzania. Tunawapongeza sana na Mungu aendelee kuwabariki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Waziri kwa kuwasilisha bajeti yake ya utekelezaji ya mwaka 2022/2023, bajeti ambayo inakwenda kupunguza changamoto kubwa ya maji katika nchi yetu ya Tanzania na kuhakikisha kwamba maji salama yanaendelea kupatikana.

Mheshimiwa Spika, nimebahatika kupita katika maeneo mbalimbali nchini Tanzania katika shughuli za Kamati ya PIC. Nimekwenda katika Majiji ya Mwanza, Arusha, Dar es Saalaam na kuangalia miundombinu ya maji na shughuli mbalimbali za usambazaji wa maji na huduma za maji kwa wananchi; maji safi pamoja na maji taka; tumeona shughuli kubwa ambayo Serikali inafanya na tunawapongeza sana katika Mkoa wa Dar es Salaam, Arusha na Mwanza kwa namna ambavyo wanasimamia utekelezaji katika kuwahudumia wananchi kupata maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, ningependa kule kwetu Lindi kukawa na mabadiliko makubwa kama yaliyopo Dar es Salaam. Kuna siku nimeshawahi kukueleza Mheshimiwa Waziri Jumaa Aweso kwamba ningeomba Eng. Juma Meneja wetu wa Lindi aje kuja Dar es Salaam na timu yake kuja kujifunza namna ambavyo wanatoa huduma ya maji safi na maji taka ili kuhakikisha kwamba wananchi wa lindi wanaunganishiwa maji na kila mwananchi anapata huduma hiyo ya maji na kuweza kuchangia Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niishukuru Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu. Katika Mji wetu wa Lindi tumepata fedha nyingi tangu mwaka 2021/2022 na utekelezaji wa miradi mingi unaendelea, miradi mingine imekamilika. Kwa mfano kama pale Ng’apa, Teleweni, Tandangongoro mradi wa Shilingi bilioni 2.8 umekamilika, na wananchi wanapata maji safi na salama. Pale Mingoyo pia tuna mradi wa tenki lenye ujazo wa lita 100,000 umekamilika na wananchi wanaendelea kupata huduma ya maji. Fedha za COVID 19 kwa ajili Mradi wa ujenzi wa tenki la ujazo wa lita 100,000 pale Kiduni zimetolewa na mradi unaendelea kujengwa; na hatimaye muda si mrefu utakamilika na wananchi wataendelea kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunao mradi mkubwa sana pale Mitwero uliogharimu shilingi bilioni 3.5 ambao umekamilika kwa asilimia 80. Bado mradi ule unaendelea kusambaza mabomba kutoka Mitwero kwenda Mbanja na Jimbo la Mchinga ambako mama yangu amezungumzia hapa. Kwa hiyo ninaamini mradi utakapokamilika utakuwa umetoa huduma nzuri katika majimbo haya mawili na wananchi wataendelea kupata maji safi na salama.

Kwa hiyo ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu kwa kazi hii na upendo mkubwa wa wananchi wake wa kuhakikisha kwamba wataendelea kupata huduma ya maji safi na maji salama kuhakikisha kwamba tunaendelea kuwalinda wananchi wetu ili waendelee kuwa na afya nzuri na kupunguza gharama kubwa ya matibabu inayosababishwa na wananchi kunywa maji ambayo si salama. Kwa hiyo pamoja na mambo hayo mazuri ambayo yamefanywa katika jimbo la Lindi mjini bado tunazo changamoto mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba kila mwananchi anavuta maji nyumbani kwake. Kwa sasa tunayo changamoto mabomba yale makubwa ambayo wananchi wanataka kuvuta maji, lakini mabomba yamepita umbali mrefu na hivyo wananchi wanashindwa kuunganisha kwasababu gharama ni kubwa. Yawezekana mwananchi mwingine akaambiwa kutoka kwenye bomba kubwa mpaka nyumbani kwake analazimika kununua mita 300 au mita 400; sasa gharama ya kuvuta maji mpaka nyumbani kwake inakuwa kubwa. Kwa hiyo wananchi wengi wanashindwa kumudu kuhakikisha kwamba wanavuta maji nyumbani kwao.

Mheshimiwa Spika, na suala hili tulishalizungumza na Mheshimiwa Waziri na nilishakueleza na ulisema kwamba miradi ikishakamilika basi utatuongezea mtandao wa maji kuhakikisha kwamba wananchi wa Lindi wanaendelea kupata unafuu wa kuvuta maji nyumbani kwao.

Mheshimiwa Spika, tunayo maombi mapya katika maeneo mbalimbali kuhakikisha kwamba mtandao wa maji unaendelea. Tuna eneo la Kitumbikwela upande wa pili wa Bahari. Tumeomba fedha Bilioni 1.95 ili kuwezesha kuweka mtandao huu kupitia Kijiji cha Mkundi, Mnengule, Iyato, Mtalala, Mwitingi Mwamoja na Nachingwea; tuhakikishe kwamba fedha hizi Mheshimiwa Waziri unatupatia ili kuhakikisha mtandao huu unakwenda kutekelezwa na wananchi wa upande wa pili wa bahari waweze kupata maji safi na salama. Tunajua kwamba maji yapo lakini bado hayajasambazwa kwenye mabomba katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tuna mradi mwingine wa usambazaji wa mabomba katika maeneo ya Mlandege, Muhimbili, Kipuri, Mmongo pamoja na Mnazi Mmoja; nayo tumeomba Bilioni 1.44. kwa hiyo Mheshimiwa Waziri tunategemea bajeti yetu itakapopita basi haraka uweze kutupatia fedha kwa ajili ya kwenda kuitekeleza hii miradi mipya kuhakikisha kwamba tunaweka wigo mpaka wa wananchi kufunga maji na kuweza kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tuna mradi mpya wa Angaza Sekondari ambao utagharimu Shilingi milioni 740, nayo ni maombi mapya kwako Mheshimiwa Waziri. Tunajua ya kwamba una kiu kubwa kuona kwamba Lindi kunakuwa na mabadiliko makubwa na mapinduzi makubwa ya kuhakikisha kwamba wananchi wa Lindi wanapata maji na sisi tuweze kuchangia mapato ya ndani katika Wizara hii ya Maji. Kwa hiyo bado yapo maeneo ambayo hayapo kwenye mpango. Tuna Kijiji cha Ruaha Mtaa wa Ruaha tuna kaya takriban 400 wanakosa maji safi na salama. Tunaiomba Serikali kuhakikisha kwamba wana Ruaha japo kwa kuwachimbia kisima.

Mheshimiwa Spika, lakini tuna eneo la Madingula…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde 30 Mheshimiwa Hamida, malizia.

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: … lakini bado tuna mtaa wa Mitonga kule Kata ya Mbanja ni mbali kutoka barabara kubwa, nao wanakosa maji. Tuhakikishe kwamba wananchi hawa tunawachimbia visima kwa haraka ili kunusuru maisha yao kwasababu wanatafuta maji umbali mrefu zaidi ya kilometa tatu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninaiomba sana Serikali kuhakikisha kwamba wanatusaidia ili wananchi wa maeneo hayo waweze kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini baada ya hayo yote niendelee kumpongeza Jumaa Aweso kwa unyenyekevu mkubwa…

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana naomba kuunga mkono hoja ahsante sana.