Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu kwa ajili ya usalama wa Taifa letu. Nasema Wizara hii ni muhimu kwa sababu kwanza ndiyo Wizara pekee ambayo inahakikisha usalama wa raia na mali zao, lakini ndiyo wizara pekee ambayo inahakikisha usalama wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kuwapongeza baadhi ya watendaji wa Jeshi la Polisi ambao wanajitahidi kufanya kazi kwa uaminifu na kutekeleza majukumu yao kisheria; japokuwa wana mishahara midogo sana ambayo haitoshelezi, lakini pamoja na hayo wamekubali kufanya kazi kwa uaminifu kwa kulitumikia Taifa letu. Niwapongeze sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hayo kuna baadhi ya watendaji ndani ya Jeshi la Polisi ambao hawafanyi kazi kwa uaminifu na badala yake wamekubali kutumiwa vibaya na baadhi ya wanasiasa kwa kutekeleza tu matakwa yao. Tanzania ndiyo nchi pekee ambayo polisi haoni aibu kwenda kumkata mwananchi eti kwa sababu tu ametangaza kiasi cha rambirambi kilichopatikana msibani. Hili ni jambo la ajabu sana.

Mheshimiwa Spika, tuna baadhi ya polisi ambaye mpaka anakwenda kumkamata raia nyumbani kwake hamwambii ana mkamata kwa kosa gani? Anamchukua anamfikisha kituoni hamwambii amemkamata kwa kosa gani, anakaa naye siku ya kwanza, siku ya pili, siku ya tatu, mwananchi anauliza umenikamata kwa kosa gani? Anamwambia kosa utalikuta mahakamani, hili ni jambo la ajabu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwingine akibananishwa sana kwamba aambiwe umenikamata kwa kosa gani? Anachukua simu anapiga anasema huyu niliyemkamata nimpe kosa gani? Hili ni jambo la ajabu sana! Hii inaonesha tuna baadhi ya Askari Polisi ambao hawatambui majukumu yao na ni hatari sana kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna jambo lingine; katika maeneo yetu na ndani ya Taifa letu kuna baadhi ya uhalifu ambao unaendelea, lakini kuna biashara nyingi ambazo zinafanyika zisizokuwa halali. Wananchi siyo kwamba hawajui, wanajua isipokuwa kuna wakati wanaogopa kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi kwa sababu ya kuhofia usalama wao. Mwananchi anakwenda kutoa taarifa polisi kuonesha kwamba kwenye eneo fulani kuna mhalifu fulani aidha anafanya biashara haramu au anafanya biashara zisizokuwa sahihi, lakini baada ya yule mtuhumiwa kukamatwa jioni anaachiwa na ana ambiwa kabisa unajua aliyekuchongea ni nani? Ni mtu fulani. Mwisho wa siku wananchi wanashindwa kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi kwa sababu ya kuhofia usalama wao, kwa sababu mwisho wa siku yule mtu anapoachiwa anakwenda ku-deal na yule mtoa taarifa. Hii siyo haki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inataka mtoa taarifa alindwe. Matokeo yake, mwisho wa siku tumeendelea kufuga wahalifu ndani ya Taifa letu kwa sababu tu ya kushindwa kuwalinda watoa taarifa; hili ni jambo la hatari sana kwa Taifa letu. Tunapaswa kuwa na askari ambao wanakuwa ni waaminifu ili tulijenge Taifa lililo salama zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuchangia katika suala zima la magereza. Magereza za ndani ya Taifa letu zimekuwa na hali mbaya, mbaya, mbaya sana. Nasema hali mbaya sana kwa sababu hata mimi kuna baadhi ya magereza nimekaa. Magereza zetu zina hali mbaya isiyokuwa kawaida, miundombinu ni mibovu, hairidhishi kabisa yaani hata kwamba mtu analala humo ndani ukioneshwa cell ambayo watu wanalala wakati mwingine ni hatari kabisa hata kwa afya za wananchi wetu. Hali ni mbaya, lakini ukifuatilia katika Ripoti ya CAG iliyotolewa Machi, 2022, imeonesha wazi kabisa baadhi ya magereza ambazo zina mrundikano mkubwa wa wafungwa na mahabusu.

Mheshimiwa Spika, mfano mzuri ni katika Gereza la Keko, Dar es Salaam. Kwa mujibu wa Ripoti ya CAG inaonesha wazi kabisa gereza lile lina uwezo wa kupokea mahabusu na wafungwa 340, lakini badala yake lilikutwa likiwa na wafungwa na mahabusu 999; ni zaidi ya asilimia 194, jambo ambalo ni hatari sana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ukienda katika Gereza la Kingurungwa huko Lindi, kwa mujibu wa Ripoti ya CAG inaonesha wazi kabisa gereza lile lina uwezo wa kutunza mahabusu na wafungwa 39 lakini badala yake lilikutwa likiwa na wafungwa na mahabusu 88 zaidi ya asilimia 126. Hii ni hatari.

Mheshimiwa Spika, ukienda katika gereza la Kiomboi lililoko Mkoani Singida, Ripoti ya CAG inaonesha wazi kabisa kwamba gereza hili lilikuwa na uwezo wa kutunza wafungwa na mahabusu 58 lakini badala yake lilikutwa lina wafungwa na mahabusu 132 zaidi ya asilimia 128, hii ni hatari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, badala yake wafungwa na mahabusu wamekuwa wakiambukizana magonjwa mbalimbali ya kuambukiza, magonjwa ya vifua, upele na mambo mengine ambayo ni hatari kwa afya zao.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. STELLA S. FIYAO: Kengele ya kwanza.

SPIKA: Kengele ni moja tu, sekunde 30 malizia.

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, naomba kuishauri Serikali, kuna umuhimu mkubwa wa kuziondoa kesi ambazo upelelezi wake umechukua muda mrefu kukamilika, ikiwa ni pamoja na kesi za kisiasa ambazo wameendelea kuwashikilia watu kutoka Uchaguzi Mkuu, 2020 mpaka leo watu wanaendelea kushikiliwa katika kuta za gereza. Kuna haja ya kuziondoa kesi hizi ili kupunguza msongamano wa watu huko magerezani.

SPIKA: Haya. Ahsante sana.

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)