Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Salum Mohammed Shaafi

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Chonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

MHE. SALUM MOHAMMED SHAAFI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Moja kwa moja naomba niende katika hoja ambayo iko mezani kwetu. Huu ni mwaka wa 58 wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. Kihistoria muungano huu ulikuwa ni baina ya nchi mbili huru; Nchi ya Tanganyika na Nchi ya Zanzibar, lakini nchi zote hizi zilikuwa ni Wanachama wa Umoja wa Mataifa.

Mheshimiwa Spika, wakati tunaungana tulikubaliana mambo 11. Katika mambo haya naomba nisiyaseme, lakini yako mambo ambayo si ya Muungano lakini Zanzibar imekosa nafasi kama ni sehemu ya Muungano huu wa Tanganyika na Zanzibar. Naomba niseme masuala ya michezo siyo sehemu ya Muungano, masuala ya afya siyo sehemu ya Muungano, lakini leo yapo mambo tumeambiwa yamepatiwa ufumbuzi, yako mambo ambayo tumeambiwa haya tayari tumeyapatia ufumbuzi na sasa hatuwezi kuyajadili tena badala yake tunaenda katika utekelezaji wake.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, masuala ya Afrika Mashariki, masuala ya kikanda pamoja na kimataifa. Leo Zanzibar tuna ZFF Tanganyika tuna TFF lakini TFF inabeba nembo ya Muungano ambayo sasa inakuwa ni member wa FIFA na inaleta misaada TFF. Je, naomba kujua Mheshimiwa Waziri atakapokuja, tunafahamu mgao ambao unatoa FIFA Zanzibar tunakuwa ni sehemu ya manufaiko katika mgao huo?

Mheshimiwa Spika, naomba niseme ukienda katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano kuna mahali, kuna sehemu imetutaka kwa mujibu wa makubaliano yetu tutakuwa na account ya pamoja na fedha. Katika wasilisho la Mheshimiwa Waziri amesema haya ni mambo ambayo sasa tunaendelea kuyashughulikia. Sasa ni mwaka wa 58, bado tunaendelea kushughulikia matatizo yale yale, kitu ambacho kwa Wazanzibar hatuoni kwamba sasa kuna nia na dhamira njema katika Muungano huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niseme wazi, hakuna mtu ambaye hautaki Muungano huu, sote tunautaka, lakini tunataka Muungano wa haki na tunataka Muungano wa usawa. Naomba sasa ufike muda Serikali ituambie ni lini Akaunti ya Pamoja ya Fedha itafunguliwa, itaanzishwa? Kwa sababu zimekuwa ni danadana za muda mrefu na sasa tumefika mahali tunaona kwamba Muungano huu ni jambo ambalo linatunyonya Wazanzibar. Tufike mahali kinia safi tu tuseme yapo mambo ambayo tuseme, haya tuyatatue kwa maslahi ya Taifa letu hili la Tanzania.

Mheshimiwa Spika, mwisho, nataka nitoe rai na naomba Mheshimiwa Waziri akija hapa ifike mahali atuambie sasa ni lini Serikali ya Jamhuri ya Muungano itakuwa na nia ya dhati kuulinda Muungano huu kwa kufungua akaunti hii ya pamoja.

Mheshimiwa Spika, la pili, nimwombe Mheshimiwa Waziri na niiombe Serikali sasa ituambie ni lini Serikali ya Jamhuri ya Muungano itaipatia Zanzibar…

SPIKA: Mheshimiwa Salum kuna taarifa.

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, (SERA, BUNGE NA URATIBU): Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa mzungumzaji anayezungumza kwamba Muungano wetu una manufaa makubwa kushinda changamoto. Kwa hiyo analipotosha Bunge na Watanzania kusema kwamba muungano unawanyonya, ziko faida nyingi za Muungano ambazo tunazo hata kuwepo hata ndani ya Bunge hili ni faida za Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.

SPIKA: Mheshimiwa Salum Shaafi, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. SALUM MOHAMMED SHAAFI: Mheshimiwa Spika, siipokei na sina haja nayo. Hakuna mimi sijasema naukataa wala naupinga, bali uhalisia ulivyo hakuna asiyejua kama Muungano huu una changamoto nyingi hususan kwa upande wa Zanzibar. Hili ni jambo ambalo naomba litambulike kwa sababu katika lile jambo ambalo kwamba Zanzibar ni sehemu ya Afrika Mashariki leo tunachagua Wabunge wa Afrika Mashariki, Zanzibar…

(Hapa kuengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji )

SPIKA: Mheshimiwa Shafi muda wako ulikuwa umeshaisha nilikuwa nimekupa muda ili umalizie hoja yako.

MHE. SALUM MOHAMMED SHAAFI: Ilishapigwa kengele.

SPIKA: Kengele ilishagonga.

MHE. SALUM MOHAMMED SHAAFI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)