Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kwanza ya kuchangia Wizara hii ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji katika bajeti yake ya mwaka 2022/2023.

Kwanza napenda nimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutengeneza mazingira mazuri kwa wafanyabiashara wa Tanzania na hatimaye kuongezeka kwa mapato ya Serikali kwa kutumia TRA. Hii ni juhudi binafsi ya kuitangaza nchi yetu, kuongeza watalii pamoja na kuwezesha wafanyabiashara kulipa kodi bila ya kuwa na kinyongo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili niwashukuru sana Mawaziri wetu; Waziri pamoja na Naibu wake wamejitahidi kuweza kutatua changamoto mbalimbali wanazokutana nazo wafanyabiashara ili kuhakikisha biashara inakwenda vizuri katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika mchango wa leo mimi nitaongelea mambo matatu; la kwanza litakuwa ni Mfumo wa Stakabadhi Ghalani na changamoto zake inazokutana nazo kutokana na bajeti finyu wanayopewa hawa wenzetu wa Mfumo wa Stakabadhi Ghalani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mfumo wa Stakabadhi Ghalani upo kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge hili kwa mazao yote ya kibiashara. Tunashukuru tulivyoanza mfumo tulikuja na changamoto nyingi, lakini tunaendea kadri tunavyokwenda kupunguza changamoto hizi na bahati nzuri kwenye mfumo wa korosho ndiyo ulioanza basi mfumo unaendelea vizuri ingawa kuna changamoto nyingi. Lakini moja ya changamoto inatokana na bajeti; bajeti inayopewa Bodi ya Leseni za Maghala haikidhi haja ya kuendeleza Mfumo wa Stakabadhi Ghalani nchini, kwa sababu fedha wanayopewa na eneo wanalolifanyia kazi ni kubwa kuliko kiasi ambacho cha pesa wanachopewa sambamba na hilo watumishi ni wachache sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili Mfumo wa Stakabadhi Ghalani uweze kwenda lazima unahitaji fedha ili wafanyakazi wa Bodi ya Leseni za Maghala watembelee maeneo yote ambayo mfumo huu unatumika. (Makofi)

Kwa hiyo, naiomba Serikali kwa bajeti ijayo waongeze fedha kwenye idara hii ili waweze kufanya kazi ya usimamizi wa Mfumo wa Stakabadhi Ghalani ipasavyo. Kwa sababu mwaka huu wametengewa shilingi 346,000,000 mfumo kwa sasa hivi unaendelezwa katika zao la korosho, kahawa, tumbaku, nadhani fedha hizi hazitoshi. Sambamba na hilo, mbele ya safari nadhani ni busara watumishi wasambazwe kila Wilaya kwenye Bodi hii ya Leseni za Maghala ili waweze kupata nafasi nzuri ya kusimamia Mfumo wa Stakabadhi Ghalani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na Mfumo wa Stakabadhi Ghalani kutekelezwa katika maeneo tofauti unachangamoto zake ambazo Serikali inatakiwa izifanyie kazi. Moja ya changamoto ni kuchelewa kwa malipo kwa wakulima, hili jambo linakatisha tamaa sana wakulima na kuonekana mfumo huu hauna faida kwao. Mtu anakusanya mazao leo anakaa mwezi mzima hajapata fedha yake, hili jambo linatia doa pamoja na kuuza kwa bei nzuri, lakini kuna kuwa na hisia kwamba kuna mchezo unaochezwa kwa sababu fedha yao inacheleweshwa kwa ajili ya malipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kutatua hizi changamoto, naiomba Serikali kupitia Bodi ya Leseni za Maghala basi watafute namna na kupata maghala kwenye vijiji vyetu ili kupunguza gharama za kusafirisha mazao, ili kupunguza gharama za kuwalipa Wajumbe wa Bodi wanaosindikiza mazao kwenye maghala makuu. Jambo hili litafanya wakulima wapate faida zaidi kwa sababu gharama ya kusafirisha mazao itapungua, gharama ya watumishi wanaosindikiza mazao itapungua.

Ninaomba sana kwenye suala la maghala kwenye vijiji vyetu ni muhimu sana, ukitembelea huko vijijini maghala yanayotumika unaweza ukashangaa, wanatumia mpaka nyumba za watu binafsi, hazina floor, hazina umeme, kwa hiyo inasababisha ubora wa mazao ya wakulima unapungua na hatimaye na bei anayotoa mnunuzi inakuwa ni ndogo kwa sababu tumeshindwa kuyatunza na upotevu wa mazao unakuwa ni mkubwa kitu ambacho kinasababisha unyaufu ambao unaosababisha mkulima akose fedha yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sana kwa kutumia wataalam wetu, tuandike maandiko, tupate maghala kwenye vijiji huko kwa sababu sheria inaruhusu kwamba ghala linaloweza kuhifadhi korosho au mazao yoyote kuanzia tani 200 linaweza kuingia kwenye Mfumo wa Stakabadhi Ghalani. Tunaomba kuanzia sasa tu-focus kwa namna ya kutatua tatizo la maghala kwenye vijiji vyetu ili kupunguza gharama za uendeshaji katika Mfumo wa Stakabadhi Ghalani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kwenye gharama za uendeshaji wa Mfumo wa Stakabadhi Ghalani; nashukuru Serikali inatoa dira, tozo zote lakini matumizi ya tozo hizi hazielekezwi au hazielezwi kwa wananchi waliochangia hizi gharama. Kwa mfano, kwenye korosho kuna tozo 25 ya Bodi ya Korosho, kuna tozo ya Naliendele, inavyotumika wananchi kupitia vyama vyao vya msingi au mikutano yao hawaambiwi kwamba fedha hii imetumika kiasi fulani. Vilevile kwenye tozo za Halmashauri zetu wananchi hawaambiwi, kwa sababu tozo hizi zinatokana na Mfumo wa Stakabadhi Ghalani wanapaswa waambiwe kwa mfano, kule Tunduru tuna timu yetu ya korosho, Tunduru Korosho inachangiwa na tozo za wakulima kutokana na wadau wa zao la korosho. Lakini tangu imeanzishwa tozo ile Mfuko ule unachangiwa tu hakuna mahesabu, hakuna chochote, jambo ambalo wananchi wanalalamika kwamba fedha hii badala ya kuhudumia kama ilivyotakiwa inatumika tofauti. (Makofi)

Naomba sana hizi tozo ambazo tunaziweka kwenye Halmashauri zetu, zinawekwa na Serikali basi tozo zile zilete mrejesho wa makusanyo na matumizi kwa wananchi wa wanaohusika ili malalamiko yaweze kupungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana hili jambo liwe mfano kwa sababu zinakusanywa kwa mujibu wa taratibu, kutumia vyama vyetu vya msingi, viongozi wetu wa vyama vikuu basi ni vizuri kuwa jambo hili walifanyie kazi kuhakikisha kwamba mapato na matumizi ya hizi tozo ambazo zinatumika kwenye Halmashauri zetu...

(Hapa kengele ililia kushiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)