Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hii Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa siku ya leo kupata nafasi hii ya kuweza kuchangia Sekta hii ya Elimu. Kweli sekta hii ina changamoto nyingi, tunao wasomi wengi nchi hii bado maisha yao ni magumu na wanahitaji support kubwa na kupata ajira katika Serikali Kuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa Jimbo langu la Mbogwe. Wananchi wangu wamenituma na hata mwaka 2021 nilisema hapa kwamba Jimbo la Mbogwe sina Chuo cha VETA. Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwenye bajeti yenu kwenye mpango huu nitashika shilingi mpaka mnithibitishie kwamba sasa Mbogwe tunaenda kupata chuo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na wenzangu wale wanaosema kuhusiana na mitaala yetu hii ya elimu kweli ni changamoto. Ukiangalia sasa hivi nchi hii tupo wasomi wengi sana na hatuna pa kwenda. Nami niweke mawazo yangu sasa kulingana na kwamba nami ni mfanyabiashara mkubwa, nazunguka nchi mbalimbali. Maana elimu neno la Mungu, linasema, “mkamateni elimu, msimwache aende zake.”

Mheshimiwa Naibu Spika, kiukweli naungana na Mbunge wa Manonga, ukiangalia masomo mengine ambayo tunayasoma, hayana faida katika maisha. Unakaa muda mrefu kufundishwa vitu ambavyo havipo, matokeo yake ni kufeli kila kitu; unafeli kimaisha na unafeli katika masomo yako. Ni vyema sasa Profesa, Waziri uliyeteuliwa mwaka huu, ukae uangalie, tunakutegemea sana kuleta mabadiliko makubwa katika sekta hii ya elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nami nichangie tu kwamba japokuwa wengine mnaweza mkashindwa kunielewa, Tanzania ni kubwa, tuna makabila zaidi ya 120. Mimi nimezunguka Mataifa mengi, unakuta watu wengine wanatumia lugha yao; ni kwanini wanatumia lugha yao? Maana elimu ni biashara. Unajua elimu ni kuchengana kitu kidogo tu! Nawaomba Wabunge hebu tubadilishe sheria ikiwezekana, maana sasa hivi kila Taifa linafundisha Kiingereza, kila mtu anajua. Utamchenga nani na utafanya biashara gani kuingiza faida katika pato la elimu? Mimi wazo langu tuangalie lugha moja katika makabila 120, lugha ambayo itaonekana ni bora, inafaa tuiingize kwenye system watu waje waisomee.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia China wanatumia lugha yao. Tukienda China huwa tunalazamika kuchukua Mkalimani; ukienda Rwanda huwa kuna wakati wanatumia lugha zao; ukienda Burundi, Angola kuna vipindi hata kwenye vyombo vya habari wanatumia lugha zao na wanapata faida.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiri tu wazi kwamba nilishawahi ku-act siku moja kwamba sijui Kiswahili hata Kiingereza. Nilikuwa Taifa fulani sitaki kulisema, nikajifanya sielewi Kiswahili, nikawa naongea Kisukuma tu, lakini kwa vile nilikuwa na bidhaa ambayo wanaihitaji, kwanza yule Mkalimani alipata hela kutokana nami. Maana alichokuwa anawaambia tu tajiri hajui kiswahili wala Kiingereza. Kwa maana hiyo ililazimika mkalimani na mimi halafu anaenda kuwatafsiria kwamba tajiri anasema mkifika hii bei mzigo tutawauzia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sisi kama Taifa, lazima tukae tufikirie tunawachenga vipi kwenye huu ulimwengu wa mapambano ya kutafuta pesa. Nami niwe muwazi tu, ni Msukuma, lugha yangu mkiipa nafasi tukaweka kwenye system humu. Kisukuma kitaingia kwenye computer na Wachina watakuja kujifunza Kisukuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile hata Wazungu wakija kwenye migodi yetu wakakuta siku nyingine askari wanazungumza Kisukuma tu, ile hali itawafanya waweze kusoma.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba sisi tuna wasiwasi labda lugha yetu ya Kiswahili au lugha zetu za Kitanzania hazitaweza kutafsiri yale masomo. Nitoe mfano, hadi sasa umri nilio nao sijawahi kusikia kwamba X + Y itatamkwaje kwenye Kiswahili mpaka leo. Ukimwuliza Mwalimu anakwambia ni unknown. Ina maana mpaka sasa unknown XY mtu anafika Form Six anasoma unknown, kitu asichokijua. Kwa hiyo, labda tuna wasiwasi na lugha yetu ya Kiswahili kwamba hatuwezi kutafsiri haya masomo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea hiyo taarifa lakini nilichokuwa nataka niombe hili suala ni muhimu sana na Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri wa Elimu siyo suala la kuchekesha, ni suala la kukaa kama Taifa, tukaeni tufikirie ni wapi tulipoangukia maana tuliachiwa elimu na mkoloni, tukakaririshwa baadhi ya vitu ambavyo havipo. Hivyo watoto wetu mpaka leo wanasumbuka kuvisomea lakini kiuhalisia wakitoka mashuleni hautaona sehemu umeulizwa maneno X, sijui nini; yaani kinacho-matter katika siasa na elimu ni jinsi gani unajipambanua kupata hela, kupata mafanikio na kuleta maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, kwa kuwa sasa hivi nchi yetu inasifika kwa madini pamoja na bidhaa nyingine, na Tanzania ni Tajiri, ni kitu tu cha kuelewana. Tukikubaliana Wabunge hapa, tuweke lugha gani ili Mataifa mengine yaje yajifunze kwetu ili tupate fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo jambo lingine tena katika Wizara hii. Naomba kwa vile yeye ndio Waziri wa Elimu, tumepata kweli misaada mingi kutoka kwa mama yetu; majengo haya tuliyopewa ya UVIKO, lakini upungufu bado ni mkubwa. Ukiangalia haya majengo yametolewa, lakini hayana vyoo wala walimu wa sayansi katika mashule hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, uone sasa sababu, na ikiwezekana baada ya Bunge hili, naomba Mheshimiwa Waziri twende kwenye Wilaya yangu tukatembelee uweze kuni-support kwa kuwa mabadiliko ni magumu sana. Kama nilivyotoa ushauri hapa kwamba tuingize lugha nyingine, najua itachukua muda, twende na huu mfumo uliopo. Ni vyema sasa, yaani kila sehemu waweze kupata hii elimu iliyopo pamoja na kwamba wengine tumeshastukia tayari. Baadhi ya Wabunge tumeshastuka kwamba tunakoelekea siko, kwamba hautofautishi mtu aliyesoma na yule ambaye hajasoma ukiwaona wanatembea barabarani au wanasimamia miradi yao tofauti na cheti.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile naomba hivi vyeti wanapomaliza chuo kikuu; nimeona katika ukurasa wa 74 hapa, NMB wametoa Shilingi bilioni 200. Unaonaje Waziri sasa hao waliomaliza elimu ya juu wakapata fursa ya kukopa angalau kujiendeleza katika maisha yao tofauti na hii na kusomea tu? Maana kuna watu wazuri, lakini hawana chanzo, pa kuanzia hawana. Kwa kuwa wana address na wana vyeti, wakopeshwe na mabenki ili waweze kufanya biashara pamoja na kufanya vitu vingine. Maana tukiangalia katika soko la ajira na kwenyewe ni changamoto, hatuwezi kuajiri watu wote hawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri aangalie sasa katika takwimu waliomaliza mwaka 2021 na mwaka 2020, wangapi wakopeshwe waweze kuendeleza maisha yao? Ahsante sana. (Makofi)