Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili niweze kuchangia hoja iliyopo mezani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetujalia afya na uhai, pili nitumie fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa sana ambayo ameendelea kuifanya katika ujenzi wa Taifa letu kila kona na tunampongeza sana kwa miongozo yake nasi Wasaidizi wake Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kazi yetu ni kuhakikisha kwamba tunaongeza juhudi katika utekelezaji wa shughuli za TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru sana sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja hii na wale ambao hawakuchangia. Kwanza tuwashukuru sana kwa maoni yao, ushauri wao tumepokea na tutakwenda kuonyesha kwamba tunatekeleza kwa ufanisi wa hali ya juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaongelea maeneo mawili. Eneo la kwanza litakuwa la Afya ya Msingi na eneo la pili la miradi ya maendeleo hususan miradi ya kimkakati na ujenzi wa majengo ya utawala.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika sekta ya afya Waheshimiwa Wabunge wengi zaidi ya asilimia 90 wamechangia kuhusiana na changamoto ya upungufu wa vifaatiba, watumishi hali ambayo imepelekea baadhi ya vituo vilivyokamilika kutoanza kutoa huduma za afya kama ilivyotarajiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika mwaka mmoja wa Serikali hii ya Awamu ya Sita chini ya Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kazi kubwa sana imefanyika ya ujenzi wa vituo vya huduma za afya. Katika mwaka huu jumla ya shilingi bilioni 437 zimetolewa katika ujenzi wa hospitali mpya za Halmashauri 28, vituo vya afya 304 na zahanati 614.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia IMF Serikali imejenga majengo ya wagonjwa wa dharura EMD 80 pamoja na vifaa vyake, ICU 28 pamoja na vifaa nyumba za watumishi 150 za three in one, ununuzi wa magari ya wagonjwa ambulance 195 ambazo zitakwenda kwenye Halmashauri zote 184 pamoja na magari ya usimamizi wa huduma za afya 212.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo kutokana na ujenzi huu tumekuwa na upungufu wa vifaatiba lakini pia na watumishi katika vituo vyetu.

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge Rais wetu na Serikali yetu imesikia kilio cha Waheshimiwa Wabunge na katika mwaka wa fedha ujao Serikali imetenga Shilingi Bilioni 69.95 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba katika hospitali zetu zote za Halmashauri zilizokamilika, zahanati na vituo vya afya. Pia Serikali imeweka mpango wa kuajiri watumishi wa sekta ya afya wa kada mbalimbali, watumishi 7,612 ambao watapelekwa kwenye vituo vyetu vyote vilivyokamilika ili vianze kutoa huduma za afya mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya pili ya Waheshimiwa Wabunge wengi ilikuwa ni changamoto ya ujenzi wa vituo vya afya ambavyo tayari vimeanza ujenzi na kama tutaendelea na ujenzi ama tutaishia hapa katika mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea na ujenzi wa vituo vya afya kwa maana ya ukamilishaji wa majengo ambayo tayari yameanza, ukamilishaji wa maboma pia ukamilishaji wa hospitali za Halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga jumla ya Shilingi Bilioni 40.15 kwa ajili ya ukamilishaji wa hospitali za Halmashauri 59 ambazo ujenzi wake unaendelea na kufanya jumla ya hospitali ambazo zitaendelea na ukamilishaji wake kufikia 102 katika mwaka ujao wa fedha. Pia ukarabati wa hospitali chakavu za Halmashauri 19 utaendelea kufanyika ambapo jumla ya shilingi bilioni 16.55 zimetengwa kwa ajili ya shughuli hiyo, lakini ukamilishaji wa majengo ya maboma ambayo wananchi wetu wametumia nguvu zao na kujenga maboma ambayo yanahitaji ukamilishaji Serikali imetenga shilingi bilioni 15 kwa ajili ya kukamilisha maboma 300.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi huu na ukamilishaji wa majengo haya utazingatia ubora, thamani ya fedha lakini na kuhakikisha kwamba yanakamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja ya uchakavu wa vituo vya afya na zahanati zilizojengwa muda mrefu, zipo zilizojengwa kabla ya uhuru na nyingine baada ya uhuru ambazo zimechakaa sana. Serikali imechukua hoja hii tutafanya tathimini nchini kote kutambua vituo vya afya chakavu na zahanati chakavu na kuviwekea mpango mkakati wa kwenda kuvikarabati ili viweze kutoa huduma bora kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na upungufu wa baadhi ya dawa katika vituo vyetu. Serikali imeweka mwongozo kwamba lazima dawa muhimu katika vituo vyetu zifike angalau asilimia 95 hadi asilimia 100. Ni kweli kumekuwa na upungufu wa baadhi ya dawa katika vituo vyetu lakini Serikali yetu Mheshimiwa Rais katika kipindi cha mwaka mmoja mpaka Februari 2022, tayari amepeleka fedha Shilingi Bilioni 333.8 katika Bohari Kuu ya Madawa (MSD) na taratibu za manunuzi ya dawa hizo zinaendelea. Hali hii itatuwezesha sana kupunguza upungufu wa baadhi ya dawa katika vituo vyetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja kwamba baadhi ya watumishi siyo waaminifu wanapelekea dawa kupotea katika vituo vyetu. Ni kweli Serikali imeendelea kuchukua hatua, mpaka Februari mwaka huu jumla ya Watumishi Wakuu wa Idara na Waganga Wakuu wa Mikoa takribani 14 na watumishi wengine wameshushwa vyeo lakini pia tumeendelea kuchukua hatua za kinidhamu kwa Wakuu wa Idara wote ambao kwa namna moja ama nyingine wameshindwa kusimamia mapato ya Halmashauri, mapato ya vituo na matumizi bora ya dawa. Utaratibu huu ni endelevu, tutaendelea kuchukua hatua ili kuhakikisha tunadhibiti upotevu wa fedha lakini pia dawa katika vituo vyetu vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na mfumo wa GoT-HoMIS ni mfumo ambao umeonesha tukiufunga katika vituo vyetu unaongeza sana mapato katika vituo vyetu kwa zaidi ya mara tatu hadi mara nne lakini pia unadhibiti upotevu na matumizi mabaya ya dawa tumeelekeza halmashauri zetu zote kutenga bajeti ya kuweka na kuhakikisha mifumo ya Got- HoMIS inafanyakazi ili dawa zote zinazokwenda kwenye vituo ziweze kuwa-tract kutoka kuingia mpaka kwenda kutumika kwa wagonjwa wetu lakini pia mapato ya vituo vyetu yaweze kudhibitiwa upotevu wake. Kwa hiyo suala hili tumelizingatia kwa dhati kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la miradi ya maendeleo kuna ujenzi wa majengo ya utawala katika Halmashauri zetu lengo ni kuhakikisha kwamba tunaboresha huduma kwa wananchi lakini na mazingira ya kutoa huduma. Serikali imetenga fedha Bilioni 83 kwa ajili ya ujenzi wa majengo hayo ya utawala lakini miradi ya mikakati itakwenda pia kuhakikisha kwamba tunafanya tathmini na kutoa kipaumbele kwenye maeneo ya vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya ninakushuku sana, nimshukuru sana Mheshimiwa Innocent Bashungwa Waziri wetu kwa ushirikiano na umahiri wake lakini na timu nzima ya TAMISEMI kwa kazi kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)