Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda na Naibu wake Mheshimiwa Omary Kipanga pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara Profesa Eliamani Sedoyeka na Naibu Makatibu Wakuu Profesa James Mdoe na Profesa Carolyne Nombo na watendaji wengine wa Serikali katika Wizara hii kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utajikita kwenye umuhimu wa Serikali kupitia upya sheria inayowafanya maprofesa kustaafu wakiwa na miaka 65 na kutokupata mikataba maalumu ya kuendelea kufundisha na pili, changamoto za utoaji wa mikopo kwa wanafunzi waliosoma shule binafsi wanaojiunga na vyuo vikuu Tanzania.

Mheshimiwa Spika, katika vyuo vyetu vikuu vya Serikali, kuna changamoto kubwa ya tatizo la rasilimali watu likiwa limesababishwa kwa kiasi kikubwa na kitendo cha Serikali kubadilisha utaratibu wa maprofesa kuendelea kufundisha kwa mikataba maalumu hadi wanapofikisha umri wa miaka 70.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, kwa miaka michache iliyopita, zaidi ya maprofesa 91 waliondoka katika Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine. Kati ya Januari 2016 na Desemba, 2020 maprofesa 111 waliondoka kwenye utumishi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam; katika Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela hakuna profesa hata mmoja wa somo la Hisabati tangu aliyekuwepo alipoondoka, hapajakuwepo na mrithi wa kusaidia kusimamia research za mahesabu katika ngazi ya uzamivu. Hata kwenye soko la ajira si rahisi kuwapata wataalamu wenye vipaji hivi na vyuo vyote vya Serikali nchini vinakabiliana na changamoto kama hii.

Mheshimiwa Spika, changamoto ya rasilimali watu vyuo vikuu Tanzania inasababishwa pia na masharti magumu ya kuajiri wataalamu kutoka nje ya Tanzania. Kuajiri wataalamu kutoka nje kwenye maeneo ya kimkakati ni muhimu ili kutusaidia kwenye kukuza rasilimali yetu na kutuunganisha na mifumo ya kimataifa.

Mheshimiwa Spika, upatikanaji wa vibali huchukua muda mrefu na husababisha walengwa kutoka nje kubadili mawazo na kuacha kuja kufanya kazi Tanzania.

Mheshimiwa Spika, katika nchi za jirani katika ukanda wa Afrika Mashariki, maprofesa wa Kenya na Uganda hustaafu wakiwa na miaka 70. Kutokana na uwepo wa maprofesa hawa kwenye mifumo ya ufundishaji na utafiti, vyuo vikuu vya Kenya na Uganda vina ubora wa kuzidi vile vya Tanzania katika orodha ya vyuo bora duniani.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ubaguzi wa kupata mikopo kwa wanafunzi wanaoomba mikopo kwa vyuo vikuu kutokana na shule walizosoma hata kama ufaulu wao unafanana. Wanafunzi waliosoma shule binafsi wamekuwa wakinyimwa mikopo kwa kigezo kwamba wana uwezo wa kifedha. Jambo hili ni la kibaguzi na sii halali.

Mheshimiwa Spika, wazazi wanaosomesha watoto wao shule binafsi si kwamba wana uwezo mkubwa wa kifedha bali hujinyima ili watoto wapate elimu bora.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuelezea changamoto za hapo juu, naishauri Serikali kufanya yafuatayo; kwanza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora wapitie sheria na kuongeza umri wa maprofesa kutumika kwa mikataba uanzie pale wanapostaafu wakiwa na miaka miaka 65 na waendelee hadi wanapofikisha miaka 75. Hii haina hasara kwa Serikali kwani wanapostaafu mishahara yao inakuwa bado iko kwenye ikama. Nchini Kenya maprofesa hustaafu wakiwa na miaka 70.

Mheshimiwa Spika, kuwaandaa hawa wataalamu, Serikali hutumia gharama kubwa sana. Tunapositisha huduma zao, vyuo binafsi huwachukua bila gharama na kuwatumia kuwajengea sifa, ilhali vile vya Serikali vinadorora.

Pili, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia iwasiliane na Wizara ya Utumishi na Utawala Bora itoe vibali vya kuajiri wanataaluma wa kutosha kuendana na idadi ya wanafunzi wanaodahiliwa. Hii ni pamoja na kuajiri wataalamu kutoka nje katika maeneo ya kimkakati kama yale ya sayansi, uhandisi na hesabu.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Bodi ya Mikopo hutoa mikopo na si zawadi, naishauri Serikali kuondoa ubaguzi kwa wanafunzi wanaojiunga vyuo vikuu bila kuangalia shule alikosoma.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.