Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia hoja mbalimbali katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa siku ya leo ningependa kwa kuanzia nijikite kwenye ukurasa wa 32 na 33 wa Hotuba ya Mheshimiwa Waziri, Kipengele cha 34 kinachohusu uthibiti ubora. Kwa ujumla wathibiti ubora ni wataalamu wetu muhimu sana katika kutuboreshea elimu yetu, kwa sababu wamekuwa wakisimamia Sera ya Elimu kwa shule zetu za msingi, sekondari, vyuo pamoja na shule za awali; pia wamekuwa wakitoa ushauri mzuri kwa wataalamu wetu kama walimu, wakufunzi pamoja na wadau wengine; vile vile wamesimamia vizuri ufundishaji na ufundishwaji unaozingatia mtaala wa elimu uliopo; vilevile wamefuatilia kwa karibu utekelezaji wa majukumu ya elimu unaozingatia viwango vilivyowekwa. Hata hivyo nasema, kwa kiasi kikubwa hawa wathibiti ubora wamesahaulikana sijui ni kwa nini? Labda kwa sababu ya nature ya kazi yao au sababu ni ipi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilikuwa Mkurugenzi wa Halmashauri miaka saba iliyopita; vitu vingi wanakuja kuomba; vifaa vingi vya kutendea kazi wanakuja kuviomba, kama vile vyombo vya usafiri, ofisi; wanaomba kwa Wakurugenzi kama siyo kwa ma-DC. Kwa hiyo, naomba Serikali ijaribu kuona kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia namna ambavyo wataboresha kwa kuwapatia vitendea kazi sawia vinavyoweza kuboresha shughuli zao kutokana umuhimu wa shughuli zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia mwaka 2014 Serikali ilitoa waraka ulioitwa Waraka Na. 3 wa mwaka 2014. Waraka huu ulihusiana na maslahi ya mishahara, posho za madaraka kwa watumishi wa sekta ya elimu, ulitolewa na Wizara ya Utumishi kupitia Ofisi ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Utumishi. Ulieleza kinagaubaga namna wale viongozi wetu wa ngazi ya wilaya wanaohusika na masuala ya uthibiti ubora watakavyolipwa mishahara yao. Ulieleza kwa uwazi kwamba wale Wasimamizi wa Ofisi za Wilaya kwenye masuala ya uthibiti ubora watalipwa mshahara wa kiwango cha LSS E1 sawasawa na Maafisa Elimu wa Wilaya, Maafisa Elimu wa Shule za Msingi wa Wilaya na wa Sekondari. Ila wale wa kanda mishahara yao kwa mujibu wa ule waraka ilionesha kwamba, wangelipwa mishahara sawasawa na wale Maafisa Elimu wa Mikoa ambayo ni LSS E3.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha ajabu ni kwamba, hawa Maafisa Elimu wa Mikoa na Wilaya, mishahara yao ilipanda mara moja kuanzia mwaka wa fedha 2015/2016, lakini wale Maafisa Uthibiti Ubora wa Wilaya na Kanda mishahara yao haijapanda mpaka leo.

Kwa hiyo, naomba Serikali iweze kuwapandishia mishahara hawa Maafisa wa Wilaya na ikiwezekana wawalipe na arrears zao ili waweze kulitumikia Taifa letu ipasavyo. Bila assurance kwenye masuala ya elimu tutakuwa tunafanya kazi bure kwa sababu uthibiti utakuwa haufanyiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, masuala mengine ninayopenda kuchangia leo ni changamoto ambazo zimebaki baada ya kuwa tumepata miundombinu ya madarasa, kumekuwa na upungufu bado wa walimu, hasa wa masomo ya sayansi kwenye shule zetu za sekondari. Naomba hili Serilikali ilifanyie kazi ili tupunguze idadi ya upungufu huu uliopo na hatimaye tuweze kuboresha elimu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye upande wa shule shikizi, kama nilivyosema hapo mwanzo, kwenye jimbo langu peke yake, madarasa 23 yamejengwa, lakini watoto bado wanasoma shule za mbali licha ya madarasa kuwepo, kwa sababu hakuna walimu wa kufundisha kwenye zile shule. Kuna baadhi ya shule katika jimbo langu, kwa mfano kule Tipo Mkongo, Kata ya Kandawale, pale Kipatimu, kuna sehemu wanaita Ngingama, kuna sehemu kule Mbelenje, Kibata, lakini kuna sehemu wanaita Namadhugutungu; ukitoka shule mama kwenda shule ile ambayo imejengwa yenye madarasa ya kutosha, lakini walimu hawapo, wanalazimika kutembea umbali mrefu, tena ni watoto wadogo wenye umri mdogo sana. Kwa hiyo, naomba Serikali iliangalie hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Serikali iangalie katika eneo la tundu za vyoo katika shule, ziko chache; meza na viti katika shule zetu za sekondari ni pungufu, lakini pia watoto wetu wa shule za sekondari wanatembea umbali mrefu sana. Wanatembea kati ya kilometa 12 kwenda na kurudi hadi kilometa 18 kwenda katika shule ambazo wanasoma. Kwa hiyo, katika eneo hili naomba kuishauri Serikali iwekeze pia katika eneo la mabweni, tuwe na mabweni ya kutosha ili watoto ambao wanatoka mbali, basi waweze kukaa shuleni wasome pale, walale pale, ili waweze kukaa katika mazingira mazuri ambayo yanaendana na taaluma zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye maslahi ya walimu; miaka ya 1990 Serikali ilifuta kitu kinaitwa Teaching Allowance. Hili ni jambo ambalo siyo zuri sana kwa upande wangu ninavyoliona, kwa sababu walimu wamekuwa wakifanya kazi kubwa ya kutia nuru kwenye vichwa vya watoto wetu kwa maana ya kuwafundisha na wana kazi nyingi nje ya muda wa kawaida wa masomo.

Mheshimiwa Naibu Spika, walimu wanatakiwa kuandaa lesson notice, walimu wanatakiwa kuandaa lesson plan, walimu wanatakiwa kuandaa scheme of work, walimu wanatakiwa kuandaa teaching aids na mambo mengine mengi ambayo wanayaandaa nje ya muda wa kawaida mpaka nyumbani wanapofika, wanakuwa wanaandaa vitu kama hivyo kwa ajili ya kuwezesha watoto wetu waweze kusoma vizuri, lakini hii allowance iliondolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii inafanana na ile ya On- Call Allowances ambayo inatolewa kwa watumishi wa afya ambayo mpaka leo haijafutwa, lakini pia wapo watumishi wa kawaida wanalipwa Extra Duty Allowances. Kwa nini walimu tu peke yao ndio wakose malipo ya ziada, tena kwa kazi halali ambayo wanaitumikia nchi hii? Kwa hiyo, nilikuwa naomba Wizara ilitafakari hili jambo kwa kina ili kuongeza morali ya walimu katika kufundisha, walipwe Teaching Allowance. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna Maafisa Elimu wa Kata. Kwa bahati nzuri Serikali yetu ya Awamu ya Tano mwaka 2016 iliwakabidhi pikipiki watumishi, hawa Maafisa Elimu Kata. Zile pikipiki kwa sasa zimechoka sana. Naomba Serikali ione uwezekano wa kuwapa pikipiki upya kwa sababu ni miaka zaidi ya mitano imepita wakiwa na hizo pikipiki. Ninaamini kwamba nafasi hizi za Maafisa Elimu Kata ni za muhimu sana kwa ajili ya maendeleo ya elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)