Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

Hon. Kavejuru Eliadory Felix

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii, kwanza nichukue nafasi ya pekee kumpongeza Waziri na Naibu wake kwa kazi kubwa wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mchango wangu nataka kuzungumzia juu ya upungufu wa mafuta ya kula. Kwanza nimpongeze Waziri Mkuu wa hamasa kubwa ambayo ameitoa katika Mkoa wa Kigoma hasa kwenye kilimo cha michikichi. Michikichi sasa hivi inalimwa katika Wilaya za Kakonko, Kibondo, Kasulu, Buhigwe, Kigoma na Uvinza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wameitikia kilimo hiki kinaenda kuondoa uhaba wa mafuta ya kula nchini, kinachohitajika kwa Wizara hii ya Viwanda na Biashara ni kusaidia hawa wakulima kuhakikisha kwa haraka sana kwasababu wameitikia na wamelima mashamba makubwa sana kuhakikisha wanatengeneza mazingira mazuri ya kuleta viwanda vya kuchakata mawese Kigoma. Wakileta viwanda vikubwa ambavyo vitakamua mawese pamoja na bidhaa nyingine zinazotokana na michikichi uchumi wa Kigoma utabadilika na uchumi wa nchi nao utabadilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze SIDO wanao mchango kwa wakulima wa michikichi, wanatoa mashine ndogo ndogo za kukamua mawese, wanatoa mikopo midogo midogo kwa wajasiriamali wanaojishughulisha na ukamuaji wa mawese, lakini shida ni moja tu riba ambayo wanaitoa kwa vikundi hivyo vya wajasiriamali ni kubwa. Mikopo hiyo ina riba ya zaidi ya asilimia 18 hadi 21; riba hiyo ni kubwa kwa wakulima, haiwezi kuleta tija kwenye makundi ya wajasiriamali.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaiomba Serikali kwa dhati kabisa ili kuharakisha na kuondoa upungufu wa mafuta ya kula nchini cha kwanza Kigoma tuhakikishe vinaletwa viwanda vitakavyokamua michikichi ili tupate mafuta ya kula. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili Kigoma ina mazao mbalimbali, tuna zao lingine ambalo tumelishahau ni zao la mihogo ambayo inalimwa katika Wilaya zote za Kigoma, wakulima wa Kigoma wanavuna mihogo haina soko.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakulima wa Kigoma wanaiomba Wizara ya Viwanda kupitia TANTRADE mtuhakikishie, mfanye jitihada za kututafutia soko la mihogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zao lingine ambalo tunahitaji msaada mkubwa sana kwa TANTRADE kututafutia soko ni tangawizi, takribani sasa Wilaya yote ya Buhigwe inalima tangawizi. Zao hili ni zao ambalo nalo ikiwezekana likawekwe kuwa zao la kimkakati. Tunaomba TANTRADE na Wizara ya Viwanda ihakikishe, itusaidie watu wa Kigoma kutuletea kiwanda cha kuchakata tangawizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu nyingine naenda kuchangia ni kwenye biashara. Miaka ya nyuma Mkoa wa Kigoma ulikuwa ni mashuhuri sana kwenye biashara, lakini sasa hivi biashara zimedumaa. Hii imetokea ni baada ya meli ambazo tulikuwa tunazitegemea katika Ziwa Tanganyika ambazo zilikuwa zikisafirisha bidhaa na wafanyabiashara kwenda Congo, kwenda Burundi, kwenda Zambia, meli hizi ni Liemba na Mwongozo zilikwishaharibika ziko grounded. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Serikali meli hizi zitengenezwe ili kuwepo kwa biashara na majirani. Mkoa wetu wa Kigoma ndio mkoa ambao unapakana na nchi karibu tatu ambazo Mashariki yake kuna idadi kubwa ya watu lile ni soko, tunaomba Wizara ya Viwanda itengeneze mazingira na kuhakikisha inaleta wawekezaji waweke viwanda katika Mkoa wetu wa Kigoma ili uchumi wetu uinuke sambamba na wa nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)