Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan - Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango - Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa - Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Waziri, Naibu Waziri na viongozi wote wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha miezi kumi ya mwaka wa 2021/2022, Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imesimamia kwa uadilifu na ufanisi mkubwa masuala yote ya elimu hasa kuboresha ufaulu na hata miundombinu ya madarasa na mabweni. Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya imekuwa inapitia kipindi kigumu cha changamoto za kuporomoka kutoka kuongoza kimkoa katika ufaulu wa elimu ya sekondari. Pia ufaulu kwa shule za msingi unapitia katika changamoto kubwa hasa kutokana na mazingira ya shule za vijijini ikiwemo upungufu wa walimu. Pamoja kuwa ni jukumu jumuishi kwa wazazi, bado kunahitaji uharaka wa kupitia sera ya elimu kuweza kuboresha taaluma kwa shule za vijijini ambazo kwa kiasi kikubwa hazifanyi vizuri ukilinganisha na shule za mijini.

Mheshimiwa Spika, walimu bado wanaendelea kufanya kazi katika mazingira magumu kwa kukosa majengo ya nyumba za kuishi. Napendekeza Serikali kuendelea kushirikiana na wananchi katika ujenzi wa nyumba za walimu iende sambamba na ujenzi wa maboma na pia madawati kwa wanafunzi wote. Ni muhimu kuhakikisha motisha kwa walimu ili kuboresha taaluma iwe ya kiushindani kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki, SADC na hata Afrika. Napendekeza pia Serikali itoe kipaumbele kwa kulipa madai ya malimbikizo kwa walimu ili kupunguza muda wa kufuatilia malipo yao na badala yake waelekeze muda zaidi kwenye kufundisha.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki tunapopambana na magonjwa yasiyo ya kuambukizwa yakiwemo magonjwa ya kansa, shinikizo la damu, figo, moyo na kadhalika, narudia tena kuishauri Serikali kuweka kipaumbele cha kuboresha elimu ya afya, ikiwemo upanuzi wa ujenzi wa ndaki ya sayansi ya afya ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam - Mbeya College of Health and Allied Sciences (UDSM-MCHAS). Serikali itoe kipaumble cha kutenga eneo la kutosha kwa chuo hiki kutoka kwa eneo la iliyokuwa Tanganyika Packers Ltd., Mbalizi Mbeya.

Mheshimiwa Spika, katika kuwezesha uwekezaji na uendelezwaji wa viwanda endelevu, Tanzania inahitaji kuzalisha watalaam wengi na hasa ujasiriamali na taalum ya ufundi ngazi za kati na chini ambapo mahitaji ni makubwa. Pamoja na kujiwekea malengo ya kuongeza viwanda, naishauri Serikali ilitazame upya suala la uwepo wa nguvu kazi (vijana kupata mafunzo ya ufundi na ujasiriamali) ya kutosha na itakayowezesha kufikia malengo yaliyokusudiwa. Kutokana na mabadiliko mbalimbali hasa ya kisayansi na kiteknolojia na hata kiuchumi, yanayoendelea duniani, kuna haja ya sera na mitaala ya elimu kuwa ya kisasa zaidi ili kuendana na mabadiliko hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa miaka kadhaa iliyopita Tanzania imeshuhudia mafundi mchundo wengi wakiongeza (upgrade) ngazi za utaalamu wao kwa kusomea kozi za uhandisi wakati idadi ya mafundi mchundo wanaofuzu masomo ya ufundi mchundo ikipungua huku mafundi wa kawaida (artisans) wanaoongeza utaalamu wao ikiwa haiongezeki. Hali hii imepelekea kupungua kwa kasi idadi ya mafundi mchundo pamoja na mafundi wa kawaida na hivyo kuathiri utendaji wa viwanda (na sekta nyingine) kwa kuwa hawa ndio wanaotenda kazi kwa mikono. Ukizingatia kuongezeka kwa uwekezaji katika viwanda, hali hii inabidi irekebishwe haraka kwa kuongeza idadi ya mafundi husika ili kukidhi mahitaji ya uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa uwiano wahandisi/ mafundi mchundo/mafundi wa kawaida ni wa chini sana na hautaweza kuisiadia Tanzania kufikia malengo tarajiwa. Hata ukilinganisha wataalamu wa juu wa stadi mbalimbali za taifa na wenye stadi za kati na za chini uwiano wake sio mzuri ukilenga uwezo wa kusimamia viwanda vya kisasa kiasi cha kuhitaji marekebisho ya uwiano kama mpango wa Taifa wa kuendeleza stadi unavyotegemea (National Skills Development Strategy).

Mheshimiwa Spika, napendekeza Serikali iongeze msukumo kwenye mafunzo ya mafundi mchundo na mafundi wa kawaida na pia elimu yetu ilenge mafunzo ya ujasiriamali. Hii pia ishirikishe elimu ya kujitegemea toka elimu ya awali na hata kutumia watalaam wetu wa kilimo, mifugo na uvuvi kuanzisha mashamba darasa mashuleni.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.