Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Simai Hassan Sadiki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana nami kuweza kunipa fursa hii ya kuchangia katika hotuba ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Ikumbukwe ya kwamba hii ni Wizara Mama ni Wizara ambayo imebeba suala zima la ulinzi wa raia pamoja na mali zao, kwa hiyo uhai wetu, usalama wetu unategemea zaidi ufanisi na uwajibikaji katika majukumu ya Watendaji wa sekta hii.

Mheshimiwa Spika, kuna nchi duniani hazina Jeshi lakini hakuna nchi iliyokuwa haina Polisi, Magereza, Uhamiaji pamoja na Zimamoto na Uokozi ila cha kusikitisha ni kwamba bado Jeshi hili hatulithamini na kulipa hadhi inayotakikana. Hivi mpaka leo bado tunang’ang’ania kuendeleza kujenga kuwa na wingi wa vituo wakati maaskari huku wanakabiliwa na changamoto nyingi? Maaskari wanalalamika hawana sehemu za kukaa, Askari wanalalamika vifaa vya utendaji kazi, maaskari wanapata changamoto kubwa wanapostahiki mafao yao, thamani yao iko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sioni sababu na wala sioni haja ya kusema kwamba tunaenda kupiga marufuku suala zima la Jeshi la Polisi au maaskari wengine kutoa michango wanapoenda masomoni wakati tunashindwa kuwajengea nyumba na kuwarekebishia maisha yao. Kwa sababu Askari wanaoenda masomoni ni wachache zaidi ukilinganisha na wale wanaokosa makazi na suala la makazi kwa maaskari ni la kila siku, lakini suala la masomoni ni suala miezi miwili miezi mitatu wamemaliza! Sasa hili fungu ningeomba liondoshwe lipelekwe huko kunakojengwa nyumba za makazi za maaskari.

Mheshimiwa Spika, wakati juzi ninazungumza hapa nilipouliza swali langu la msingi Mheshimiwa Naibu Waziri alijibu kwamba Nungwi kuna ukosefu wa nyumba za maaskari, akatoa agizo kwa wawekezaji na wahisani wanaomiliki nyumba maeneo yale wawapangishe maaskari wale. Sasa najiuliza hivi Nungwi kodi chumba kimoja kile chumba kimoja tu kinaweza kufika Shilingi 100,000 hadi Shilingi 150,000 hivi ni Askari gani ana uwezo wa kulipa hizo gharama si tunawatengenezea mianya ya kuchukua rushwa kabisa? Suala hili naomba liangaliwe kwa kituo zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la mafunzo kwa askari ni jambo muhimu lakini lazima tuwafundishe Askari kufanya kazi kulingana na mazingira, sambamba na hilo lazima wakati tunapogawa hawa maaskari na kuwapeleka vituoni tuwapeleke kwa mujibu wa taaluma na ile sehemu wanayoenda.

Mheshimiwa Spika, hapa napenda nizungumze kitu kimoja lazima ieleweke sana na Mheshimiwa Waziri, kuna maeneo tuliyo nayo hayafananii, Zanzibar hii tuna maeneo yamekabiliwa zaidi na sekta nzima ya utalii ambapo raia unaweza ukawakuta inawezekana ni wachache zaidi kuliko hao wageni wanaokuja. Sasa changamoto inakuja mgeni anapokuwa na kesi yake au anapokuwa na changamoto yake aende kituo cha Polisi unakuta maaskari wanapenya kwa mlango wa nyuma kwa sababu hawajui kiingereza. Kiingereza chao kikubwa photo man sasa photo man inaendaje? Sasa hayo mafunzo unayotoa isiwe ya kupiga kwato tu, lazima na lugha ifundishwe mtenge vitengo maalum katika maeneo kama yale Mheshimiwa Waziri. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, hili suala la mafunzo kwao ni suala moja la msingi vinginevyo tutaliaibisha Jeshi letu la Polisi lakini tutaibisha mitaala yetu ya elimu ya Tanzania. Katika hili napo Mheshimiwa Waziri nisipopata majibu ya msingi huenda nikazuia Shilingi yako Kaka yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala zima la ajira sekta yako ina asilimia kubwa ya masuala yanayohusika na Muungano, Zanzibar tuna asilimia 21 au watu 21 ndiyo wanaotakiwa kuajiriwa? Kwa sababu hizi nafasi hatuzioni zinapokuja, zinakuja Zanzibar tunasikia lakini wachache mwisho wa siku unakuja kukuta labda watu watatu, watu wanne kutoka sehemu nyingine na ubaya wa mambo, hii yote inasababishwa kwamba ajira hizi zinapitia Makao Makuu haziji kwa Mikoa na ndiyo maana Wabunge wengi wanalalamika kwamba zinapokuja ajira bora zipite Majimboni lakini sisi tusiende Majimboni tuzipeleke hizi ajira kunako Mikoa kwa sababu miongoni mwa sifa ili uajiriwe katika sekta hizi basi uwe na cheti cha JKU umepita JKU au JKT, sawa wanapotafuta watu wawe wanapita Mikoani hizi nafasi zinakuja Mikoani lakini sasa nyinyi wakati tayari watu wameshamaliza mafunzo mnataka kuajiri hamzingatii kigezo cha Mikoa na ndiyo maana unakuta Jeshi letu letu lina sura ya sehemu moja na Wabunge wengine wanalalamika. Suala hili lazima tuliangalie kwa makini sana.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)