Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza Waziri wa Madini Dkt. Doto Biteko na Naibu wake Dkt. Stephen Kiruswa na watendaji wote wa Serikali kwa kazi nzuri wanazofanya kwenye sekta ya madini na mimi nitachangia kwenye changamoto za wachimbaji wadogo wadogo wa madini ya Tanzanite nchini.

Mheshimiwa Spika, sekta ya madini ni moja ya sekta kubwa nchini inayoinua uchumi wa nchi. Tanzanite ni kati ya madini yanayolipatia Taifa pesa za kigeni na kuliingizia Taifa kipato. Madini ya Tanzanite hupatikana nchini Tanzania tu.

Mheshimiwa Spika, wachimbaji wa kigeni wamefanikiwa sana kunufaika na rasilimali hii ya Taifa letu. Kampuni ya nje ya Tanzanite One ni moja ya kampuni iliyofanikiwa kwa kuwa na vifaa vyenye ubora kwa wachimbaji wake.

Mheshimiwa Spika, wachimbaji wadogo wadogo wa Tanzanite wanakabiliwa na changamoto mbalimbali kubwa ambazo Serikali inapaswa kuzitatua ili kuwanufaisha na rasilimali hii ya Taifa lao.

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa inayowasumbua wachimbaji wadogo wadogo wa madini ya Tanzanite ni matumizi ya teknolojia za kizamani, upatikanaji wa zana za kisasa za uchimbaji na mitaji midogo kwa kundi hili.

Mheshimiwa Spika, bei ya zana za uchimbani ni kubwa na vilevile hutozwa kodi kubwa. Hapa nchini Tanzania ni wafanyabiashara wachache wanajihusisha na biashara ya zana za uchimbaji kama vile vifaa vya kuchoronga miamba, vilipuzi miamba na kadhalika kutokana na kodi nyingi kwenye bidhaa hizi. Kwa hali ilivyo sasa hivi, vifaa hivi vikiingizwa nchini wachimbaji wadogo hushindwa kumudu gharama.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto nilizotaja hapo juu, naishauri Serikali yafuatayo; kwanza Wizara ya Madini kwa kushirikiana na Waziri wa Fedha washauriane na kuondoa kodi kwa wazawa wanaoagiza na kufanya biashara ya vifaa ili viingie kwa wingi, madini yachimbwe na wengi na kodi iongezeke kutoka kwenye mauzo ya Tanzanite badala ya ile ya kwenye vifaa.

Pili, Wizara ijadiliane na benki za biashara nchini ili zitoe mikopo ya mitaji na ya kununulia vifaa vya kuchimba Tanzanite kwa wachimbaji wadogo wadogo.

Tatu, Serikali kupitia taasisi zake iwasaidie wachimbaji wadogo wadogo wa Tanzanite kupata wataalamu na teknolojia za kisasa za kuchimba madini.

Mheshimiwa Spika, nne, Serikali ifanye tafiti za kina katika maeneo ya Mererani ili kujua maeneo yenye madini na kujua yapo umbali gani ili kurahisisha uchimbaji kwa wachimbaji wadogo wadogo. Kwa kufanya hivi, itarahisisha uwekezaji na uchimbani na kuipatia Serikali kipato cha uhakika.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.