Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi, lakini vilevile niishukuru Serikali kwa kutusikiliza sisi Wabunge kwa sababu tunayoyasema ndio ambayo wananchi wetu wametutuma.

Ningependa nianze kwa kuchangia Wizara hii kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Viwanda amewasilisha bajeti nzuri sana. Nilikuwa naisoma hapa naifuatilia naona bajeti iko vizuri, ila nimuombe tu Mheshimiwa Waziri, Wizara yake iongeze kasi katika kusimamia bei ya bidhaa, mfumuko wa bei. Nimeona una mikakati mizuri, naomba sana uweze kusimamia ili wananchi waweze kupungukiwa na hizi changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano jana nilikuwa nazungumza na Mwenyekiti wa Kijiji cha Mbongo kilichopo Kata ya Manda, Wilaya ya Ludewa, alinipa bei ya vitu vichache sana na alisema atafurahi sana akiona nimekutajia. Alitaja bei ya sukari, mwaka jana ilikuwa shilingi 2,500 kwa kilo sasa ni shilingi 3,500; sabuni ilikuwa shilingi 2,000 leo ni shilingi 4,000 kwa mche mmoja; chumvi ilikuwa shilingi 500 sasa shilingi 700; mafuta ya kula yalikuwa shilingi 7,000 kwa lita sasa ni shilingi 16,000; petroli ilikuwa shilingi 2,500 sasa shilingi 4,000; nondo ilikuwa milimita kumi na mbili shilingi 22,000 leo shilingi 28,000 na mabati hizi ni bidhaa ambazo wananchi walikuwa wananitajia, pamoja na mbolea ambayo ilitoka shilingi 50,000 mpaka shilingi 150,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana Serikali iongeze kasi ya kufuatilia hizi sababu ambazo Mheshimiwa Waziri ameziainisha kwenye bajeti yake. Sababu nyingi tunazozitoa zimekaa kitaalamu sana, zimekaa kisomi sana, wale wananchi kule Ligumbiro wanapata taabu sana kutuelewa. Unavyomueleza chumvi imepanda bei kwa sababu ya vita anashindwa kuelewa, unavyomueleza sabuni imepanda bei, wananchi hawatuelewi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilisali misa ya Pasaka pale Ludewa wananchi walilalamika sana. Nimejaribu kujieleza mpaka nalia na machozi hawanielewi kabisa.

Kwa hiyo, naomba Wizara hii ijitahidi sana kufanyia kazi pamoja na mapendekezo ya Wabunge wengine ili wananchi waweze bkufurahia maisha kwenye nchi yao, lakini nina imani kubwa Mheshimiwa Waziri kwa wepesi wako, kwa umahiri wako hili linawezekana kwako, kwa hiyo, natarajia kuona mabadiliko na wananchi watafurahi. Na kwa kweli nikuhakikishie wananchi wa Ludewa hawana shida wakiona mambo yanakwenda vizuri wataendelea kuiunga mkono Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ningependa nizungumzie huu Mradi wa Mchuchuma na Liganga. Nimesoma kwenye ripoti mwaka jana ilikuwa kwamba majadiliano yanaendelea na sasahivi majadiliano yanaendelea. Pamoja na hii niipongeze Kamati ya Viwanda na Biashara ambayo iko chini ya Mheshimiwa Kihenzile, niliweza kushiriki kikao chao walivyojadili huu mradi, niliona kwa kweli Serikali ina mkakati mzuri, sasa naomba kwa kweli hili jambo limezungumzwa mno, kwa hiyo, hata wananchi tunavyowaeleza wanajua tunawapiga kamba tu, tunawadanganya. Kwa hiyo, naomba kwa kweli mambo yaanze kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano huu mradi ulipitishwa na Waraka wa Baraza la Mawaziri mwaka 1996 kwa Waraka Namba 06/96 kwamba mradi uanze. Ilivyofika mwaka mwaka 2011 mkataba ulisainiwa ubia kati ya NDC na Kampuni ya Tanzania China International Mineral Resources Limited. Kwa hiyo, toka mwaka 2011 uthamini ukaja kufanyika mwaka 2015 kwa nia ya kulipa fidia eneo la wananchi wale wa makaa ya mawe pale Nkomang’ombe, lakini na huku kwenye chuma cha Liganga huku Mundindi. Sasa toka mwaka 2015 mpaka sasa ni miaka saba/nane imepita, kwa kweli wananchi wamepoteza matumaini ila nimesoma kwenye bajeti yako kwamba umetenga fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, ila ningependa sana kuishauri Serikali lile wazo la kwenda kurudia kufanya uthamini, Serikali isilipe kipaumbele sana kwa sababu gani; mwananchi akishapewa ile fomu namba 69 kwamba sasa eneo lako tunalifanyia uthamini, hupaswi kubadili chochote, hupaswi kuondoa chochote.

Kwa hiyo, wananchi w akule walitii Serikali, ukisema uende leo ukafanye uthamini upya ile itawaumiza sana wananchi, pale jambo la kwenda kuangalia ni thamani ya ardhi inaweza kuwa imeongezeka kidogo, lakini mambo mengine wananchi kule walitii sheria walivyozuiwa kufanya chochote wale wananchi wa Nkomang’ombe na Mundindi hawakufanya chochote.

Mheshimiwa Naibu Spika, na hata hii sheria ambayo inasema kwamba maisha ya jedwali la uthamini ni miaka miwili ni Sheria ya Uthamini na Usajili wa Thamini Namba 7 ya mwaka 2016. Sasa hawa wananchi walitumia ile Sheria ya Ardhi ya Vijiji ndio iliyotumika kuwafanyia uthamini ya mwaka 1999 sasa hii imekuja baadaye na ni msingi wa haki na sheria duniani kote kwamba sheria inayotungwa leo haiwezi kunyang’anya haki zilizotolewa jana. Kwa hiyo, wale wananchi walielezwa kwamba watalipwa fidia pamoja na riba kwa kila muda unaochelewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ningeshauri Serikali iweze kwenda kuwasikiliza wananchi wale na kuwalipa....

(Hapa kengele ililia kushiria kwisha muda wa Mzungumzaji)