Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza, nianze kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa ajili ya yote. Pili, napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, kwa kazi kubwa anayofanya na tunamwombea afya njema ili aweze kuendelea kututumikia. Wakati huo huo, nawaombea Waheshimiwa Wabunge wenzangu na wananchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mengi yamezungumzwa, lakini kazi yetu sisi Wabunge tuliyopewa kwa mujibu wa Sheria na Katiba, ni kuwasemea wananchi kuwatetea na vile vile kuhakikisha kwamba tunakuwa na sheria nzuri zinazosaidia na mambo yote. Kwa misingi hiyo, kila mtu anapokuwa kwenye nafasi hii ya Ubunge lazima atimize wajibu huo kwa nguvu zake zote. Tunapozungumza, haijalishi jana nilikuwa nani au juzi nilikuwa nani? Leo mimi ni Mbunge, lazima niseme bila kuficha, ndiyo maana tunalindwa katika mazungumzo yote tunayosema humu Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitaanza kuzungumzia hali ambayo binafsi naiona siyo nzuri, inayoendelea katika mitandao mbalimbali. Mitandao naichukulia ni sehemu rasmi ya taarifa, kwa sababu sisi wenyewe tumeshasema kwamba hata ushahidi wa kimtandao unaweza ukatumika hata Mahakamani. Hiyo ni kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo, nasema nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hii hali ambayo inaendelea katika nchi yetu, nami kama mtu mzima ambaye Mwenyezi Mungu amenibariki nikaishi katika Awamu zote za Uongozi, nashangaa ninavyoona sasa hivi watu wanapenda kuendelea kutupiana maneno, wengine wakijaribu kuwasema viongozi waliopita, wengine wakijaribu kuwasema viongozi waliopo mambo mbalimbali, haileti afya kwa Taifa letu. Tuache. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Taifa hili lisingefika hapa leo bila uwepo wa wale viongozi waliopita. Taifa hili haliwezi kuendelea bila viongozi waliopo sasa. Kwa hiyo, badala ya sisi kushikamana kuangalia mbele tunakoenda, tunaendelea kupigana na tena wanaopigana wengine kuna chawa sijui wa watu wa zamani; kuna chawa wa watu wa sasa. Ukiangalia hawa wanaosema ni chawa, kwanza mimi neno lenyewe chawa linanitia kizunguzungu; maana yake chawa akiingia anaweza akakunyonya zaidi akakuharibia hata maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nasema hawa chawa wasaidie kuifanya nchi iende mbele. Hatutaki kutupasulia nchi yetu, hatutaki. Wote tunawataka wale wanaosifu yale mazuri ambayo yametufikisha hapa kutokea nyuma, na wanaosifu yale mazuri tunayoendelea nayo kwenda mbele. Hatutaki mambo ya ovyo. Nimeongea kama mtu mzima, ninao wajibu wa kupaza sauti kwa Taifa langu kwamba tunapoenda hatuko sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni la kuhusu watumishi. Wengi wamezungumza. Tunaongezea tu kuonesha uzito wa tatizo. Watu wanaoishi maeneo ya pembezoni wana gharama kubwa za kupata huduma kuliko walioko mjini. Inasikitisha, kama ambavyo tumesikia taarifa mbalimbali, nami kwa Jimbo la Nyasa, kwa mfano, katika afya tuna watumishi 206 tu kati ya watumishi 800 wanaohitajita. Ni kama robo tu. Huyu mtumishi ambaye ataweza kuhudumia wale watu wote atakuwa wa aina gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hawa wananchi wanapokosa zile huduma muhimu wanatakiwa wazifuate mbali zaidi ambapo wanakutana na gharama ya nauli, gharama ya mihangaiko na gharama ya vifo. Hili hatuwezi kulivumilia. Kuna baadhi ya maeneo ya mjini humu kuna watumishi wengi. Kwenye shule kwa mfano, watu wanafikia kugawana vipindi, walimu wanne wanagawana kipindi kimoja, yaani somo moja wakati kule hakuna watumishi, kwa sababu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi tumeambiwa kuna ajira karibu 32,000 zitatolewa, lakini zote zitaishia mjini, hazitakwenda huko vijijini. Naomba kama kulikuwa na nia njema ya kusema kwamba tusiwe na ukabila, tuwe tunaajiri centrally, mimi naona hiyo kuajiri kati na yenyewe imeshakuwa ni tatizo, turudi tutafakari. Kuna wakati tulikuwa tunaajiri kupitia Serikali zetu hizi za Mitaa, lakini wengine wakawa kwenye Serikali Kuu. Baadaye tukasema hapana, tuweke mfumo ambao utawezesha wote kulipwa vizuri, pengine umesaidia kidogo, lakini bado matatizo ni mengi. Hivi kweli hata dereva mpaka unataka umwajiri wapi sijui, tumeambiwa hapa kwamba wataangalia utaratibu vizuri. Naona kuna mambo mengine tunaya-complicate pasipo lazima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hali ya mishahara kwa upande wa madereva ni duni sana. Hata madereva wa kwenye Wizara mishahara yao siyo mizuri. Wakati tunapigia kelele mishahara ya watumishi wengine, hao madereva wanakesha usiku kucha. Naomba nao waweze kusaidiwa, waweze nao kupanda mishahara angalau itakayowezesha kupata pension inayoweza kuwasaidia zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende katika suala la kuondoa umasikini na hapo naiangalia TASAF. Hii TASAF tulikoanzia imefanya kazi nzuri, lakini nadhani sasa hivi tuiangalie zaidi. Kwa mawazo yangu ya kufikirika, nilifikiria kwamba pengine tuwachukulie hawa wanafunzi wanaohitimu, kwa mfano, hata ada walilipiwa, wanatakiwa sasa kwenda kufanya kazi, ajira hakuna. Kwa nini hili kundi la TASAF tusiliangalie upya katika kundi hili ambalo halina ajira na lina elimu tayari ya kuweza kufanya kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nafikiria kwamba wanapomaliza kwa mfano JKT kwa wale walioenda, au ambaohawajaenda; pengine tungewatawanya moja kwa moja kwenye maeneo ambayo wanaweza kutoa huduma, lakini wapangiwe angalau fedha ya kuweza kujikimu wakati wakipata zoezi hilo la kufanya kazi na wakati huo huo ikawa wanachangia katika kutoa huduma na kupata uzoefu ili baadaye waweze hata kama ni kujiajiri wenyewe au kuajiriwa lakini angalau wanakuwa wamekaa hapo kwa muda fulani.

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini kama kutakuwa na mfumo rasmi wa kutoa hizo ajira za muda, hasa katika Halmashauri zile ambazo mimi nasema kwamba ni za Ki- TASAF, maana yake kuna Halmashauri hazina mapato ya kutosha na zenyewe ziingie tu kwenye mfumo wa TASAF, ziweze kupewa huo msaada wa watumishi hata hao wa muda waweze kusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, katika kufanya hivyo, naamini kwamba itasaidia hata kuibua mambo mbalimbali yanayowezesha kutoa ajira zaidi. Kwa mfano, kutengeneza vikundi vya kuweza kutoa ajira katika hao wahitimu wa vyuo mbalimbali. Naona pamoja na kwamba tunasema kuna ajira binafsi, lakini ajira hizo binafsi hazijawa na mvuto. Hazijawekewa mfumo ambao unawasaidia. Hata Mungu akibariki, watu wamechangia hapa, pengine mama ikupendeze kutufikiria, watumishi; na hao je? Itawapendeza katika mfumo gani? Watasaidiwa katika mfumo gani? Angalau sisi tuko ndani, tunapata hizo kidogo tulizonazo, hao hawana kabisa na ndio kundi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, huyu mtu ambaye ameelimika, akiamua kuingia kwenye uhalifu anaweza hata kutumia integration katika kufanya uhalifu wake. Anajua hesabu zote, naye anaweza kujua kwamba atapata nini? Kwa hiyo, ni mambo ya hatari kuliacha hili kundi kubwa bila kuwa na hali halisi ya kulisaidia ili liweze kuajirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nasisitiza hayo na nikiomba kwamba rasilimali za Taifa hili siyo la kikundi cha watu au watu wachache. Rasilimali za nchi hii lazima zitumike kwa kadri inavyowezekana, kwa watu wote, kwa usawa unaostahili. Haiwezekani! Kwani mimi kuzaliwa kule kijijini kwangu ndiyo imekuwa nongwa? Nami nifikiriwe, watu wa maeneo ya vijijini wafikiriwe, wasaidiwe, wapunguziwe mateso yaliyopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kama tulivyoanza katika masuala ya Vituo vya Afya, shule, twende zaidi, kuwe na fedha maalum ya kusaidia kuibua mambo mbalimbali ya kiuchumi maeneo hayo ili kuongeza ajira na utumishi ulio rasmi na usio rasmi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)