Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Kasalali Emmanuel Mageni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sumve

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Nitumie fursa hii kuwapongeza watu wa Wizara ya Elimu kwa kazi nzuri wanayofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze mchango wangu moja kwa moja kwa kuwaletea kilio cha watu wa Wilaya ya Kwimba. Tangu mwaka 2019 Serikali ilianza mchakato wa kujenga Chuo cha VETA kwenye Wilaya ya Kwimba katika Mji wa Ngudu ambao ni Makao Makuu ya Wilaya. Ujenzi wa hiki chuo umechukua sasa miaka takribani mitatu na Mheshimiwa Waziri ulikuja ziara kwenye Wilaya yetu ya Kwimba; na alikuwepo pia Mkurugenzi wa VETA aliahidi kwamba watamaliza mapema na Serikali iliahidi watamaliza mapema hakijakwisha mpaka sasa. Sasa sisi watu wa Kwimba hatupendelei sana kuwa na magofu ya kujificha wezi kwa sababu kimekuwa cha muda mrefu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwashauri Wizara ya Elimu, nilifikiri matatizo ya usimamizi yamebaki Serikali za Mitaa, lakini naona na Wizara ya Elimu kwenye usimamizi wa miradi yenu hasa mimi naona mfano wa hiki Chuo cha VETA kilichoko Kwimba, yaani Chuo kinajengwa Kwimba anayesimamia ni Chuo cha VETA Kagera. Hapo unaona kwamba ni kutengeneza maigizo fulani na kukwamisha shughuli za Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa wanaojenga Chuo cha VETA kwenye Wilaya ya Kwimba badala ya kuwa neema wametuletea matatizo. Kuna wajasiriamali ambao nilisema wakati wa ziara ya Naibu Waziri wametumia fedha zao wameleta kokoto, wameleta mawe mpaka leo hawajalipwa na nilisema na Mkurugenzi wa VETA aliahidi mbele yangu kwamba watalishughulikia, watawalipa. Wamefilisi watu, yaani badala ya kuwa neema imekuwa ni laana. Sasa tuwe serious kwenye jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kabisa hawa watu wa Wizara ya Elimu jambo la kumalizia VETA ya Kwimba na jambo la kulipa watu walioshiriki kwenye ujenzi wa VETA hiyo, ambao niliahidiwa kama Mbunge wao siku ya ziara ya Wizara husika, mpaka leo hawajatekeleza, wanawatisha hao watu, wanaomba rushwa na vitu vingine. sasa naomba Wizara ya Elimu wawe serious, walimalize suala la VETA Kwimba watu waanze kusoma lakini, yalipwe madeni ya watu wote wazabuni wa Kwimba walioweka nguvu zao pale. Najua bajeti ilikuwepo, hawawezi kuitisha kokoto wakati hakuna bajeti, vinginevyo tunataka kufilisi watu wetu na kuleta vitu ambavyo havina msingi huko site.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo nataka nichangie hapa ni kwamba Wizara ya Elimu ndio uti wa mgongo wa maendeleo ya nchi yetu, ili nchi iendelee ni lazima fursa na matatizo na vitu vilivyopo kwenye nchi vifahamike. Sasa tunaweza kufahamu vipi matatizo yetu, tunaweza kufahamu vipi fursa zetu na tunaweza kuwa na mbinu gani za kutatua matatizo yetu, kuna kitu kinaitwa utafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Elimu ndio wanaosimamia Vyuo Vikuu na Vyuo vya Elimu ya Juu. Vyuo Vikuu ndio kitovu cha utafiti kwenye nchi yoyote inayotaka kuendelelea na nchi yoyote inayotaka kutatua matatizo ya watu wake.

Hata hivyo, nasimama hapa nikiwa na masikitiko, Serikali iliahidi kwamba asilimia moja ya GDP, tutakuwa tunapeleka kwenye utafiti, kitu ambacho hatujakifanya. Utafiti kwenye vyuo vyetu vya elimu ya juu umekuwa ukitegemea fedha za wafadhili, mfadhili hawezi kuleta fedha ambayo haisaidia jambo lake. (Makofi)

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, ili sisi tutatue matatizo yetu tunahitaji kuwa na fedha zetu wenyewe.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

MHE. KASALALI E. MAGENI: …na tuziwekeze kwenye utafiti.

T A A R I F A

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba sio tu vyuo vyetu vinategemea fedha ya tafiti kwa fedha za nje, lakini tu hata mtoa fedha akitoa tafiti ili mwanachuo afanyie tafiti, Mwalimu huyo huyo aliyepewa fedha mwanachuo afanye tafiti anamshika hamalizi chuo miaka sita ya PhD. Naomba nitoe taarifa hiyo.

NAIBU SPIKA: Ahsante. Mheshimiwa Mageni.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naipokea hii taarifa. Kwa kuweka msisitizo ni kwamba, hawa wafadhili wanaofadhili utafiti wetu wanawatumia wasomi wetu kutatua matatizo yao. Sisi tunao hawa wasomi, lakini tumeshindwa kuwatumia kutatua matatizo yetu, kwa sababu nafikiri tumeshafikia wakati tumekosa vipaumbele kwenye elimu, kwamba, umefika wakati sasa hata watu wanaoweza kutushauri kufahamu matatizo yetu hatuwapi fedha za kufanya hiyo kazi. Badala yake hao Maprofesa wetu/Madaktari tuliowajaza kwenye Vyuo Vikuu wanatumika na nchi za nje, wanatumika na wafadhili kufanya utafiti kwa ajili ya hao wafadhili badala ya kufanya utafiti kwa ajili ya nchi yetu. Kwa hiyo, nataka niishauri Wizara kwamba nguvu kubwa iwekeze kwenye utafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu ina matatizo mengi, kwa mfano, tatizo moja tu la wizi, ubadhirifu na kukosekana kwa uaminifu kwenye usimamizi wa mali za umma. Tumekuwa tukilalamika huko kwenye halmashauri, tumekuwa tukilalamika kila sehemu, je, tumewahi kuwekeza kwenye utafiti kujua chanzo cha hili tatizo? Kwa sababu, hawa wanaoiba kila siku tunatengeneza CAG nenda kakague, Waziri nenda katumbue, tunaowatumbua ni wasomi wetu, wanaoiba ni wasomi wetu, tumeshatafiti elimu yetu ina msaada gani kenye Taifa letu? Kama inatuzalishia wasomi wanakuwa wezi, wasomi ambao wanahitaji ziara za Waziri awatumbue ndio wafanye kazi, kwa hiyo, hatuwekezi kwenye kutatua matatizo yetu, tunawekeza kwenye vitu ambavyo havina msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wamezungumza Waheshimiwa Wabunge hapa kuhusu mfumo wetu wa elimu. Hata mimi ukiniuliza mimi mwenyewe ni mfano, nimesoma form four nafikiri nilisoma masomo 10, ukiniuliza hayo masomo niliyoyasoma kwanza hata nilishayasahau. Yaani tunapoteza muda mwingi kwenye mfumo wa elimu wa kikoloni kupotezea muda watoto wetu mashuleni, badala ya kuweka mfumo ambao unatatua matatizo yetu ya sasa na jibu la haya yote hatufanyi utafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika,Nani amefanya utafiti nani amejiridhisha kwamba ni lazima mtoto wa shule ya msingi akae miaka saba shuleni? Atoke hapo aende sekondari miaka minne, aende A Level miaka miwili, halafu sasa hao watu wetu ambao tunawasomesha muda wote huo na wale wanaosoma miaka minne Kenya, tukiwaweka sokoni tunaona tofauti gani? Kwa hiyo ni lazima tufike wakati kama Waheshimiwa Wabunge walivyoshauri kwamba tufike wakati mfumo wetu wa elimu ya msingi na sekondari, tuuangalie.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuna sababu ya kuweka watoto shuleni muda wote huo, tunawapotezea muda wanakuja kumaliza vyuo vikuu ni wazee, wanakwenda kazini muda mfupi tu wameshastaafu, lakini muda mwingi wameupoteza wanasoma logarithm, wamesoma kipeuo cha nini, mtoto unakuta amerundikiwa masomo mpaka anachoka kusoma. Unakuta mimi niliyoyasoma O Level nimeshasahau, sina kazi nayo, nakumbuka tu labda niliyosoma Chuo Kikuu machache ambayo niliyafanyia kazi. Kwa hiyo, tutafute tu namna ya kuwapa watoto wetu package ambayo inawastahili kwa ajili ya kutatua matatizo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee pia suala la Bodi ya Mikopo, Waheshimiwa Wabunge hapa wamelizungumzia. Vigezo vya kutoa mikopo imekuwa ni kuangalia umaskini na uhitaji wa mtu. Hawa watu wetu waliopo Bodi wako kama wangapi wangapi hao wana uwezo wa kujua huyu ni maskini na huyu ni tajiri?

Nafikiri tufike wakati tunatengeneza tu utaratibu mwingine wa kuonea watu, mimi Mbunge wa Sumve, kuna watu wengi kule wananilalamikia na ukiwaangalia ni maskini wamenyimwa mkopo. Vigezo vinavyotumika sio rafiki na naamini hatuna nguvu kazi wala wataalam wa kutosha kutafiti na kujua huyu ni maskini, huyu sio masikini. Cha msingi hapa tutafuteni namna ya kusomesha watu wetu. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)