Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Nianze kuunga mkono hoja ya Mheshimiwa Kigua kwamba tatizo hili la mafuta ni kubwa na lina athari kubwa kwenye uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kusema kwamba, kwanza naipongeza michango mbalimbali ya Waheshimiwa Wabunge waliotangulia, lakini niseme tu kwamba hatua zozote tutakazozichukua zisiende kuleta athari katika ile mikataba ambayo tumeshaingia na wakandarasi wetu katika maeneo mbalimbali hususan katika maendeleo ambayo tayari tulishajipangia, REA ikiwa ni mojawapo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema hivyo kwa sababu tayari walishaingia mikataba na kwa sababu kazi lazima zifanyike, pale utakaposema kwamba simamisha fedha labda ya tozo mahali fulani ina maana utakuwa unasimamisha ule mradi, unless kama tutakuwa na uwezekano wa kutoa fedha kutoka maeneo mengine na kupeleka huko kama ambavyo imesemwa bajeti tayari ilishawekwa.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na suala ambalo tulimsikia Mheshimiwa Waziri, kulikuwa na jitihada ya kwenda kuongea moja kwa moja na wale wazalishaji wa mafuta ili tuweze kuyapata kwa bei ambayo ni rahisi au wao kutuuzia moja kwa moja, huo mpango sijajua ulifikia wapi. La pili ninaloliona ni kwamba suala la uadilifu na lenyewe lazima tulipigie kelele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Tabasam alizungumza siku ile hapa hatuna uhakika, lakini tunasema iko haja ya kufuatilia anapolia mtu yawezekana kuna jambo, iko haja ya kufuatilia ili tuone kwamba taratibu tulizojiwekea zinakwenda sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine niseme tu kwamba athari hizi za mafuta tumeziongelea zaidi kwa ujumla wake. Siku za nyuma tulikuwa na taasisi ambazo zilikuwa zinapanga bei ya bidhaa mbalimbali, sasa hivi ikiongezeka lita moja kwa Sh.100 au Sh.200, kila mtu anapandisha bidhaa mara mbili au mara tatu, huko ndiko wanakoumia wananchi zaidi. Kwa nini huko tumekuacha kunakwenda kiholela?

Mheshimiwa Spika, nimeangalia bei ya bati iliyokuwa inauzwa Sh.19,000 sasa hivi Sh.28,000 gauge 30; ukienda kwenye mafuta hivyo hivyo. Kwa hiyo, kuna maeneo tumeacha kuyasimamia ipasavyo, pamoja na haki ya wafanyabiashara kuweka bei ambayo ni bei huria, lakini… (Makofi)

MHE. KABULA E. SHITOBELO: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: …iko haja ya kufuatilia upatikanaji wa bei hizo.

SPIKA: Mheshimiwa Stella Manyanya kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kabula.

T A A R I F A

MHE. KABULA E. SHITOBELO: Mheshimiwa Spika, ahsante napenda tu kumwambia kwamba tozo zinazoongelewa ni zile ambazo hazitaathiri mapato ya Serikali. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Stella Manyanya, unaipokea Taarifa hiyo?

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, naomba nisimjibu.

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba, kimsingi tozo zote ambazo zipo kwenye mafuta ziliwekwa kwa sababu na ndio maana tunaona kwamba namna ya kusaidia watu waweze kuendelea na mfumo ule wa kupata maendeleo tuliyojipangia, lakini pia kuhakikisha hatukwami. Kuna kupunguza matumizi yasiyo ya lazima hiyo ndio ambalo naungana nalo. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Manyanya, kuna taarifa nyingine kutoka kwa Mheshimiwa Khadija Taya.

T A A R I F A

MHE. KHADIJA S. TAYA: Mheshimiwa Spika, nataka nimpe taarifa mzungumzaji kwamba, leo mabasi ya Shabiby yameongeza bei kutoka VIP shilingi 35,000 mpaka shilingi 45,000 na mabasi yale ya kawaida shilingi 22,000 ni shilingi 28,000, kwa hiyo hali ni mbaya Waheshimiwa. (Makofi)

SPIKA: Sasa ngoja, ngoja, kabla sijaleta hiyo taarifa ili uipokee au hapana hayo mabasi yametajwa mahususi, lakini nadhani bei za mabasi zimetangazwa kwa mabasi yote. Kwa hiyo, tusije tukajikuta hapa kwamba tunazungumzia kampuni moja kana kwamba kampuni nyingine bei ziko kawaida. Bei mabasi yote yametangazwa na chombo chetu cha Serikali kinachoangalia bei za vyombo vya usafiri. Kwa hiyo tusije tukajikuta kwamba tunazungumzia kampuni moja hapa ya mabasi, mabasi yote yametangaziwa bei mpya. Mheshimiwa Stella Manyanya. (Makofi)

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunisaidia eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, ninachosisitiza ni nini, tupo katika vita vya kiuchumi na jambo hilo la vita vilivyotokea huko kulikotokea duniani kuna wengine wananufaika humo humo kwa wao sasa kuwa ma-supplier wa mafuta katika nchi nyingine. Matokeo yake tunazuiliwa mafuta yasitoke maeneo fulani au vikwazo vinawekwa sehemu nyingine, lakini kuna wengine ambao wananufaika na mfumo huo kwa sasa hivi. Hilo suala pia liko kidunia na dunia tunaomba ituelewe sisi tupo katika kukuza uchumi wetu sasa hivi, wenzetu wameshatangulia, lakini kila vikwazo vinavyowekwa vinaumiza nchi hizi ambazo zinaendelea sasa hivi. Kwa hiyo, lazima tutupie na jicho huko kwa hiyo mimi nasema kwa ujumla wake dunia hii kwa sababu tunaongea live inatusikia tunaumizwa katika nchi zinazoendelea. (Makofi)

MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja, lakini iko haja ya kufuatilia kwa karibu kuona kwamba bei za bidhaa mbalimbali zinasimamiwa vizuri na mafuta tutafute fedha itakayopatikana kupitia vyanzo vingine, lakini tozo za msingi…

SPIKA: Sasa kwa sababu unaendelea kuongea basi Mheshimiwa Ighondo, Taarifa. (Makofi/Kicheko)

T A A R I F A

MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Nilitaka kumpa taarifa mzungumzaji kwamba, pamoja na sababu za kidunia, lakini sisi tunazungumzia dharura iliyopo mbele yetu kama Taifa kwa sababu zetu za ndani tuchukue hatua za makusudi hasa kwenye tozo ambazo sio za lazima, ambazo haziwezi kuathiri masuala yetu ya maendeleo ili kunusuru uchumi wetu pamoja na kushusha hali ya maisha kwa wananchi wetu. (Makofi)

SPIKA: Haya Mheshimiwa Stella Manyanya unaipokea taarifa hiyo?

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, hii siipokei kabisa, kwa sababu tumefahamishwa kwamba changamoto mojawapo inayosababisha haya tuliyofikia ni hivyo vita vilivyoko huko kwenye mataifa. Kwa hiyo lazima tu-deal na sababu zinazosababisha, kwa hiyo pamoja na hayo ya kupunguza, haya ni matokeo ya athari zinazoendelea huko duniani. Tunasema kwamba hao wanaoweka hivyo vikwazo, hao wanaosema hili lisifanyike wakati wenyewe pia wanafanikisha kupeleka bidhaa zao maeneo mengine wanatuua nchi zinazoendelea. (Makofi)