Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora na Naibu wake pamoja na watendaji wa Serikali katika Wizara hii kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajikita kwenye; kwanza umuhimu wa Serikali kuanzisha mfuko maalumu wa pension kwa sekta isiyo rasmi ya wakulima, wafugaji na wavuvi; pili umuhimu wa Serikali kupitia upya sheria inayowafanya maprofesa kustaafu wakiwa na miaka 65 na kutokupata mikataba maalumu ya kuendelea kufundisha; na tatu, wakuu wa idara na taasisi mbalimbali kukataa kupitisha barua za watumishi wanaoomba kuhamishwa kutoka vituo vyao vya kazi kwa sababu maalum.

Mheshimiwa Mwenyekiti, karibu asilimia 65 ya Watanzania wako kwenye sekta za uzalishaji za kilimo, mifugo na uvuvi. Kundi hili huishi maisha ya shida sana wanapofikia uzee na kukosa nguvu za kuendelea kujipatia kipato. Kwa kuwa watu hawa wako kwenye mifumo ya uzalishaji na hujipatia kipato, ni vyema Serikali ikafikiria namna ya kuanzisha mfuko maalum wa pension ukisaidiwa na makato maalum kutoka kwenye mauzo ya mazao kwa makundi haya ili yaingie kwenye mfuko wao maalum wa pension.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili likiratibiwa vyema litakuja kusaidia makundi haya katika maisha yao ya uzeeni watakapokuwa hawana tena nguvu ya kufanya kazi na kujipatia kipato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pendekezo hili likifanikiwa na likisimamiwa vizuri, huko mbele ya safari wazee wetu waliostaafu katika kazi za kilimo, ufugaji na uvuvi hawatakuwa tegemezi wala ombaomba kwenye jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vyuo vyetu vikuu vya Serikali, kuna changamoto kubwa ya tatizo la rasilimali watu likiwa limesababishwa kwa kiasi kikubwa na kitendo cha Serikali kubadilisha utaratibu wa maprofesa kuendelea kufundisha kwa mikataba maalum hadi wanapofikisha umri wa miaka 70.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kwa miaka michache iliyopita, zaidi ya maprofesa 91 waliondoka katika Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine kati ya Januari, 2016 na Desemba, 2020; maprofesa 111 waliondoka kwenye utumishi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Katika Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, hakuna profesa hata mmoja wa somo la hisabati tangu aliyekuwepo alipoondoka, hapajakuwepo na mrithi wa kusaidia kusimamia research za mahesabu katika ngazi ya uzamivu. Hata kwenye soko la ajira si rahisi kuwapata wataalam wenye vipaji hivi na vyuo vyote vya Serikali nchini vinakabiliana na changamoto kama hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya rasilimali watu vyuo vikuu Tanzania inasababishwa pia na masharti magumu ya kuajiri wataalam kutoka nje ya Tanzania. Kuajiri wataalam kutoka nje kwenye maeneo ya kimkakati ni muhimu ili kutusaidia kwenye kukuza rasilimali yetu, na kutuunganisha na mifumo ya kimataifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upatikanaji wa vibali huchukua muda mrefu na husababisha walengwa kutoka nje kubadili mawazo na kuacha kuja kufanya kazi Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imejitokeza tabia ya wakuu wa idara na taasisi mbalimbali za Serikali kukataa kupitisha barua za watumishi wanaoomba kuhama na kwenda kufanya kazi kwenye sehemu tofauti kwa manufaa ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni haki ya mtumishi kuomba kuhama na kwenda kulihudumia Taifa sehemu yoyote hapa nchini anapoona ataongeza tija na maendeleo ya Taifa. Uamuzi wa mwisho wa kutoa ruhusa ya kuhama hutolewa na Katibu Mkuu - Utumishi na Utawala Bora. Wajibu wa mkuu wa idara au taasisi ni kupitisha barua ikiwa na mapendekezo yake na si kuzuia barua isifike ngazi za juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuelezea changamoto za hapo juu, naishauri Wizara yafuatayo;

kwanza Serikali ianzishe mfuko maalum wa pension kwa sekta zisizo rasmi za wakulima, wafugaji na wavuvi.

Pili, Wizara ya Utumishi na Utawala Bora itoe vibali vya kuajiri wanataaluma wa kutosha kuendana na idadi ya wanafunzi wanaodahiliwa. Hii ni pamoja na kuajiri wataalam kutoka nje katika maeneo ya kimkakati kama yale ya sayansi, uhandisi na hesabu.

Tatu, Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora wapitie sheria na kuongeza umri wa maprofesa kutumika kwa mikataba uanzie pale wanapostaafu wakiwa na miaka 65 na waendelee hadi wanapofikisha umri wa miaka 75. Hii haina hasara kwa Serikali kwani wanapostaafu mishahara yao inakuwa bado iko kwenye ikama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwaandaa hawa wataalam, Serikali hutumia gharama kubwa sana. Tunapositisha huduma zao, vyuo binafsi huwachukua bila gharama na kuwatumia kuwajengea sifa, ilihali vile vya Serikali vinadorora.

Nne, Waziri wa Utumishi na Utawala Bora atoe maelekezo kwa wakuu wa idara na taasisi za Serikali watende haki ya kupitisha barua za watumishi wanaoomba kuhama kwenye vituo vyao ili wampe fursa Katibu Mkuu mhusika kutoa uamuzi wa mwisho. Napendekeza watakaokaidi hili wachukuliwe hatua za kinidhamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.