Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara (Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji) na Naibu wake (Mheshimiwa Exaud Kigahe) na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajikita kwenye sekta ya uwekezaji kwenye viwanda katika jimbo langu la Moshi Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkoa wa Kilimanjaro kihistoria ni mkoa ambao ulikuwa na viwanda vingi ambavyo vilichangia sana kuinua pato la wananchi wa mkoa huu na pato la Taifa kwa ujumla. Viwanda hivyo kwa sasa vingi vimefungwa kutokana na sababu mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya kiwanda kilichokuwa kimepata mafanikio makubwa sana ni kile kiwanda cha kukoboa mpunga cha Kilimanjaro Paddy Hulling Co. Ltd kilichopo Chekereni – Moshi, katika Kata ya Mabogini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda hiki kiko kwenye eneo ambalo linazalisha mpunga mara mbili hadi tatu kwa mwaka. Kiwanda hiki hakifanyi kazi tangu Septemba, 2014. Kiwanda cha kukoboa mpunga kilikodishwa na Chama Kikuu cha Ushirika cha Kahawa (KNCU) na baada ya kushindwa kukiendesha, mkoa ulimshauri Msajili wa Hazina kukirudisha Serikalini ili atafutwe mwekezaji mwingine anayeweza kukiendesha. Tayari Msajili wa Hazina amerejesha kiwanda hiki Serikali tangu tarehe 18/10/2018, lakini bado hajapatikana mwekezaji na shughuli zimelala. Kutokuwepo kwa kiwanda hiki kumeondoa fursa ya wakulima kupata bei nzuri ya mpunga na ajira kiwandani kwa wana Moshi Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda cha pili kilichopo jimboni kwangu na hakifanyi vizuri ni kiwanda cha bidhaa za ngozi Msuni kilichopo Kata ya Uru Kaskazini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda hiki kinamilikiwa na Kamati ya Maendeleo Kata ya Uru Kaskazini (WDC). Kina uwezo wa kuzalisha bidhaa mbalimbali za ngozi kama viatu, mikoba na mikanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyoomba mwaka jana, narudia tena kuiomba Serikali itume wataalamu wa TiRDO kwenye kiwanda hiki ili ushauri wa kitaalamu upatikane na kiwanda hiki kifufuliwe na kuunga juhudi za wana ushirika huu kwenye kukuza uchumi wao na wa Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Moshi Vijijini ni maarufu sana katika uzalishaji wa mazao ya kilimo na mifugo. Kama Serikali itakuwa na mikakati ya kuhamasisha uwekezajj wa kuanzisha viwanda vidogo vidogo vya kusindika mazao ya kilimo na mifugo, hii itasaidia kutengeneza ajira na kuongeza kipato cha wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo yangu hapo juu, naishauri Serikali ifanye yafuatayo: -

Kwanza, Wizara itafute mwekezaji katika Kiwanda cha Kukoboa Mpunga cha Kilimanjaro Paddy Hulling Co. Ltd kilichopo Chekereni – Moshi, katika Kata ya Mabogini. Kiwanda hiki kinaweza kuwa ni chanzo cha kusafirisha nje mchele ulioongezwa thamani na kuwapatia wakulima kipato na Taifa kwa ujumla.

Pili, Vyama vya Ushirika vilivyopo Jimbo la Moshi Vijijini vihimizwe na kuhamasishwa kuwa na viwanda vya kuchakata mazao mbalimbali ya kilimo na mifugo na kuyaongezea thamani ili kuzalisha bidhaa zinazotokana na kahawa, ndizi, mbogamboga, nafaka, mikunde, maziwa, asali, alizeti na mengine mengi.

Tatu, kama nilivyoomba mwaka jana, naomba tena Shirika la Utafiti wa Viwanda Tanzania (TiRDO) lishiriki kikamilifu kwenye kutoa ushauri wa kitaalamu kukifufua kiwanda cha bidhaa za ngozi Msuni kilichopo Kata ya Uru Kaskazini.

Nne, Serikali ianzishe programu maalumu itakayowashirikisha wadau muhimu wa viwanda kama vile TiRDO, SIDO, TCCIA, VETA na CTI ili watoe mafunzo ya kuhamasisha ujasiriamali wa viwanda Mkoani Kilimanjaro na hususani katika Jimbo la Moshi Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.