Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye Wizara yetu hii ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara. Kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kupanua diplomasia ya Kimataifa ya kiuchumi ambako sasa itafungua fursa kubwa nyingi sana za uwekezaji hapa nchini. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze pia Waziri wetu wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, dada yangu Mheshimiwa Ashatu pamoja na timu nzima ya Wizara kwa kazi zile wanazozifanya pamoja na hotuba nzuri aliyowasilisha katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita katika maeneo machache la kwanza ni mazingira ya ufanyaji biashara hapa nchi (easy of doing business). Kwenye ukurasa wa 26 mpaka 27 wa hotuba hii, ameelezea ufanyaji wa biashara hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ripoti ya Benki ya Dunia ya Mwaka 2018 inasema Tanzania ilikuwa nchi ya 141 kati ya nchi 190; lakini nchi ya jirani ya Kenya ilikuwa 56 kati ya nchi hizo190; Uganda ilikuwa 116; Rwanda ilikuwa ya 38. Mwaka 2019 Tanzania ni nchi ya 141 kati 190 na Kenya ya 56, Uganda 116 na Rwanda 38. Nchi yetu katika region hii ndiyo iko chini kabisa urahisi waufanyaji biashara hapa nchini. Kwa hiyo niombe sana Wizara ya Uwekezaji Viwanda na Biashara iitoe nchi yetu katika...

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa, Mheshimiwa Abbas Tarimba.

T A A R I F A

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, anayozungumza Mheshimiwa Sillo ni mambo mazito sana, ni mambo muhimu sana na ukiangalia maandiko mengi ya Serikali yanahubiri private sector kwa maana ya taasisi binafsi au sekta binafsi kwamba ndiyo engineer ya growth, kila mahali Serikali inazungumzia hivyo. Vile vile ukiangalia Tanzania Private Sector Engagement Fact Sheet inatuambia kwamba private sector yenyewe mchango wake ni asilimia 90 ya ajira hapa Tanzania, lakini vile vile ni asilimia 60 ya uwekezaji na zaidi ya asilimia 80 ya kodi za Serikali. Hivyo analolizungumza ni suala zito ambalo naliunga mkono, naomba nimpe taarifa katika mchango wake. Ahsate sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Daniel Sillo, taarifa hiyo.

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hii ya Mheshimiwa Tarimba, mjumbe makini kabisa wa Kamati ya Bajeti naipokea kwa mikono yote miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mwarobaini wa tatizo hili nini? Mwarobaini wa suala hili ni ukamilishaji wa Blueprint for Regulatory Authority – Mpango Maalum wa Kuboresha Ufanyaji wa Biashara hapa Nchini. Nimwombe Mheshimiwa Waziri hili jambo la Blueprint limeanza muda mrefu, naomba likamilike. Zipo taasisi za Serikali zinafanya ama shughuli zinazofanana, lakini mwekezaji au mfanyabiasha anaingia kwenye taasisi nyingi za Serikali. Naamini kabisa kama huu mpango utakamilika basi itarahisisha sana ufanyaji biashara hapa nchini. Tunalia kila siku kwamba tupanue wigo wa walipakodi, tunapokuwa tunawafukuza hawa wafanyabiashara hatuwezi kukuza wigo wa walipakodi hapa nchini na kwa maana hiyo Serikali inapoteza mapato mengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatarijia kupata ajira kwa Watanzania Ilani ya Uchaguzi ya 2025 inasema tuajiri Watanzania milioni nane. Bila kuwezesha Sekta Binafsi hatuwezi kufikia lengo hilo, kwa hiyo niiombe sana Wizara iboreshe mazingira ya wafanyabiashara hapa nchini ili nchi yetu itoke kwenye rating hii ya nchi iende kwenye hatua ya juu kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine la kuelekeza; nielekeze kwenye mifumo, ukienda kwenye taasisi zetu unakuta kuna OSHA, kuna TBS, kuna TMDA waweke mifumo inayosomana ili mwekezaji au mfanyabiashara akienda ofisi moja akilipa basi iende moja kwa moja kwenye zile sector zingine kuliko kumsumbua mfanyabiashara aingie jengo hili, aingine jengo lile, tunajikwamisha wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni eneo la uwekezaji. Hapa naipongeza Serikali imechukua hatua mbalimbali katika mazingira ya uwekezaji hapa nchini. Tunapenda Kituo chetu cha Uwekezaji (TIC) pamoja na EPZ kiwe ni one stop shop kwamba akiingia mfanyabiashara pale, mambo yake yote yanakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kwenye EPZA tuna TRA pale, tunataka mifumo isomane mtu wa TRA pale awe na maamuzi, akishaona mfuko umehakikiwa pale ukienda bandarini unasafiri kwenda nje ya nchi bila shaka biashara inafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana kwenye eneo la TIC pia tuweke wataalam wa Serikali wenye maamuzi. Inapoteza muda mwingi sana unaweka watu ambao hawana maamuzi, document zinafika pale zinabebwa kwenda makao tena tunapoteza muda mwingi sana wa wafanyabiashara. Kwa hiyo niombe sana wawepo watu watoa maamuzi wa Serikali katika maeneo haya ambayo tunayasema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa sana, tumeletewa wawekezaji wengi, kwa hiyo, niombe sana Wizara ijielekeze katika kuhakikisha kwamba tunamuunga mkono Mheshimiwa Rais katika juhudi hizi za kuweka wawekezaji hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maeneo mengine ya wawekezaji, yapo mashamba makubwa ya wawekezaji hapa nchini, lakini yana migogoro na wananchi, mashamba hayaendelezwi, watu wamewekeza, wanachukua robo ya shamba, lingine sijui wanakopea, kwa hiyo, wananchi wetu hawapati maeneo ya kufanya shughuli zao za uchumi kama kilimo, ufugaji na kadhalika. Niombe sana Wizara ijielekeze kutatua migogoro hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukiwa na migogoro mwekezaji hatawekeza. Kwa hiyo hata Serikali inakosa mapato iliyotarajia, lakini wananchi wetu wanakosa kufanya shughuli zao za uchumi, lakini Serikali pia inakosa mapato ambayo ingeyapata. Kwa hiyo niombe sana Waziri wetu msikivu kabisa, dada yangu Mheshimiwa Ashatu ajielekeze kabisa ili wananchi wetu waendelee na shughuli zao za kiuchumi kwa manufaa makubwa ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano, kule Halmashauri ya Babati kuna mashamba makubwa kwenye Kata za Kiru, Magugu, Magara na Kisangaju lakini migogoro mitupu. Napongeza Serikali kuna ziara za Waziri wamefanya kazi kubwa, lakini bado migogoro ipo. Naiomba Serikali iweze kujipanga vizuri kumaliza migogoro hii ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana na naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)