Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini

Hon. Neema Kichiki Lugangira

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo kwa mara zote amekuwa akiibeba agenda la local content na akiendelea kusisitiza umuhimu wa kuongeza na kuimarisha ushiriki wa Watanzania kwenye sekta hizi za uziduaji ikiwemo na sekta ya madini.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu nitajielekeza kwenye ule mradi wa Kabanga Nickel uliopo Wilayani Ngara Mkoani Kagera, hapa napenda nitambue jitihada kubwa sana za Mhashamu Baba Askofu Niwemugizi pamoja na Mbunge wa Jimbo la Ngara Kaka yangu Mheshimiwa Ndaisaba wamejitahidi sana kulisemea suala hili kwamba kwenye mradi huu wa Kabanga Nickel yanachimbwa yale madini lakini yatasafirishwa na kufanyiwa uchenjuaji Kahama, jambo ambalo tukirudi kwenye misingi ya local content itafifisha namna ambavyo wananchi wa Ngara na Mkoa mzima wa Kagera kwa ujumla watakavyonufaika na mradi huu wa Kabanga Nickel. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa lugha nyingine ni kwamba Mkoa wa Kagera na Wilaya ya Ngara yatabaki mashimo wakati fursa zote ambazo ndiyo nyingi za wananchi wa Ngara na wananchi wa Kagera kwa ujumla kuweza kushiriki zitahamishiwa Wilayani Kahama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo ningependa kupata maelezo ya kina kutoka kwa Serikali kwanini wameamua kwenda kinyume na ambavyo inatakiwa kwamba katika mnyororo wa mradi, mnyororo mzima wa mradi unatakiwa ufanyike katika eneo la mradi. Kwanini katika mradi huu wa Kabanga Nickel Serikali imeamua kuchimba Wilayani Ngara ambako mradi ndiyo upo na madini ndiko yalipo lakini kuwekeza refinery Wilaya ya Kahama Mkoa wa Shinyanga.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hilo litafifisha ushiriki wa wananchi wa Ngara, litafifisha ushiriki wa wananchi wa Kagera, litafifisha fursa za wanawake, vijana na jamii nzima ya Mkoa wa Kagera. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili wote tunafahamu kwamba kuna kitu kinachoitwa service levy asilimia 0.3, hii service levy itakuwa inakwenda Kahama, sasa Je, Ngara watanufaika vipi na hii asilimia 0.3 ya service levy. Kwa hiyo, naomba nipate maelezo ya kuridhisha kutoka kwa Serikali kwanza kwanini wameamua kutowezeka refinery ifanyike pale pale Ngara. Pili, tutakapokuwa tunabeba haya madini na kuyasafirisha mpaka Kahama ni hasara gani ambayo itatokea katika uharibufu wa barabara zetu. Tatu, wananchi wa Ngara watanufaika vipi kutoka kwenye ile similia 0.3 ya service levy ambayo sasa italipwa Kahama.

Mheshimiwa Spika, labda Serikali ije na mpango madhubuti wa kuhakikisha kwamba Wilaya ya Ngara itapata asilimia fulani kutoka kwenye ile asilimia 0.3 ya service levy. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo mimi nisiporidhika na majibu ya Serikali nitashika Shilingi ya mshahara wa Waziri. Ahsante. (Makofi)