Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Dr. Amandus Julius Chinguile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya uhai, lakini kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya kwa ajili ya kuboresha maisha ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Dada yangu Mheshimiwa Jenista Mhagama na Naibu Waziri, Mheshimiwa Deo Ndejembi, kwa kweli, wanafanya kazi nzuri. Na mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa, yako mambo mengi tumewashauri, lakini tumejadiliananao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye upungufu wa watumishi. Kwenye Jimbo langu la Nachingwea kwa mfano, kwenye elimu ya msingi mahitaji ni watumishi 1,319 waliopo ni 788, upungufu ni 531. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye elimu sekondari. Mahitaji ni 786, waliopo ni 412, mapungufu ni 374. Na afya vilevile nae neo la utawala kwa maana ya maafisa watendaji wa kijiji na wa kata. Eneo hili tulitolee macho kwa ukubwa wake na hasa maeneo haya ambayo ni mikoa ya mipakani, Lindi, Mtwara na maeneo mengine. Twendeni tuyape kipaumbele cha makusudi kabisa. Na hapa ndipo tunapokuja sasa kuona namna ambavyo wenzetu wanaoomba kwa mfumo huu wa mtandao akipangiwa kwenda Nachingwea anasema niko tayari, lakini akifika baada ya miezi mitatu, baada ya muda anasema sasa baba ni mzee kwelikweli, amezeeka baada ya mwaka mmoja? Haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, anachagua kwenda Nachingwea ni kwa sababu, nafasi iko Nachingwea, lakini akishapata check number basi anakumbuka sasa kumbe naweza nikaomba kwa sababu sheria ipo na inamruhusu yeye kuomba uhamisho baada ya muda fulani. Kwenye hili, mimi nishauri Serikali yangu, tuone namna ambavyo tutatoa kipaumbele kwa wale wenye sifa ya kufanya hizi kazi wanaotokea kwenye maeneo haya; na hii itatusaidia, wale vijana wako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii imejaliwa wasomi kwelikweli katika kila kata, kila wilaya, wasomi, ma-graduate ni wengi kwelikweli wapo. Ni Serikali tu kuweka utaratibu mzuri wa kuwatumia hawa ma-graduate ili tusipate upungufu huu kwa sababu ya watumishi wengine kuhama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwa wale makaimu. Nilitoa taarifa hapa kwa Mbunge mwenzangu, sasa naona nilielekeze hilo. Kwa mfano, Halmashauri yangu ya Wilaya ya Nachingwea ziko idara na vitengo vinne kuna makaimu, lakini kibaya zaidi yuko kaimu anakaimu zaidi ya miaka 11, hii haikubaliki. Sasa hapa utamleta sasa mtumishi ambaye wewe umeona ana sifa kutoka eneo lingine, huyu mtu nimesema hapa tunampa ugonjwa wa sonona, tunamsababishia pressure na magonjwa mengine yasiyoambukiza, hii si sawa. Na kama ni vetting tunamuacha miezi sita ya kisheria, anakwenda mwaka, anakwenda miaka miwili… (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mbunge ni vizuri hilo jina ulilosema anakaimu miaka 11 ukawapatia pia Mawaziri badae.

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nitafanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inapomletea sasa mkuu wa idara kutoka eneo jingine na yeye awe chini yake kwa kweli, unamuacha kwenye mazingira magumu sana huyu mtumishi. Hii si sawa na haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maelekezo yako nimeyapokea nitafanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni juu ya wastaafu, kuna suala la uhakiki. Hili ni kizungumkuti, kila mwaka wanakwenda kuhakikiwa mkoani; ni jambo jema kuhakiki kama wazima au la, lakini suala la kutoka huko vijijini waliko kwenda mkoani jambo hili ni gumu na hawa wastaafu walio wengi hali zao ni ngumu kwelikweli. Hapa Waheshimiwa Wabunge wenzangu wamesema… (Makofi)

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa, Mheshimiwa Kuchauka.

T A A R I F A

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nampa Taarifa muongeaji, hili suala la kwenda kuhakikiwa mkoani limekuwa ni janga kwelikweli. Mtu anatoka Kijiji kwa mfano Mpigamiti, kilometa zaidi ya 30, aje Liwale Mjini kilometa 50, atoke Liwale Mjini kwenda Lindi ambako ni kilometa 360. Huyo mstaafu huyo ana umri wa miaka 80 au mwingine ana miaka labda 75 hivi, unamtakia kweli maisha mema?

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mzigo huu. Kwa hiyo, nampa Taarifa anachikisema ni sahihi kabisa kwamba, huu mzigo tunaubeba sisi Wabunge. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa unapokea Taarifa?

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa mikono miwili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii si sawa na bahati nzuri hao wastaafu walio wengi wamechoka sana. Tuone namna ya kuwawekea mazingira rahisi sehemu ambayo ya kuhakiki, wanaweza kufanya kule Halmashauri, lakini pia tunaweza tukaboresha kwa namna nyingine ambayo tunaona inafaa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwenye hizi ajira mpya zinazotolewa, hili nalo ni tatizo lingine. Tatizo sio kupata ajira, tunajua na tunaiheshimu sana mamlaka, na kwakweli kubwa zaidi niipongeze Serikali kwenye eneo hili kwa kutoa hizo ajira. Kazi kubwa hiyo mmefanya tunawashukuru, lakini ni namna gani hawa vijana wanakwenda kupata hizi kazi? Ni kizungumkuti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na huu mfumo wa ajira kwa maana ya kuomba kwenye mtandao si Rafiki na hasa kwa wale vijana walioko vijijini. Huu mtandao una changamoto, unaweza ukakaa wiki nzima bado wewe unaendelea kuingia online na mtandao hausomi, badala yake hata muda wa kuomba hizo nafasi umeshapita. Tuone namna tutakavyowasaidia hawa vijana kweli wa Kitanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako Wabunge hapa wamesema ni vizuri sasa tukaona mgawanyo mzuri kwa kutumia wilaya, majimbo, namna tutakavyoona inafaa ili kila kijana Mtanzania aweze kunufaika na hizi ajira zinazotoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la mwisho, niwapongeze sana wenzetu wa TASAF na hasa kwenye ile miradi ambayo wameitekeleza, wanafanya kazi nzuri sana. Nimesema mimi ni mjumbe wa kamati na tumeona miradi mingi inapendeza kwelikweli; tumekwenda Zanzibar, kazi nzuri tumeiona. Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yako ya TASAF mimi nawapongeza sana. Kazi hii nzuri iendelee, lakini pia sasa mtolee macho na maeneo mengine ambayo hamjafika kwenye miradi ya kimkakati ikiwemo kule Nachingwea, Liwale, Rwangwa na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)