Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Ahmed Juma Ngwali

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ziwani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. AHMED JUMA NGWALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, sitaki nijihuzishe sana na mazungumzo yaliyopita, naomba nijielekeze kwenye hoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijachangia hoja hii niliamua kwanza nipitie Sheria ya Baraza la Michezo, Sheria Namba 12 ya mwaka 1967 ikafanyiwa marekebisho na Sheria Namba 6 ya mwaka 1971 pamoja na Kanuni za Michezo na Kanuni za Usajili Namba 442 ya mwaka 1999.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipitia hii sheria, ukistajabu ya Musa utayakuta ya Firauni, bahati nzuri sana Mwanasheria Mkuu yupo, lakini Waziri wa Sheria Mheshimiwa Mwakyembe pia yupo. Naomba ninukuu Kifungu cha12 cha Sheria ya Baraza la Michezo, Kifungu hicho kinachohusu usajili wa vilabu kinasema;
“Msajili atakataa kusajili au kutoa msamaha wa usajili kwa chama cha michezo, ikiwa (a) Ikiwa ameridhika kwamba chama hicho ni tawi la au; kimeshirikishwa au; kina uhusiano na shirika au kikundi chochote chenye mwelekeo wa kisiasa isipokuwa chama au chombo chochote cha Chama cha Afro-Shiraz cha Zanzibar au chombo chochote cha chama hicho.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, Afro-Shiraz ipo kwenye Sheria ya Baraza la Michezo, Chama cha Afro-Shiraz hakipo tena hata katika Katiba ya Zanzibar, hata katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini sheria hiyo tayari imeshafanyiwa marekebisho na bado Chama cha Afro-Shiraz kinaonekana baada ya miaka sijui mingapi kwa sababu ilikufa mwaka 1977.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepata maswali mengi ya kujiuliza kwanza, kwa nini iwe Afro-Shiraz isiwe TANU. Kwa hiyo, inaonekana kwamba Waziri hata alipochaguliwa kuwa Waziri hata hii sheria hakuipitia. Inaonekana Serikali haipitii sheria na kuangalia sheria ambazo zinatakiwa kufanyiwa marekebisho. Jambo la msingi Serikali pitieni sheria ni aibu. Leo tunakuta Afro-Shiraz katika Sheria ya Michezo, ASP. Baada ya kuweka sawa hilo, tuendelee sasa na soka, mimi ni mdau mkubwa wa soka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha sana, Tanzania leo unasimama hapa unazungumza, ni ya mwisho katika viwango vya FIFA katika mpira wa miguu katika East Africa ni ya mwisho. Ya kwanza ni Uganda, ambayo inashika nafasi ya 72, ya pili ni Rwanda ambayo inashika nafasi ya 87, ya tatu ni Kenya inayoshika nafasi ya 116, ya nne ni Burundi inayoshika nafasi ya 122, lakini Tanzania inashika nafasi ya 129. Tumewazidi kila kitu hizo nchi nyingine. Hizo ni takwimu ambazo ukitaka kuzidadavua nenda kwenye website ya FIFA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha sana kwa sisi watu wa michezo kuona leo Taifa kama Tanzania ndiyo Taifa la mwisho kabisa katika soka kwa East Africa. Ukubwa wa nchi, uchumi wetu, tunapitwa na Kenya tu kwenye uchumi, kwenye population, kwenye eneo tuko juu. Maana yake ni kwamba hakuna mkazo katika michezo hasa soka mchezo ambao unapendwa na watu wengi Tanzania hasa ukifanya tafiti. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine Wazungu wanasema one swallow does not make a summer. Inashangaza sana leo Mheshimiwa Nape, alikuja kwa mbwembwe sana na kumtangaza kama Mbwana Samatta ndiyo shujaa wa Tanzania katika mpira wa Kimataifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ni ya mwisho katika nchi zenye wachezaji wa wanaocheza Kimataifa. Tanzania ni ya mwisho, nataka nikupe takwimu. Tanzania ina wachezaji kumi tu nje ya nchi, Mheshimiwa Nape huwajui, nina hakika huwajui. Lakini Rwanda ina wachezaji 17 wanaocheza nje soka la kulipwa, Burundi wana wachezaji 25, Kenya wana wachezaji 32 wanaocheza nje na Uganda wana wachezaji 41. Watu wanajitahidi kadri siku zinavyokwenda kuwekeza katika mpira wa miguu, ndiko wanakotakiwa wawekeze kwa sababu mpira wa miguu, mfano chukua mchezaji mmoja tu, Victor Wanyama mchezaji wa Kenya anayecheza Southampton ya Uingereza analipwa kwa wiki pound 30,000 ni sawa na shilingi karibu milioni 300 kwa wiki moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mnakwenda kuwekeza kwenye boda boda, hii ni Serikali gani isiyokuwa na mipango mizuri bwana eeh? Mnakwenda kuwekeza kwenye boda boda Rais anasema mshahara mwisho shilingi milioni 15, kwa mwezi Yaya Touré wa hapo Ghana anapata zaidi ya bilioni tatu kwa mwezi.
Jambo lingine ambalo ni muhimu sana ni suala la mapato ya michezo. FIFA wanakuwa na Financial Assistance Program (FAP) wanatoa dola 250,000 lakini wana Goal Project ambazo wanatoa dola 400,000. Tanzania Football Federation inapotoka nje kuwakilisha nchi inawakilisha kama Tanzania ambapo Zanzibar nao wanahitaji kupata hizo fedha. Hakuna takwimu zozote zinazoonesha kwamba Zanzibar wanapata hizo fedha, lakini kuna vyama tofauti vya michezo kama International Basket Ball Federation (FIBA) wanaleta fedha ndani, Zanzibar hatupati, tuna International Boxing Association wanaleta fedha hazipatikani, kuna Internationa Golf Federation zinakuja fedha kutoka nje hatupati, kuna Internationa Handball Federation hatupati fedha, kuna sports association chungu nzima za nje, Zanzibar hatujui mambo haya yanakwenda vipi, wala mambo yanakuwa vipi yaani tupo tu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukichukuwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ukiisoma hii iko katika mambo ya Muungano, mambo ya nje ni mambo ya Muungano, kwa hivyo mnavyotoka International Zanzibar tupo. Zanzibar tukizungumza tayari unatoka nje tu ya nchi, tukiwa ndani fanyeni shughuli zenu za ndani lakini kwa nini mnapokwenda nje misaada ile ya kimichezo Zanzibar hatuioni au mnaipeleka wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Nape namalizia kwa kusema tunakwenda katika Olympic ya Rio de Janeiro 2016. Tanzania toka mwaka 1964 ina medali mbili tu za shaba, Kenya wana medali 86, wana medali 25 za dhahabu, kama haujaja na medali lazima ujiuzulu kwa sababu hatuwezi tena kuvumilia kuona kwamba Tanzania ndiyo imekuwa shamba la bibi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, siungi mkono hoja.